Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kusimama na kuchangia Mpango wa Maendeleo uliopo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali ya Awamu ya Tano pamoja na Waziri wa Fedha na Mipango, Naibu wake Dkt. Ashatu Kijaji pamoja na Watumishi wote wa Wizara hii kwa kazi kubwa ambayo wameionesha kuhakikisha kwamba mpango huu unakuja mbele yetu nasi kama Wabunge tuchangie na kuongeza nyama pale ambapo tunaona panahitaji kuongezwa nyama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa uamuzi mgumu wa kuamua Serikali sasa ihamie Dodoma rasmi, watumishi wote wa Wizara zote zihamie Dodoma sasa, yeye mwenyewe, Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu alikwishahamia na tunawakaribisha wageni wote ambao mnakuja; Dodoma hakuna foleni, Dodoma ni salama, waje wafanye kazi ya ujenzi wa Taifa hili kwa umakini na kwa wepesi zaidi kwa sababu hakuna foleni katika Mji huu wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo ambayo yanatakiwa na yanahitaji utekelezaji wa haraka katika suala la kuhamia Dodoma. Mpaka sasa hakuna sheria inayotamka kwamba Dodoma ni Makao Makuu na nadhani kuna mambo yanaweza yakakwama kama hakuna sheria ambayo inatamka Dodoma ni Makao Makuu. Kwa hiyo, niiombe Serikali sasa Sheria iletwe Bungeni itakayotamka rasmi kwamba Dodoma ni Makao Makuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serikali ya Awamu ya Tano, kabla ya kazi zote zilizokuwa zinafanywa na CDA kukabidhiwa Manispaa, CDA walikuwa na bajeti yao ya takribani shilingi bilioni 47 kwa ajili ya kuendeleza Mji huu wa Dodoma. Kwa sababu hatuna sheria inayoiruhusu Manispaa kutumia au kutoza tozo kwa ajili ya uendelezaji wa Makao Makuu ya Dodoma, Manispaa ina bilioni tisa tu za fedha za maendeleo. Zile bilioni 947 ambazo zilitengwa kwa ajili ya CDA kuendeleza Mji huu bado hazijapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu shughuli za uendelezaji wa Manispaa ya Dodoma ni kubwa sana na hatutaki kuingia kwenye matatizo ya msongamano wa magari kama Dar es Salaam na Arusha na Miji mingine, tunataka Mji wetu upangwe vizuri na mji wetu usiwe na squatter, Mji wetu uwe na barabara za kutoka na kuingia zisizoruhusu msongamano. Manispaa hawawezi kufanya kama hatuna fedha za maendeleo za kutosha kwa ajili ya kuendeleza Mji huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapenda tuwe na wataalam pia wenye uwezo ambao watasaidia kupanga Mji wa Dodoma. Tunataka Mji wa Dodoma uwe tofauti na Miji Mikuu ya Barani Afrika kwa sababu mji huu unajengwa kwa wakati muafaka na kwa fedha ambazo naamini kabisa kwamba tutazipata. Tunataka barabara za mabasi yaendayo kasi, tunataka malori yasiingie mjini, hatuwezi kufanikiwa kama hatuna bajeti. Tutafanikiwa tu pale ambapo tutakuwa na bajeti, lakini la muhimu tuwe na sheria inayotamka Dodoma kama Makao Makuu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani CDA walikuwa wanatoza tozo ya asilimia 35 kwa ajili ya kuendeleza Mji.

