Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Mchungaji Peter Msigwa kwa hotuba yake nzuri iliyosheheni weledi na busara. Aidha, nampongeza Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, kwa jitihada kubwa anazozifanya katika kuleta mabadiliko ya kiutendaji katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhusiano wa Tanzania na mataifa mengine duniani ni sharti uendane na utii wa Serikali yetu kwenye mikataba ya kimataifa. Mwaka 2016 Bunge la Kumi na Moja katika mikutano mbalimbali pamoja na mambo mengine lilipitisha Sheria ya Huduma ya Habari (Media Services Act of 2016) na Sheria ya Upatikanaji wa Habari (The Access to Information Act, 2016). Serikali ilieleza hapa Bungeni kwamba utungwaji wa Sheria ya Upatikanaji wa Taarifa au wengine wanaita The Access to Information Act kuwa utoaji wa taarifa siyo tena jambo la hiari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hizo mbili hazikidhi matarajio ya wananchi na zimesheheni maneno matamu lakini yakiwa hayatekelezeki. Kinyume na matarajio ya wengi, sheria hazioneshi kwamba kutakuwa mwarubaini wa ukiritimba wa mamlaka za Serikali katika kutoa taarifa. Hii ni kwa kuwa zimepingana na dhana ya haki ya kupata taarifa na zimezika haki ya kikatiba ya raia kupata taarifa. Badala ya kusaidia wananchi kupata habari, sheria hizo zilizotungwa zitatumika kama kichaka cha kuficha udhaifu wa viongozi wasio waadilifu na zinaweza zikatumika hata kufungia baadhi ya vyombo vya habari. Hii ni kwa sababu ndani ya sheria hizo kumewekwa vifungu vinavyompa mamlaka mwenye taarifa kutotoa taarifa alizonazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha 6(3) cha Sheria ya Haki ya Kupata Taarifa kimetaja mambo ya Usalama wa Taifa yasiyopaswa kutolewa kuwa ni taarifa ya nchi au Serikali ya kigeni inayohusiana na Usalama wa Taifa na uhusiano wa mambo ya nje au shughuli za mambo ya nje yakiwemo masuala ya kisayansi na teknolojia yanayohusiana na Usalama wa Taifa, mathalani, taarifa juu ya ununuzi wa rada; udhaifu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU); uuzaji wa hati fungani za Serikali kwa benki ya Stanbic na unyonyaji kwenye mikataba ya madini na gesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, udhaifu wa TAKUKURU uliripotiwa na mtandao mashuhuri wa WikiLeaks. Ulimnukuu aliyekuwa Balozi wa Marekani nchini, Michael Retzer akisema, Edward Hoseah ambaye kipindi hicho alikuwa Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU alizuiwa na bosi wake, Rais Jakaya Kikwete, kuwashtaki vigogo wa wizi wa fedha za EPA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uuzaji wa hati fungani uliibuliwa na Taasisi ya Uchunguzi wa Makosa Makubwa ya Ufisadi ya Uingereza (SFO). Kiasi cha shilingi trilioni 1.3 zimedaiwa kupotea katika sakata hilo. Kifungu cha 5(3) cha sheria kimetaja taarifa ambazo hazipaswi kutolewa ni upelelezi unaofanywa na vyombo vya uchunguzi, faragha binafsi na taarifa za Usalama wa Taifa lakini nani asiyejua udhaifu wa vyombo vya uchunguzi? Vingi vinatuhumiwa kubebana kwa njia ya upendeleo au rushwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria mpya ya Upatikanaji wa Taarifa imerejesha kwa mlango wa nyuma sheria katili ya magazeti (Newspaper Act ya mwaka 1976) na ndivyo ilivyotarajiwa pia kwenye mikataba. Taifa hili limenyonywa kwa miaka mingi na limekumbwa na migogoro lukuki inayotokana na kuwapo mikataba iliyofungwa kinyemela na watendaji wa Serikali. Wengi walitarajia kuwa mikataba hiyo ingekuwa wazi angalau kwa Bunge, mambo mengi yangekuwa tofauti na yalivyo sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Azimio la Ulimwengu la Haki za Binadamu, Ibara ya 19; Ibara ya 19 ya Mkataba wa Haki za Kijamii na Kisiasa wa mwaka 1966 (ICCPR), Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu wa 1981 na kifungu cha 18 cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 1977 kinatoa uhuru wa maoni bila kikwazo cha aina yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kilio hiki cha Wabunge na wananchi hakijasikilizwa na hivyo kinaishia kuipaka matope Jamhuri ya Muungano mbele ya macho ya kimataifa. Baada ya Serikali na Bunge kutunga sheria hizi zinazoratibu shughuli za waandishi wa habari nchini, je, Wizara haioni kuwa sheria hizo zinaharibu taswira ya nchi yetu kimataifa?

