Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa jinsi anavyoongoza nchi hii, lakini pia na Baraza zima la Mawaziri, tunawaomba nendeni mkamwambie Mheshimiwa Rais asilegeze uzi. Nchi yetu hii inahitaji mwendo wa Rais sasa, si lelemama na maneno mzahamzaha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaanza na hatua ya kwanza kumuomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, naomba mfumo wetu wa ukusanyaji wa mapato utazamwe. Nchi yetu bila mapato ya kutosha kutoka ndani ya nchi hatuwezi kufika mahali popote. Sasa hivi mfumo unaotumika unagandamiza sana wale walipakodi kulingana na mfumo na utaratibu unaotumika. Mimi ninaomba basi, tufanye utaratibu wa Serikali kutazama upya mfumo mzima wa ukusanyaji wa mapato yetu ya Serikali ili walau walipakodi wawe marafiki wa Serikali na wavae moyo wa uzalendo katika kulipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kutazama upya ahadi za Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Rais ameahidi mambo mengi sana na kama hatutaweka kwenye utaratibu ule wa kawaida wa kuangalia ni namna gani zile ahadi zake zinaanza kutekelezwa kwa awamu kila mwaka ili ziweze kuingia kwenye mfumo wa bajeti ya Serikali, hatuwezi kufika mahali popote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo. mimi naona kama kule kwetu Mbulu ahadi zote alizoahidi bado hazijatekelezwa, tunandelea kusubiri Serikali itekeleze kwa sababu tayari viashiria vimeonekana. Naipongeza Serikali kwa jinsi ambavyo tayari wametangaza tenda ya Daraja la Magara na mwaka huu wa fedha ambao tuko nao watatekeleza ahadi hiyo ya Rais ili kujibu kiu na matarajio ya wananchi wa Mbulu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu barabara ya lami aliyoahidi kule Mjini Mbulu, naona tender pia imetangazwa. Tunaishukuru sana Serikali kwa jinsi ambavyo tender ya ahadi ya Rais kilometa tano pale Mjini Mbulu imetangazwa, na ni imani yangu kuwa itatekelezwa katika mwaka huu wa bajeti kwa kadri ambavyo imetangazwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, humu ndani tunaweza kuzungumza mambo mengi sana, lakini bila pesa, bila nchi kuwa na uchumi, hata tukiongea namna gani mafanikio yetu hayatafika mahali popote. Kwa hiyo, katika eneo hili la ahadi za Mheshimiwa Rais, ni imani yangu kuanzia mwaka huu wa fedha tunaouendea kila mahali pataguswa ili iingie kwenye mfumo wa utekelezaji wa bajeti ya Serikali na iweze kutekelezwa. Mheshimiwa Rais ameahidi mambo mengi na kwa kadri alivyoahidi si rahisi kutekeleza kwa mwaka mmoja, lakini kwa kuwa Serikali ni endelevu na ina miaka mitano, ni imani yangu itatekeleza ahadi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwa kadri walivyoongelea kilio kikubwa cha bei ya mazao ya wananchi. Kwa sasa wananchi wanahangaika kutafuta masoko yao. Tuone Serikali itumie wataalam na mifumo mbalimbali na marafiki zetu ili kuona ni namna gani tunapata bei nzuri ya mazao ya wananchi ikiwemo mifugo na mazao yanayotokana na kilimo ili kuwezesha mwananchi wa chini kupata uchumi unaoweza kumudu mahitaji na matarajio ya nchi na katika kujihudumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ninapenda nizungumze kwa ufupi sana kutokana na muda ni eneo la miradi ya maendeleo. Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, alianzisha mpango kabambe wa ujenzi wa maabara katika Halmashauri mbalimbali nchini. Hivi sasa bado baadhi ya maeneo mengi kwenye ujenzi wa zile maabara hakujakamilika na wananchi wamechanga vya kutosha. Tunaomba fedha hizi za ukamilishaji wa maeneo ya viporo ya maendeleo zingeweza kutafutwa kwa kila mwaka kwa awamu ili miradi ile ya maabara iweze kutekelezwa na iweze kufanya vizuri kwa maana ya kuwahudumia wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili la elimu tunaomba Wizara ya Elimu iangalie upya mfumo wa wakaguzi wa elimu katika nchi yetu. Wakaguzi wetu wa elimu mara nyingi wanapata wakati mgumu wa kukosa vitendea kazi na fedha za kuwawezesha ili waweze kutekeleza matakwa yale ya kukagua kiwango cha elimu, ubora wa elimu na hali yao ya kutekeleza mipango ya kazi kwa kuwa tunawalipa katika mishahara na kwa kuwa wao tayari tumewaajiri. Mfumo huu ungewekwa kama mfumo ule wa ukaguzi kitaifa kwa maana ya CAG hata kwa Taifa letu huu ukaguzi wa elimu ungejengewa mfumo mzuri kutoka ngazi ya Taifa