Mamlaka ya Manispaa hawana huo uwezo. Tunaomba sasa tukumbukwe katika hilo ili Mji wa Dodoma upendeze kwa barabara, kwa mipango ya mitaa kuwa maeneo ya masoko, stendi na kila kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijasema mengi pia niipongeze Serikali ya CCM kwa maamuzi makubwa ya kuangalia kwamba yale ambayo yalikuwa yamesimama sasa yanafanyiwa kazi. Sisi watu wa Dodoma tunashukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano, reli inakuja mpaka Dodoma, sio reli iliyokuwa standard gauge inayoishia Morogoro, wameshapatikana Wakandarasi na wanaendelea na upembuzi yakinifu na taarifa ya Waziri imeonesha kwamba hawa watu wamekwishapatikana, wanafanya upembuzi na mwisho wa siku tutakuwa na reli ya mwendokasi mpaka Dodoma. Kutoka Dodoma mpaka Dar es Salaam itakuwa aidha saa moja au masaa mawili na wananchi watafaidika na reli ambayo inajengwa sasa kwa standard gauge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaona kwamba ilikuwa kuja Dodoma lazima ukodi ndege yako, sasa hivi ndege ya Serikali inakuja Dodoma bila shida. Waheshimiwa Wabunge wengi nawaona mnapanda Bombadier bila kujali wewe ni wa Chama cha Mapinduzi au wewe ni wa Upinzani au wewe huna chama au wewe una chama. Kila Jumatatu asubuhi Bombadier ikitua hapo ina wananchi wengi wanaoshuka Dodoma, kwa hiyo, naishukuru sana Serikali ya CCM kwa kununua ndege na ndege sasa inawahudumia wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Spika na niwapongeze kwa kile walichokifanya. Mheshimiwa Spika, aliunda Kamati mbili zilizoshughulikia madini na ikatungwa sheria ya kushughulikia madini na sasa wizi tuliokuwa tunafanyiwa haupo tena, fedha zile ambazo tulikuwa tunaibiwa na wawekezaji hazitakuwepo tena! Naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa haya mambo makubwa ambayo tumeona wamefanya kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kuhusu suala la kilimo. Asilimia 75 ya Watanzania ni wakulima lakini hawapati mbegu bora kwa wakati. Pembejeo za kilimo ni ghali mno na hata viwanda tunavyotaka kuanzisha tunaanzisha malighafi tutapata shambani. Niishauri Serikali yangu, pembejeo zipatikane kwa wakati kwa wakulima lakini zipatikane kwa bei nafuu anayoweza kumudu mkulima. Wakulima wetu baadhi bado wanakwenda kununua mahindi sokoni, wanakwenda kupanda mahindi waliyonunua sokoni. Wananunua mtama sokoni, wanakwenda kupanda mtama walionunua sokoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali sasa wahakikishe kwamba pembejeo zinafika kwa wakati. Hata hivyo, bado hatujatilia mkazo suala la kilimo cha umwagiliaji. Kufuatana na tabia nchi kuharibika, sasa hivi mvua hazieleweki zitanyesha wakati gani, kwa hiyo ni vizuri pia tukakazania kilimo cha umwagiliaji, mabwawa yale ambayo yalichimbwa na mengine hayajafikia hatua za mwisho, basi Serikali ione namna ya kupeleka fedha. Sisi Dodoma tuna bwawa la Farkwa, lingetusaidia kwa kilimo cha umwagiliaji, lingetusaidia hata kwa masuala ya maji katika Wilaya zetu ambazo zinapakana na Mto Farkwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kilimo, mifugo na uvuvi sijaona kama limetiliwa mkazo sana kuhusu suala la mifugo na uvuvi. Kuna ng’ombe wengi sana hapa nchini lakini hatuna viwanda vya nyama, hatuna viwanda vya ngozi, hatuna viwanda vya maziwa ya kutosha. Niiombe Serikali kama kuna uwezekano wa kuingia ubia na wananchi wawekezaji wakafungua viwanda vya nyama, migogoro ya wakulima na wafugaji itapungua, kwa sababu wafugaji watauza mifugo yao kwenye viwanda vya kuzalisha nyama, wakulima watakuwa na viwanda kwa ajili ya mazao yao. Pia suala la uvuvi tuna viwanda vichache sana vya samaki, Serikali iangalie suala hilo.