Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Pia nimshukuru sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini na kunipa dhamana hii. Nimshukuru sana Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa, kwa miongozo yao wanayonipa katika utekelezaji wa majukumu yangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru na nimpongeze sana Waziri wangu, nilimsikia kwa makini hapa wakati alipokuwa akijaribu kunishukuru na kunipongeza kwa jinsi ambavyo nashiriki katika shughuli nzima za Wizara tuliyokabidhiwa na Mheshimiwa Rais. Aliongea maneno mengi ambayo hata mengine hayajaandikwa kwenye vitabu na mimi namshukuru sana. Namshukuru sana pia kwa weledi wake kwa jinsi ambavyo anaiongoza Wizara. Pia niwapongeze Wenyeviti wa Kamati zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababau muda ni mfupi na hoja za Waheshimiwa Wabunge ni nyingi mno, basi nianze moja kwa moja na hoja za Waheshimiwa Wabunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, hoja yao ya kwanza ilikuwa ni kwamba kutokana na Serikali kujenga jengo la Ofisi ya Makamu wa Rais chini ya kiwango, Kamati inashauri Serikali kuwa makini wakati wa uteuzi wa wakandarasi ili kuhakikisha kuwa wanaopewa tender ya ujenzi wa ofisi kama ya Makamu wa Rais wanakuwa na uadilifu, uwezo, ujuzi, weledi wa hali ya juu.
Aidha, Wakala wa Majengo wa Serikali (Tanzania Building Agency - TBA) wawe makini wakati wote kukagua na kuhakikisha kuwa majengo ya Serikali yanajengwa kwa ubora wa kiwango stahiki. Pia wakala ahakikishe kwamba Serikali kwa namna yoyote ile haikabidhiwi jengo lililojengwa chini ya kiwango ili kuepusha kupata hasara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nachukua nafasi hii kuwapongeza sana Kamati hii chini ya Mwenyekiti mahiri Mheshimiwa Mohamed Omary Mchengerwa kwa kuliona hili. Naomba tu niweke kumbukumbu sawasawa kwamba wakati Wizara yangu ina-appear kwa Mwenyekiti tayari ilikuwa imeshamuandikia barua CAG kuchunguza uhalali wa jengo hili, uhalali wa gharama zilizotumika pamoja na upungufu uliojitokeza. Sasa hilo ndilo ninalotaka kuliweka sawasawa. Sasa hivi naliarifu Bunge lako Tukufu kwamba hatua zinaendelea vizuri ili CAG aweze kufanya tathmini ya kujua thamani halisi ya jengo hilo na tulishamuandikia barua mapema na sasa hivi anaendelea vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Ofisi yangu ilikuwa tayari imeshazuia malipo. Tulikuwa tumeshaandika kuzuia kwamba malipo yoyote yale hayawezi kufanyika hadi pale tutakapokuwa tumejiridhisha kwamba gharama zilizotumika katika jengo hili ni halali ndipo hapo tutakapotoa tena ruhusa ya kutoa malipo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili ya Kamati ilikuwa Serikali iendelee kuchukua jitihada za dhati katika kutatua kero za Muungano ili kuongeza tija katika shughuli mbalimbali za biashara na maendeleo kati ya Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar. Ushauri huu umepokelewa, Serikali zetu mbili zitaendelea kuhakikisha kuwa mambo yote yanayokwamisha utekelezaji wa masuala ya Muungano yanapatiwa ufumbuzi wa haraka. Nataka nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba tutakachokifanya katika Awamu hii ya Tano, vikao vyote kwa mujibu wa ratiba za Serikali hizi mbili vya mazungumzo na maridhiano vitafanyika kwa mujibu wa ratiba iliyopangwa, hiyo kazi tutakahakikisha tunaifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile lazima ifahamike kwamba sisi na Mheshimiwa Waziri wangu hatuna uwezo, kwa sababu maamuzi haya yanatokana na vikao viwili vya maridhiano kati ya pande zote mbili. Sisi ni kuhakikisha kwamba tunaratibu vizuri, ni kuhakikisha kwamba vikao vinafanyika salama, lakini mimi na Waziri wangu hatuna uwezo wa kuamua hata jambo moja katika mambo haya ya changamoto za Muungano zilizopo, tukasema kwamba hili tunataka tuamue hivi, haya yote yatatokana na maridhiano ya pande zote mbili. Kwa hiyo, tutakachohakikisha ni kwamba vikao vyote vilivyopangwa vinafanyika kwa mujibu wa ratiba kama ilivyopangwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine lililozungumzwa na Kamati ilikuwa ni suala la Serikali kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa faida zitokanazo na Muungano kwa pande zote mbili. Ushauri tunaupokea, jitihada zaidi zitaongezwa ili kuelimisha umma kuhusu muungano kadri rasilimali fedha zinavyopatikana. Ndivyo tutakavyofanya na mkisoma vizuri hotuba yetu tumeeleza mambo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda basi niende tena hoja za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira chini ya Mwenyekiti hodari Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu.
