Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nipate nafasi ya kuchangia Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana Serikali kwa kuleta mpango mzuri na nishukuru sana Serikali kwa miradi ambayo imeanza kutekelezwa kwenye maeneo ya Jimbo langu na Mkoa wa Katavi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianzie na suala la kilimo. Mikoa ya Ruvuma, Njombe, Iringa, Rukwa, Katavi na Songwe ni mikoa ambayo inategemea sana kilimo cha mazao ya mahindi na mpunga, kwa ujumla ni wazalishaji wa nafaka ambao wanalisha sehemu ya nchi yetu kwa ujumla. Kwa bahati mbaya sana mikoa hii imepata balaa kwa sababu ya kuzalisha hizo nafaka ambazo kimsingi zinasaidia maeneo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo tunaona kwa mikoa hii tuna balaa ni kwamba Serikali ilipiga marufuku kuuza mazao ya aina ya nafaka kwa maana ya mahindi na mpunga kuuza nje ya nchi jambo ambalo kwa sasa linawatesa sana Watanzania wa mikoa hiyo. Ninaiomba sana Serikali ifike mahali sasa waangalie kwamba kuchagua zao la mahindi kulima si sehemu ya adhabu kwa wananchi wa mikoa hiyo, kwa sababu wananchi wanajitegemea, wanafanya shughuli za kilimo kwa kujituma sana, wamezalisha kwa kiwango cha juu mpaka wamepata ziada na matokeo yake eneo hilo mkulima hanufaiki na kitu chochote na inaonekana kwamba mkulima wa zao la mahindi hana thamani kubwa kwa sababu zao hilo halina soko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie Serikali wasipochukua umuhimu wa aina yake wa kuangalia kutatua tatizo la ukosefu wa soko la mazao hayo wananchi hawatafanya shughuli za uzalishaji na mwakani kunaweza kukajitokeza njaa kubwa sana kwa sababu wanaona watalima kilimo cha kujikimu wao na familia zao tu. Ni vema Serikali lile katazo ambalo waliliweka wakaliondoa ili liweze kuwasaidia wananchi waweze kufanya shughuli zao. Sasa hivi wakulima watoto wao hawaendi shule, hawana uwezo wa kufanya shughuli za maendeleo kwa sababu mazao yako ndani, Serikali hakuna ilichowasaidia na ukizingatia mkulima huyu katumia nguvu zake zote kwake yeye binafsi na wala Serikali haikumsaidia kitu chochote. Kwa hiyo, naomba mliangalie hili na muone ni jinsi gani mnawasaidia wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie zao la tumbaku. Mkoani kwangu wakulima wanazalisha zao la tumbaku, lakini si mkoa wa Katavi tu na mikoa jirani ya Tabora, Mbeya, Kigoma, Kahama kwa maana ya mkoa wa Shinyanga wanalima zao la tumbaku na Mikoa mingineyo. Wakulima walizalisha zao la tumbaku wakajituma, wamefanya shughuli njema wamezalisha lakini zao lile halina soko mpaka sasa na tumbaku yao iko ndani. Niombe sana Serikali wasiliangalie jambo hili kama ni jambo ambalo ni dogo, ifike mahali Serikali waangalie umuhimu wa kusimamia mazao mengine kama walivyosimamia korosho, walivyosimamia kahawa na mazao mengine kama pamba, walipe kipaumbele zao hili, kwa sababu ndiyo zao lililokuwa linaongoza kwa uzalishaji mkubwa na kuingiza kipato kwa Taifa letu.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao hili limesaidia sehemu za Halmashauri ambazo wanazalisha zilikuwa na kipato kizuri kuliko ilivyo sasa, ni vema sasa Serikali ikaona umuhimu wa kulisimamia zao hili ili na wao waweze kunufaika kama mazao mengine yalivyosimamiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie jitihada za Serikali zilizofanywa hasa kupeleka umeme vijijini. Niipongeze Serikali kwa juhudi ambazo zimefanyika lakini niombe sasa Serikali ielekeze nguvu sana kuhakikisha ile miradi ya umeme Phase III inafanyiwa kazi na inasambazwa kwenye maeneo husika. Jimboni kwangu nina vijiji 32 ambavyo vipo kwenye mpango. Mpaka sasa bado hata kijiji kimoja hakijafanyiwa kazi kwa sababu umeme uliokuwa umepangwa kuanza Phase III bado. Ulioanza kufanyiwa kazi ni ule ambao ulikuwa wa mpango wa Orion ambao vijiji vitano wamepata, tunaishukuru na kuipongeza Serikali. Pia tunaomba maeneo mengine ambayo yalibaki yaweze kufanyiwa