Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niunge mkono tu haya yote ambayo yamezungumzwa. Mipango ni mizuri sana, tunapanga vizuri sana lakini tatizo letu kubwa ni utekelezaji na utekelezaji umezorota kwa sababu fedha haziendi Mikoani, fedha haziendi Wilayani. TRA wanajitahidi sana kukusanya mapato, wanakusanya sana, lakini fedha haziendi kwenye Halmashauri, haziendi Mikoani; miradi mingi imekwama na tunategemea sana wafadhili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nadhani wakati umefika sasa wa kupunguza hii misaada, kwa sababu tukitegemea sana wafadhili ipo siku wafadhili watasema sasa sisi tunajiondoa, Kwa hiyo, tujitahidi sana kutumia fedha zetu za ndani. Miradi mingi imekwama, kwa mfano katika Jimbo langu la Mpwapwa kuna barabara hii ya kutoka Mbande, kwenda Kongwa mpaka Mpwapwa. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi kwamba ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami umeshaanza tayari, lakini bado wapo kipande cha Mbande hawajafika hata njia panda ya Kongwa.

Kwa hiyo, mimi ni mategemeo yangu kwamba wananchi wa Jimbo la Mpwapwa wategemee kwamba barabara hii itakamilika kwa wakati, kuanzia Mbande - Kongwa mpaka Mpwapwa kwa kiwango cha lami, naisubiri kwa hamu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu misamaha ya kodi. Ni kweli kisheria inaruhusu kwamba baadhi ya wafanyabiashara wasamehewe kodi, lakini hii inatupotezea mapato mengi sana. Ninaishauri Serikali kwamba ipunguze misamaha ili fedha nyingi zikusanywe ziende katika miradi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukusanyaji wa kodi ya majengo kwenye Halmashauri zetu. Tulishaishauri Serikali kwamba utaratibu huu kwa kweli ni mgumu sana. Halmashauri nyingi zilikuwa zinakusanya kodi ya majengo vizuri sana, hii property tax.

Kuna Halmashauri ambazo zinaweza zisitegemee hata ruzuku ya Serikali kwa kutegemea mapato yao ya ndani (own source). Kwa mfano Halmashauri za Jiji la Dar es Salaam walikuwa wanajitahidi sana kukusanya property tax, lakini baadaye Serikali ikaamua kwamba inakusanya yenyewe. Sasa Mheshimiwa Waziri naomba taarifa, ni kiasi gani kimeshakusanywa na kiasi gani kimesharudishwa kwenye hizi halmashauri zetu. Tulikwishakataa jambo hili; tuachie halmashauri zenyewe zikusanye kwa sababu property tax ni chanzo kimoja wapo cha mapato ya ndani kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maghala yetu ya hifadhi ya chakula cha msaada. Kila mwaka tunatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa maghala na Serikali imenunua chakula kingi sana cha akiba, lakini jambo la kushangaza ukame unaendelea katika nchi yetu chakula hawagawi, njaa inaendelea hasa katika Jimbo langu la Mpwapwa na Mkoa wa Dodoma kwa ujumla. Hali ni mbaya sana. Watu hawana chakula, sasa hivi wameanza kuandaa mashamba yao lakini hakuna chakula; kwa nini Serikali isianze kugawa chakula cha msaada?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatusemi kwamba kuna njaa maana Serikali inazuia neno la njaa, inasema upungufu wa chakula, lakini mimi nadhani upungufu wa chakula na njaa ni neno lilelile tu. Kwa hiyo, hakuna haja ya kuhifadhi chakula kwenye maghala na chakula kinaharibika. Serikali ianze kugawa chakula maeneo yote ambayo yana upungufu wa chakula au yana njaa, chakula kitaharibika kwenye maghala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Ujenzi wa Vituo vya Afya Jimbo la Mpwapwa. Ninashukuru sana Kituo cha Afya Mima kimepata shilingi milioni mia tano safari hii, lakini bado Kituo cha Afya cha Mbori hakijakamilika. Ninaomba sana fedha itolewe, vituo vikamilike ili huduma iweze kutolewa kwa maeneo yale. Vituo vya afya vinasaidia sana hasa wale akina mama wajawazito badala ya kupelekwa Hospitali ya Wilaya ya Mpwapwa wanahudumiwa kwenye vituo vya afya kwa sababu pale kuna Assistant Medical Officer au Clinical Officer ambao wale ni trained au wale madaktari wasaidizi wanakuwepo kwenye vituo vya afya kwa ajili ya operation ndogo ndogo. Kama akina mama wanashindwa kujifungua basi wanafanyiwa operation ndogo ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ya kwangu yalikuwa ni hayo; nikushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono asilimia mia moja hoja hii ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha, lakini tukusanye fedha na tutekeleze miradi. Fedha ipelekwe halmashauri na mikoani. Ahsante sana.