mpaka kwenye Halmashauri zetu ungeweza kufanya vizuri na kuweza kujenga utaratibu unaofaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna viporo vingi na kwa kweli kwa kadri ambavyo Serikali imefanya kazi katika mwaka huu mmoja tu wa Serikali wa 2016/2017 kazi nyingi sana zilifanyika na inaonekana tukiendelea kutafuta Wakala wa Maji, tukaendelea kutafuta na mawakala wengine, tukatafuta fedha kwenye vyanzo vya ndani vikaungana na fedha za wabia wa maendeleo, basi tunaweza tukafanya vizuri zaidi ili tuweze kukamilisha miradi iliyokusudiwa na kutoa huduma stahiki kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi niombe utaratibu wa upelekaji wa fedha za miradi ya maendeleo katika mwaka huu ulioisha wa 2016/2017 haukuweza kukaa vizuri kwa sababu fedha zilikuwa zinapelekwa, lakini hazilingani na asilimia. Tunaomba fedha za miradi ya maendeleo zitolewe kwa asilimia, kama Halmashauri ilikusudiwa bilioni 50 basi kama tunatoa asilimia 30, iwe ni asilimia 30 kwa namna ambavyo kila Halmashauri inapata kwa sababu yule aliyepangiwa fedha nyingi atapata asilimia 30 na yule ambaye fedha zake kwa mpango wa maendeleo si nyingi atapata zile asilimia 30. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa nimemfuatilia Mheshimiwa Rais kwenye ziara yake siku moja, alitoa taarifa ya kwamba fedha za miradi ya maendeleo zimetolewa kwa asilimia 90, naomba tusimdanganye na kumpotosha Mheshimiwa Rais kumpelekea utaratibu wa taarifa isiyo rasmi, tuwe tunapeleka kile halisi ambacho tumepeleka kwa sababu tunaingia mgongano kati yetu sisi na wananchi kwamba zile fedha zimepelekwa wapi, mbona kwenye taarifa ya Rais zimepelekwa zote ama zimepelekwa asilimia
90. Mambo kama haya yanaipa mkanganyiko mamlaka ya kuchaguliwa kwa maana ya Waheshimiwa Madiwani, Waheshimiwa Wabunge na hata viongozi wengine, lakini pia na watendaji wa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo napenda kuliongelea ni eneo hili la uadilifu, uwajibikaji kwenye mifumo ya Serikali; bado kuna baadhi ya watendaji Serikali hawajabadilika. Tunaomba Serikali itazame upya watendaji wake wote kwa kila Wizara ili wabadilike, wawajibike kwa wananchi, watoe kauli nzuri kwa wananchi, waweze kuwahudumia wananchi na waweze kujitambua kwamba wao wana dhamana kama ambavyo wamekabidhiwa na watumie lugha nzuri wanapowahudumia wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda katika ofisi nyingine majibu wanayopewa watumishi wadogo na wananchi hayalingani kabisa na Serikali ya Awamu ya Tano. Ninaomba sana kama itawezekana Serikali ifungue macho, hasa wale wenye mamlaka ya kusimamia rasilimali viongozi na rasilimali wananchi ili watu ambao wanawajibu wananchi wetu vibaya kwenye ofisi za Serikali, ambao hawataki kuwajibika waweze kuchunguzwa na waondoke kwenye mfumo mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili nalizungumza kwa sababu unapoona huku juu Serikali inafanya kazi vizuri sana, kule kwenye maofisi bado kuna watu wamekaa kwenye ma- bench hawawajibiki, kutoa file meza moja kwenda meza ya pili inachukua mwezi mzima, hii inatukatisha tamaa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naishukuru sana Serikali kwa jinsi ambavyo imeweka nia ya dhati ya kufanya mapitio ya barabara ya Karatu – Mbulu hadi kule Haydom kwa ajili ya kufungua wananchi wa Wilaya ya Mbulu ili waweze kuungana na wananchi wengine kwa mfumo wa barabara ya lami kwa maana ya kuwaunganisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni muhimu sana, itachochea uchumi kwa Wilaya ya Mbulu na Wilaya za Karatu na Wilaya nyingine za kule Mkalama na Shinyanga kwa sababu ukanda huu wa juu wa bonde la ufa ni kama umezungukwa na uzio ambao umefungwa moja kwa moja na Ukanda wa Bonde la Ufa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitaka kuchukua saruji ya Dangote, kama unataka kupeka Mbulu ni lazima kwanza iende Singida, halafu Itoke Singida ije Mbulu. Kwa hiyo gharama yake ni tofauti kabisa na maeneo mengine katika Tanzania yetu kwa kuwa barabara ni ya udongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata ukienda kule Tanga ukachukua saruji kule ukataka kuleta hiyo saruji, ni lazima iende kwanza Mto wa Mbu, ije Karatu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: …ije Mbulu. Kwa hiyo tunaomba sana barabara hii ni ya muhimu sana…