Je, Serikali haioni haja ya kuwahusisha wadau wa habari ili kuanza kufanyia kazi malalamiko yao na hatimaye kuleta muswada ili sheria hizo zifanyiwe marekebisho?

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Ubalozi wetu kule Washington DC kumepatikana taarifa kuwa kumelipwa kiasi cha dola za Marekani milioni 1.05 (karibu shilingi bilioni 2.4), kwa mwanamke aliyepelekwa nchini humo kuwa mtumishi wa nyumbani wa Afisa wetu wa Ubalozi, Dkt. Allan Mzengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyombo vya habari vimenukuu taarifa kutoka Ubalozi wa Tanzania mjini Washington DC zinasema, Serikali ililipa kiasi hicho cha fedha kwa makosa binafsi yaliyofanywa na Dkt. Allan Mzengi na alituhumiwa kumsafirisha kinyume cha sheria hadi nchini Marekani Bi. Zipora Mazengo. Dkt. Mzengi alishtakiwa kumfanyisha kazi kwa saa 15 kila siku na kushindwa kumrejesha nchini kwa miaka minne hata pale alipofiwa na ndugu yake Bi. Zipora Mazengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chini ya sheria za Marekani, upelekaji mtu yeyote (mwanamke au mwanaume) kutoka eneo moja hadi lingine kwa shabaha ya kumtumikisha linakuwa ni kosa baya sana nchini humo la usafirishaji haramu wa binadamu (human trafficking offence). Aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Bi. Mwanaidi Maajar ananukuliwa akieleza wasiwasi wa kuharibika uhusiano kati ya nchi hizi mbili wakati akiwasiliana na Sanze Salula, aliyekuwa Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barua ya Balozi Maajar kwa Salula yenye Kumb. Na. WEPC.179/53 ya tarehe 4 Februari, 2011 ilinakiliwa pia kwa aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi Philemon Luhanjo na aliyekuwa Katibu wa Rais Prosper Mbena. Alisema ingawa kwa sasa Serikali ya Marekani imeonyesha karidhika kutokana na Mawakili wa Bi. Zipora kupunguza deni na Dkt. Mzengi kukubali kuanza kulipa kwa awamu, suala hili litabaki kuwa tete kutokana na hatua ya Mawakili wa Bi. Zipora kupinga utaratibu wa kulipa. Balozi Maajar anasema Mawakili hao wameanza tena kampeni za kuichafua Tanzania katika Congress, pamoja na kuishinikiza tena Serikali ya Marekani ili nayo iishinikize Serikali yetu kulipwa deni hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, akiandika kwa njia ya tahadhari, Balozi Maajar alieleza Sheria ya Kupambana na Usafirishaji Haramu wa Watu ya Marekani ina kipengele kinachoipa mamlaka Congress kuiamuru Serikali kusimamisha misaada kwa nchi ambayo imethibitika kuvunja sheria hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kupata maelezo ya Waziri kama fedha hizo zimeshalipwa zote ili kuiondolea nchi yetu aibu katika nyanja za kimataifa na kuyumbisha uhusiano kati ya Tanzania na Marekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, naomba maelezo ya Waziri kuwa ni hatua gani za kinidhamu alizochukuliwa Dkt. Mzengi kutokana na kosa alilolifanya ambalo limeiaibisha Tanzania mbele ya nchi wahisani? Tatu, Serikali inachukua tahadhari gani ili kuzuia kosa kama hili lililofanywa na Dkt. Mzengi lisijirudie tena?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii na naomba kuwasilisha.