Hoja ya kwanza, Serikali iendelee kuwaelimisha wananchi juu ya udhibiti wa taka za plastiki, kukuza matumizi ya mifuko mbadala na pia mpango wa kupiga marufuku matumizi ya mifuko ya plastiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lako linafahamu tulikuwa na Kanuni za mwaka 2006 baadaye zikaondolewa na Kanuni za mwaka 2015 ambazo zinazuia matumizi ya plastiki yanayozdi macron 50. Kamati imesema ni tarehe 01 Julai, 2017 lakini tulishalitangazia Bunge lako Tukufu kwamba tumetoa huu muda wa kutosha wa wenye viwanda na wahitaji wengine wa matumizi ya plastiki ya kwamba ifikapo tarehe 01 Julai, 2017 itakuwa mwisho wa matumzi ya plastiki hapa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili ilikuwa ni vyanzo vya fedha kwa ajili ya Mfuko wa Taifa wa Mazingira vitokane pia na tozo zitakazotozwa na Wizara zingine, zitambuliwe na zihamishiwe katika mfuko. Tumeainisha shughuli muhimu za Mfuko wa Taifa wa Mazingira na Waheshimiwa Wabunge hapa kila mmoja amezungumza kwa hisia kubwa kuhusiana na mambo muhimu yanayohusu suala la mazingira. Waheshimiwa Wabunge wamezungumza jinsi athari kubwa za mabadiliko ya tabianchi ambazo Taifa sasa hivi linasakamwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unazungumzia kuta za Pangani ambapo sasa Pangani inakuwa kwenye hatari ya kudidimia kutokana na hiyo mikondo ya maji ya bahari ambayo imeuandama Mji huo. Mimi mwenyewe nilifika na kujionea. Ukizungumza kuhusu Kisiwa Panza - Pemba, kisiwa kile kimeandamwa na maji ya bahari ambayo sasa hivi mikondo yake inaingia mpaka kwenye mji ule. Kisiwa kile kiko kwenye hatari kubwa ya kuzama.
Vilevile unazungumzia Kilimani lakini unazungumzia Wabunge ambao leo wanalalamika kuhusu mafuriko makubwa yanayotokana na mabadiliko ya tabianchi. Mabonde yamejaa, hakuna mifereji, hakuna mabwawa ya kutunza yale maji ili kuweza kuyaondosha kwenye makazi ya watu. Unazungumzia suala zima la uharibifu mkubwa wa mazingira na suala la jinsi misitu ilivyoandamwa na kukatwa kulingana na shughuli mbalimbali za kiuchumi za wananchi ambapo Taifa linalazimika lipande miti kwa nguvu zote. Unazungumzia uchafu wa mazingira, lazima uzungumzie ujenzi mkubwa wa madampo na ujenzi mkubwa wa machinjio.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yote haya ndiyo Mfuko huu wa Mazingira ambao tunaupigania kwamba lazima upate fedha za kutosha walau shilingi bilioni 100 kwa kila mwaka wa fedha. Bunge hili tunaliomba na kama Mwenyekiti alivyoshauri na sisi tunapokea ushauri wake, ni lazima tujipange kwa nguvu zote tuhakikishe tunapata fedha za kutosha kupambana na mambo yanayotukabili ya mazingira na tabianchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Wabunge wengine walifikia mahali wakajaribu kusema kwamba suala la mazingira hivi ni kufagia tu au kuondosha taka tu au ni kufanya ukaguzi wa viwanda. Tumekwenda zaidi ya hapo labda kwa mtu ambaye hajasoma hotuba yetu. Ukisoma hotuba yetu imesheheni mambo mazito kuhusu mazingira ya nchi hii, imesheheni mambo mazito kuhusu mabadiliko ya nchi hii, yamechambuliwa kisayansi na kwa ufasaha mkubwa.
