Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nijikite kidogo tu kwenye sehemu ndogo ya mapato pamoja na udhibiti wa matumizi ya pesa za umma. Kama alivyosema mwenyewe Waziri kwenye ripoti yake ukurasa wa 25 ya kwamba jukumu lake kubwa ni pamoja na kusimamia mapato na matumizi ya Serikali, jukumu hili ni muhimu sana kwa sababu ukisimamia vizuri matumizi na kukawa na cost saving, nayo inakuwa ni sehemu ya mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika uzoefu wangu kwenye Halmashauri zetu, nimeona upotevu mkubwa sana wa pesa kwenye matumizi ambayo sio yaliyolengwa. Waziri amezungumzia kuhusu kuimarisha ukaguzi wa ndani, ukaguzi wa ndani ni kitengo muhimu sana kwenye Halmashauri, lakini ukiangalia nafikiri Wizara ina wataalam wengi wa mambo ya uhasibu, itakuwaje Mkaguzi wa Ndani amkague Mkurugenzi halafu yeye aripoti kwa Mkurugenzi, unategemea hiyo ripoti ya Mkaguzi wa Ndani itakuwa na maana yoyote? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hilo kwa experience tulizonazo huku kwenye Halmashauri zetu. Pesa nyingi zinazokwenda kwenye Halmashauri ambazo ni sehemu kubwa sana ya mapato zinapotea. Kwenye Halmashauri yangu tuna Mkaguzi mzuri sana, ameleta ripoti nzuri sana na bahati nzuri Madiwani wakazifanyia kazi, baada ya kuzifanyia kazi yule Mkaguzi wa Ndani akaonekana kuwa hakutenda jema kwa sababu aliweza kuwaambia Madiwani uovu ambao umekuwa ukifanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haitoshi katika suala la usimamizi, hata yule aliyekuwa Mhasibu wa ile Halmashauri naye alipata matatizo, baada ya kuandika ripoti kuwa tuna matatizo ya matumizi ya pesa alihamishwa kupelekwa kijijini kutoka Halmashauri. Fikiria Serikali imemsomesha mtu kwa kiwango cha CPA, ndiye Mhasibu wa Halmashauri, kwa vile tu ameandika ripoti ambayo inaeleza maovu kwenye Halmashauri anahamishwa ili waendelee kuficha yale maovu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba hiyo Wizara yako kwa vile inasimamia matumizi bora ya hizi rasilimali, iweke hili kama chanzo kimoja wapo cha mapato ya Serikali kwa sababu tukikusanya pesa tena kwa shida kabisa zikaenda kutumika sehemu ambazo hazikulengwa, hayo mapato yote ambayo tunakusanya yanakuwa ni kazi bure. Naomba sana tuimarishe ukaguzi wa ndani. Vilevile, umezungumzia kuhusu Kamati za Ukaguzi kwenye Halmashauri zetu, hizi Kamati za Ukaguzi hatuzioni, ambazo nazo ni chombo muhimu sana cha kusimamia mapato na matumizi ya Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la vyombo vya fedha kusaidia katika kilimo, hasa hii Benki ya Maendeleo ya Kilimo. Wabunge wengi hapa wamechangia kuhusu mtaji mdogo wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo, kuna mchangiaji hapa kaongelea kuhusu shilingi milioni 50 kwa kila kijiji. Sasa nilichokuwa najaribu kuangalia, labda na kuishauri Wizara, kwa nini kama kuna hiki chombo ambacho ni kwa ajili ya kuwasaidia wakulima kikapewa nafasi ya hizi pesa ambazo ni shilingi milioni 50 kwa ajili ya kila kijiji wakapewa, sio lazima iwe mtaji, ila wao wakawa ni wakala wa Serikali kwa sababu hizi pesa nazo ambazo zitakwenda huko ni kwa ajili ya kukopesha wakulima na wajasiriamali wadogo wadogo, kwa hiyo zinahitaji usimamizi mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya Kilimo ni mahala pazuri na itapata nafasi hata ya kuweza kujitanua kwenda mahali mbalimbali hapa Tanzania. Ningeomba hizi milioni hamsini hizo hata shilingi bilioni 60 ambazo sasa hivi zimezungumziwa kuwa zitatolewa mwaka huu pamoja na zile shilingi bilioni 52 ingepewa Benki ya Kilimo ili iweze kuanza kufanyia kazi zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni masoko kwa ajili ya wakulima. Kuna chombo ambacho kilikuwa kinazungumzwa kuwa kingeanzishwa (commodity exchange), sijaiona katika hii report labda kwa ajili yakuangalia haraka kama imezungumziwa, lakini kwa wakulima hiki ni chombo muhimu sana. Wakulima wetu wanalima sana na wakati wa mavuno bei zinakuwa chini, tungekuwa na chombo kama hiki kingetusaidia sana kuhakikisha kuwa bei za mazao yetu zinakuwa stable.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni Msajili wa Hazina. Naomba sana tena sana Wizara ijaribu kuimarisha hiki kitengo cha Msajili wa Hazina vilevile wapewe bajeti ya kutosha. Kwa sababu kwa mchango wao mwaka huu wa shilingi bilioni 500 mpaka mwezi Machi, nina imani kuwa ingekuwa mara mbili au mara tatu zaidi kama wangepata nafasi ya kusimamia haya Mashirika yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili ya muda kumalizia ni suala la deposits zilizochukuliwa na Serikali kutoka kwenye mabenki kupelekwa Benki Kuu. Jana jioni nilikuwa namsikiliza Mkurugenzi wa Benki ya Mkombozi akielezea kuwa Benki zimepata matatizo baada ya Serikali kuondoa zile deposits kutoka kwenye Benki za Biashara na kuzipeleka Benki Kuu.

Sasa lile lilinishtua kidogo kuwa inawezakana labda hayakuwa maksudi ya Serikali, lakini kwa kuondoa zile deposits zilipunguza ukwasi (liquidity) kwenye haya Mabenki. Labda nalo ningeiomba Serikali ijaribu kuangalia kwasababu nia na madhumuni ni namna gani tunaweza kuzisaidia hizi Benki ziweze kuwakopesha wakulima, ziweze kwenda vijijini, kuwe na a real financial inclusion. Kwa hiyo, naomba sana tena sana tuangalie kurudi nyuma wakati mwingine siyo vibaya kama tutafanya marekebisho ambayo yatasaidia kwa ajili ya uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nashukuru sana. Naunga mkono hoja.