Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze mchango wangu kwa maandishi kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kufanya kazi hii ya kuwawakilisha wapiga kura wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upimaji ardhi, ili kuiona Tanzania ya viwanda ni lazima upimaji wa ardhi upewe umuhimu wa kutosha. Kwani hivi sasa uwekezaji wa mashamba makubwa ni mgumu sana kwani vijiji vingi hivi sasa bado havijaingia kwenye mpango wa matumizi bora ya ardhi. Jambo linalofanya Halmashauri kukosa wawekezaji kwenye mashamba makubwa ya mazao ya kilimo na ufugaji wa kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano katika Halmashauri ya Liwale yuko Mwekezaji mmoja toka Japan. Huyu ni mzaliwa wa Liwale, mwaka 2015 aliamua kurudi nyumbani na mradi wa kilimo cha alizeti lakini hadi leo anahangaika kupata shamba japo Halmashauri ilishafanya maamuzi ya kumpatia ardhi mwekezaji huyu mzawa. Hatua ya uhaulishaji ardhi ndio kikwazo kikuu kilichobakia katika kukamilisha mradi huu. Namwomba Mheshimiwa Waziri, mwenye dhamana kuhakikisha Mwekezaji huyu anapata ardhi kwa ustawi wa Wanaliwale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali isiziachie Halmashauri shughuli za upimaji wa Vijiji ili kuviingiza katika matumizi bora ya ardhi. Kwani Halmashauri nyingi hazina mapato ya kutosha kumudu kazi hii. Hivyo kuvifanya vijiji vingi kukosa wawekezaji, kwani kigezo cha kwanza cha uwekezaji vijijini ni kijiji kuwa na matumizi bora ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhaba wa watumishi, Wizara hii ina tatizo kubwa sana la upungufu wa watumishi hasa kwenye Halmashauri zetu. Jambo hili linaongeza makazi holela katika Halmashauri nyingi kutokana na uhaba wa viwanja na Halmashauri kushindwa kupima viwanja kwa wakati na jambo linaloongeza rushwa kwa ugawaji wa viwanja na makazi yasiyopimwa. Mfano, katika Halmashauri ya Liwale hatuna Afisa Ardhi mwenye taaluma ya kutosha na hatuna wapimaji wa ardhi tunategemea toka katika Halmashauri ya Nachingwea. Jambo hili linafanya gharama kubwa za upimaji wa viwanja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Gereza la Liwale limechukua ardhi ya wananchi tangu mwaka 1982 lakini hadi leo wananchi wenye mashamba yaliyotwaliwa bado hawajalipwa fidia ya mashamba yao. Naomba Wizara ya Ardhi wakishirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani wamalize mgogoro huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile mgogoro wa mpaka kati ya wanakijiji cha Kikulyungu na Wizara ya Maliasili na Utalii. Ni bora sasa Wizara zote mbili wakashirikiana katika kutatua mgogoro huu. Mgogoro wa Kikulyungu na hifadhi ya Selous ni wa muda mrefu sana.