haraka na kuweza kufanya shughuli za maendeleo yatakayowasaidia sana wananchi kwenye eneo la Jimbo langu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo tetesi kuwa mradi huu umekwama kwa ajili ya kushindwa kuelewana kati ya wakandarasi, ninaiomba Serikali iingilie zoezi zima la kukamilisha utaratibu ambao ni wa kisheria ili waweze kuwaruhusu wakandarasi waweze kufanya kazi yao kwenye mikoa ambayo walikuwa wameelekezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la elimu. Niipongeze Serikali kwa jitihada ambazo zimefanywa kwa kupata idadi kubwa ya watoto ambao wanafaulu. Inaonesha Serikali imeangalia mfumo mzima na kuuthamini nzima hasa ya sekta ya elimu. Tunalo tatizo kubwa sana, tuna idadi ya wanafunzi ambao wamefaulu na wamekosa vyuo vya kwenda kusoma. Niombe sana Serikali iweke mazingira ya haraka kuhakikisha wale wanafunzi ambao wamefaulu wapewe nafasi kwenye vyuo ili waweze kuanza masomo ya kwao katika vyuo ambavyo wameomba. Na tuiombe Serikali, zile tofauti zinazojitokeza, zinazowafanya watoto washindwe kufika kwenye maeneo husika ya vyuo wazitoe ili waweze kuratibu haraka, watoto waanze kupata masomo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna maeneo kwenye suala hili la elimu hasa maeneo ya jimboni kwangu. Tunayo majengo mengi ambayo yameanzishwa, tunaomba sana Serikali ielekeze nguvu kusaidia yale majengo ambayo yameanzishwa na Halmashauri na Halmashauri zikawa hazina uwezo hasa yale yaliyoanzishwa na wananchi wenyewe kwa kujitolea. Serikali ielekeze nguvu kusaidia maeneo hayo ili kuweza kumudu ufaulu wa wanafunzi walio wengi kwenye maeneo husika ambayo ni kwenye eneo la shule za msingi, eneo la shule za sekondari, kote huko kunahitaji kukamilisha yale majengo ambayo yameanzishwa na wananchi kwa jitihada zao binafsi, lakini uwezo wa Halmashauri wa kuweza kuhudumia nguvu za wananchi ukweli bado hazijakuwa kubwa za kutosha. Kwa hiyo, tunaomba na maeneo haya Serikali ieleleze nguvu kuhakikisha miradi hii inasimamiwa na inafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kwenye eneo la afya. Tunaipongeza Serikali kwamba huduma za dawa kwa sasa zinapatikana, lakini bado tuna changamoto kubwa sana hasa pale sera ya Serikali ilipokuwa imezungumza kwamba kila kijiji kiwe na zahanati. Vijiji vingi vimejitokeza, wananchi wameweza kujenga majengo mengi na wameandaa utaratibu wa kuanzisha majengo ya zahanati lakini majengo yale bado hayajakamilika.

Kwa hiyo, tunaomba Serikali itenge fedha za kutosha kuhakikisha nguvu za wananchi ambazo wamejitolea waweze kupewa nafasi ya kukamilisha yale majengo. Naamini tukifanya hivyo tutakuwa tumewasaidia sana Watanzania hasa wa maeneo ya vijijini, ambako bado huduma za afya zinahitajika kwa karibu sana ili kuweza kuwasaidia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni sekta ya maji. Kwenye eneo la sekta ya maji Serikali inajitahidi kufanya kazi yake vizuri, lakini kwa ukubwa wa nchi yetu bado tunahitaji miradi ya maji kwa kiwango kikubwa sana. Niombe sana Mkoa wa Katavi ambao upo unategemea sana kupata maji kutoka kwenye chanzo cha Bwawa la Milala bado hautoshelezi. Kwa hiyo, tulikuwa tunaomba maji yapelekwe, hasa tunahitaji mradi mkubwa wa kutoka Ziwa Tanganyika ambao utapeleka maji kwenye Makao Makuu ya Mkoa wa Katavi, lakini utasaidia kwenye maeneo mengine ya maeneo husika ya Jimbo la Mpanda Vijijini. Kwa hiyo, niiombe Serikali iharakishe kuweka mpango mkubwa wa maji ambao utasaidia kutoa kero ya maji ndani ya Mkoa wa Katavi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naiomba sana Serikali, Mkoa wa Katavi hauna hospitali ya Mkoa. Tunaomba Serikali iweze kutenga fedha za kutosha kujenga hospitali ya Mkoa sambamba na hospitali ya Wilaya mpya ya Tanganyika ambayo bado haijaanza kujengwa. Tunategemea sana Serikali itafanya hayo, ili kuweza kuwasaidia wananchi wa Mkoa wa Katavi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Ahsante.