Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ili na mimi niweze kujadili na kutoa mchango wangu katika hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango kuhusiana na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2018/2019 na Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Wasaidizi wake kwa kuja kwa wakati na mpango mzuri wa mapendekezo haya. Mimi katika kuchangia niseme tu kwamba vipaumbele ambavyo vimewekwa na Serikali katika miradi ambayo itapewa kipaumbele, nami nipendekeze kwamba suala zima la ujenzi wa Mji Mkuu wa nchi yetu wa Dodoma liwekwe katika mipango ya Serikali, jambo hili liwe la kudumu, ili kwamba kwa sababu huko mbele hatuna mpango mwingine tena wa kuja kuhamisha Makao Makuu ya nchi yetu kutoka hapa tulipo Dodoma kwenda sehemu nyingine, basi maandalizi yawepo ya Serikali ya muda mrefu ya kuhakikisha kwamba Mji huu unapangwa vizuri. Mji huu uje uakisi Tanzania mpya ambayo tunaitarajia kuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, ninaiomba sana Serikali ije na mpango mkakati kabambe kabisa wa kuhakikisha kwamba Mji huu unapimwa, unawekewa miundombinu yake halisi ambayo ita-reflect uwepo wa Dodoma mpya, Dodoma ambayo itakuwa na miundombinu mizuri ya zile gari ambazo zinaendeshwa kwa umeme hapa Dodoma, flyovers ambazo tunaziona kwenye nchi za wenzetu zijengwe Dodoma, Dodoma hii iwe na uwanja wa ndege ambao ni wa kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo niombe Serikali iliangalie eneo la uwanja wa ndege la Msalato kama eneo lenyewe linaweza lisiwe kubwa sana basi Serikali ione uwezekano wa kupanua eneo hilo ili kusudi tuepukane na uwezekano wa baadae kuja kuanza kubomolea watu, kufidia watu na kuwahamisha katika miaka mingine ijayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema haya nikijua kabisa kwamba nchi hii ni yetu wote na kwa maana hiyo tufikiri sana, niombe sana kwamba yale maeneo ambayo yanatengwa kwa ajili ya ujengaji wa viwanda katika maeneo mbalimbali ya nchi hii, hata maeneo Maalum kama strategic cities au satellite cities kama kule Kigamboni inavyofanyika kule Dar es Salaam, na hapa Dodoma mipango hiyo iwepo, tusije tukachelewa tukaja tukafika mahali sasa tukajikuta kwamba sasa tunapotaka kujaribu kufanya master plan nyingine mpya tunaanza kujikuta tupo kwenye crisis. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali yangu iwe makini kabisa katika kuhakikisha kwamba tunapokwenda na mipango hii mizuri, ujenzi wa miundombinu ya umeme, kwa mfano hiyo Stiegler’s Gorge kwa maana hiyo tuna uhakika wa kuja kupata umeme wa kutosha na Tanzania ya viwanda inaelekea kuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningependa kusema ni kuhusiana na kuiomba Serikali ijiandae kuweka taratibu nzuri kwa ajili ya ujenzi wa Makao Makuu ya Mikoa na Wilaya mpya, kuna maeneo mengi watu wanakaa kwenye majumba ambayo kwa kweli hayastahili. Kwa mfano, katika Halmashauri yangu ya Mbogwe, Ofisi ya Halmashauri ni jengo ambalo lilikuwa guest house zamani, sasa ukiangalia kwa kweli haikubaliki. Niombe kwa kweli Serikali ifanye utaratibu iweke katika mipango yake kuhakikisha kwamba maeneo kama haya mapya yanapata ofisi na nyumba za wafanyakazi ambazo zinalingana na hadhi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ningependa pia kuishauri Serikali ni kuhusiana na viwanda vya mbolea. Nchi hii ni nchi inayotegemea kilimo kwa kiasi kikubwa na bahati nzuri Serikali yetu na nchi yetu imejaliwa kupata gesi ambayo ni malighafi nzuri ya kuweza kutumika katika ujenzi wa viwanda vya mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali jambo hili iliangalie na ilione kwamba ni jambo la msingi, iwa- encourage watu wanaoweza kuja kuwekeza katika sekta hii ya viwanda vya mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbolea inatumika katika mazao yote; mazao ya chakula na mazao ya biashara yanategemea sana mbolea, Sasa mbolea ikipatikana kwa bei rahisi maana yake uzalishaji utakuwa ni wa hali ya juu na uzalishaji ukishakuwa mzuri maana yake sasa hata hiyo Tanzania ya viwanda ambayo itakuwa inahitaji malighafi kutoka kwa wakulima itashamiri kwa wepesi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo ninaunga mkono hoja zote ambazo zimeletwa na Serikali za kuhakikisha kwamba tunakamilisha ujenzi wa viwanda hivyo vya makaa ya mawe, kufua chuma kule Liganga na ujenzi wa reli ya kati kwa standard gauge, ni ukombozi na zaidi niiombe Serikali iendelee na upanuzi wa bandari zote zilizopo kule Tanga, Bagamoyo, Dar es Salaam pamoja na kule Mtwara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtwara kuna bandari moja nzuri sana, Kamati yetu ilitembelea kule, ile bandari nadhani Mungu aliiumba pamoja na ile Dar es Salaam kwa sababu namna ambavyo Bandari ya Mtwara ilivyokaa imekaa sawa sawa na Bandari ya Dar es Salaam, hiyo ni ishara kwamba Mungu anaendelea kutupenda na hivi ni vitu ambavyo anatujaalia tuvitumie katika kuhakikisha kwamba nchi yetu inaanza kuwa ni center ya maendeleo kwa nchi nyingine za jirani zinazotutegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mungu aibariki Serikali yetu na Mungu awabariki wote mlionisikiliza. Ahsante sana.