Waheshimiwa Wabunge, mkisoma mtaiona nia ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Tano katika kuhakikisha kwamba mazingira yetu yanakuwa salama, katika kuhakikisha kwamba hali ya mabadiliko ya tabianchi iko salama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Jitu Soni pamoja na Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti Mheshimiwa Hawa Ghasia wameliongelea vizuri sana suala la mita 60 na kutuomba kwamba hizo mita 60 tujaribu kuangalia upya matumizi yake. Serikali inapokea kwa heshima zote wazo hili na sasa hivi tuko kwenye mapitio ya Sera na Sheria ya Mazingira ya 2004 ili kuangalia vifungu vya sheria ambavyo vina dosara katika utekelezaji ambavyo havina tija kwa wananchi, tunavifanyia marekebisho ili viweze kuleta tija na faida kwa Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu walisema Serikali hii inafungia viwanda, inapiga faini wenye viwanda na kwamba kwa kufanya hivyo inakuwa haiwatendei haki na inadhulumu ajira pamoja na uchumi wa nchi. Nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge, sisi ndiyo mmetupa dhamana ya kusimamia jukumu hilo. Kwanza haya mambo tunayafanya kwa mujibu wa sheria lakini hivi mnazungumzia mtu gani aliyefungiwa na kwa faida ipi? Yaani mnamzungumzia mwenye kiwanda ambaye anatiririsha maji ya kemikali watu wanakunywa sumu kwamba huyo ndiyo anatoa ajira kwenye Taifa? Ndiyo mnamzungumzia kwamba eti huyo analipa kodi na anatoa faida katika uchumi wa Taifa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda kama kile cha Rhino Tanga tulikifunga kwa sababu kinatoa vumbi na limeenea mji mzima, wanafunzi hawawezi kusoma wala walimu hawawezi kufundisha, ndiyo viwanda hivyo mnavyovitetea? Mnazungumzia Kiwanda cha Ngozi cha Shinyanga ambacho kinatoa harufu mji mzima kiasi kwamba watu wanaugua maradhi makubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia inatutahadharisha inatuambia sasa hivi zaidi ya watu milioni tano katika nchi maskini wanakufa kwa magonjwa ya saratani za mapafu kwa maana ya kushindwa kupumua, wanavuta hewa ambayo hairuhusiwi, wanavuta hewa chafu, leo Wabunge ndiyo mnazungumzia hilo? Mnazungumzia migodi ambayo inatiririsha kemikali kwa wananchi, wananchi wanakunywa sumu, wananchi wanababuka, wananchi wanakufa, mifugo inakufa, leo Mbunge ndio unazungumzia migodi hiyo kwamba tunahujumu, tuna-frustrate ajira, tuna-frustrate uchumi wa nchi! Tutaendelea kuchukua hatua na tutazingatia sheria katika kutekeleza majukumu yetu haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, NEMC, nataka niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge kwamba NEMC itafanya kazi. Pamoja na changamoto zake zote za ukosefu wa rasilimali, tunaomba rasilimali ziongezwe lakini kabla ya hapo tutaendelea kuhakikisha kwamba mapinduzi ya viwanda hapa nchini yanakwenda sambamba na utoaji wa huduma ya kufanya tathmini kwa athari ya mazingira. Tumeshatoa maelekezo NEMC kwamba Sheria ya Mazingira ya 2004 inatupasa kutoa cheti cha mazingira ndani ya siku 90.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nilihakikishie Bunge hili, pamoja na changamoto tulizonazo tutaendelea kuhakikisha kwamba tunatoa cheti cha mazingira kwa muda wa siku 90. Tumeshawaelekeza NEMC hakuna namna yoyote ile ya kuchelewa ndani ya siku 90. Wale consultants waliokuwa wanahusika na uchambuzi wa miradi, wale wavivu wale, tulimuagiza Mkurugenzi wa NEMC kuwaondoa mara moja kwenye orodha na wameshaondolewa. Vilevile tulimuelekeza ndani ya idara yake inayosimamia uchambuzi wa tathmini ya mazingira inaweka watu ambao ni competent, wenye uwezo wa kuchambua tathmini ya mazingira kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kaka yangu Mheshimiwa Nsanzugwanko ameongea kwa hisia kubwa sana kuhusu suala la wakimbizi kwamba halimo kwenye taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumeomba fedha za Mfuko wa Mazingira shilingi bilioni 100, tusaidiane Wabunge tutafute fedha hizi za kutosha ili Mfuko huu uweze kutunishwa. Tusingeweza kuainisha mambo yote hapa lakini tumesema Mfuko huu wa Mazingira ukiimarishwa tutatatua mambo makubwa yaliyoliathiri Taifa hili katika mazingira, tutatatua mambo makubwa ambayo yamelisababisha Taifa hili kuwa na mabadiliko ya tabianchi. Tuungeni mkono hapa ili tufanye kazi hizi kwa ufanisi mkubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja asilimia mia moja.