Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kunipatia fursa hii ili na mimi niweze kuchangia machache juu ya mpango huu. Kwanza kabisa nimshukuru Spika, kwa asubuhi ya leo amefungua milango ya namna ya uchangiaji na kututoa hofu. Wapo watu wamekuwa na hofu namna ya kuchangia wakihofia labda mtu anaweza kutumia maneno yakasababisha kupelekwa kwenye Kamati ya Maadili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama ndivyo, ushauri wangu sasa kwa Wabunge wote lakini zaidi kwa vijana wasomi, mnayo nafasi ya kuisaidia Serikali, kuishauri kwa uwazi na kwa haki ili mawazo yenu na ushauri uweze kupokelewa. Hatuna haja ya kuwa na wasiwasi na bahati nzuri uteuzi umepita mpaka 2020 naamini tusiwe na hoja ya kufikiri kwamba, kuna uteuzi au mambo gani. Kwa hiyo, tujikite kuishauri Serikali kwa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuwapongeza Mawaziri, kwanza wale waliobaki kwenye Baraza la Mawaziri, lakini pili ni wale ambao wamepata fursa ya kuingia kwenye Baraza la Mawaziri, ni imani yangu nafasi hiyo wataitumia vizuri kutusaidia kusonga mbele kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia liko jambo ambalo ni vizuri nikalisema ambalo ni tatizo lililoko jimboni kwangu, lakini kwa maana ya kitaifa juu ya hifadhi. Wananchi wetu sasa wanateswa. Tunazungumzia mipango ya maendeleo, wakati huo huo kuna watu wanapitisha mabango kusema shughuli za kibinadamu zisifanyike, watu baada ya wiki mbili wahame, unazungumzia Wilaya ambayo
asilimia 90 ni hifadhi, lakini ndani ya hifadhi kuna vijiji ambavyo vimesajiliwa, kuna shule ambazo zimesajiliwa, tunaenda wapi? Unapowaambia watu eneo lote la Ulyankulu ni hifadhi, halafu watu wako mle kabla, si ajabu hata ya Sheria ya Hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuiombe sana Serikali kama kweli tunazungumzia maendeleo hebu tusiwabughudhi watu wetu, tusiwaone watu bora wakati wa kufikia uchaguzi. Wakati tunapo-approach uchaguzi mambo yote haya tunaambiwa kaeni, chapa kazi muishi kwa amani, lakini hapa katikati anakuja mtu wa TFS anavuruga kila kitu, unataka watu waishi wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani jimbo zima, wilaya nzima tunatunza miti, ifike mahali tujue nani bora, bora msitu au bora binadamu? Itatusaidia sana badala ya kuwa tunawavuruga wananchi wetu, wanapanga na wao mipango yao ya maendeleo, leo unawaambia kuanzia sasa shughuli za kibinadamu zisimame, maana yake maendeleo yasimame. Maeneo hayo yanayoambiwa hivyo, labda wiki moja u mwezi mmoja nyuma Waziri Mkuu amepita na hata yeye kuchangia.

Kwa hiyo, Serikali hii iangalie huyu anasema hivi, kesho mwingine anasema hivi na mwingine atakuja weka ndani. Imefikia hatua Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya anawekwa ndani kwa jambo kama hili. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali itusaidie kutuliza hali hiyo na ninajua mdogo wangu Mheshimiwa Kigwangalla atalirekebisha pamoja na Mheshimiwa Hasunga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa twende kwenye kilimo. Kilimo ndio uti wa mgongo tunavyozungumza kila siku na kilimo ndicho kinachotuletea pesa nyingi za nje, hapo tunakuwa tunazungumza habari ya mahindi. Nawashangaa sana watu wanaotetea wakulima wasiuze mahindi, sisi mishahara yetu hakuna anayetupangia matumizi. Iweje mkulima ambaye kalima bila mkopo, kwa fedha zake, halafu apangiwe namna ya matumizi ya mahindi yake? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Ulyankulu tunalisha Mwanza, tunalisha Shinyanga kwa mahindi yanayotoka Ulyankulu. Ni kwa vile tu mnaowataja hamuitaji Tabora, lakini kumbuka kwamba watu wa Mwanza, watu wa Shinyanga, Kahama, mahindi wanayokula yanatoka Ulyankulu na sisi tuko tayari kuuza. Kama ni hivyo mimi siko tayari kuhimiza kilimo kwa sababu watu wanafanya juhudi, wanalima chakula kipatikane, lakini tunaanza kuweka vikwazo kwa mkulima kutumia rasilimali zake. Mbolea amenunua mwenyewe kwa pesa zake, kila aina ya pembejeo amenunua, lakini inafika amevuna anapatikana mtu wa kumpangia, haijapata tokea, hayo ni mahindi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumbaku hii ya sasa imekuja mwaka 1967, na mimi mkubwa tu mwaka 1967, sasa tumbaku hiyo huko nyuma tarehe 5 au 6 Julai, kabla ya Sikukuu ya TANU ilikuwa ni lazima wakulima wote wawe wameshapata pesa; haijapata tokea safari hii masika mvua inanyesha tumbaku bado iko kwenye ma-godowns, tumeweza kwenye makinikia eti tunashindwa kwenye tumbaku, haiwezekani. Nini kipo hawa wazungu wa tumbaku wawe na kiburi kuliko wa makinikia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi tena siko tayari, nasema kabisa, yaani siwezi kusimama jukwaani kuhimiza kilimo ambacho watu wanateseka, tumbaku limekuwa zao la kuleta umaskini sasa. Hiyo korosho ya wenzetu Mtwara huko, Lindi zamani isingesikika, lakini kwa sababu nia ya Serikali ilikuwa kuhakikisha kuwakomboa wenzetu wakulima wa korosho, leo hii wanafurahia. Lakini tumbaku tunahangaika. Tumbaku iko kwenye ma-godown, mvua zinanyesha, lakini utashangaa tunasema tumbaku hii ni zao linaloleta pesa kuliko mazao mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii kampuni ile iliyochukua mali za TAT inauza mpaka ma-godown, itauza kwa tender ma-godown yote nchi nzima yametangazwa yanauzwa, hiyo tumbaku itakuwepo, haitakuwepo. Na leo hii tunazungumza hivi kama mzaha, watu wameuza tumbaku wale ambao hawakuwa kwenye mpango kwa maana ya bajeti ile ya tumbaku wameuza mpaka ile bajeti ime-burst, wale wakulima sasa waliochelewa wanaambiwa mna tumbaku ambayo hamkupangiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili linaleta taabu. Sisi wanasiasa wa Tabora na hasa Wabunge tunapata kigugumizi, iko shida lazima, iko shida hapa katikati. Tumesafisha WETCU, lakini iko shida hiyo shida huko mbele najua itakuja kuumbua watu, hatuwezi kukaa jambo moja tu tunarudia, Waziri Mkuu amekuja karibu mara nne, lakini hakuna ufumbuzi. Wazungu wameona kwamba, wao ni zaidi ya Serikali, lakini tunaambiwa watu tutafute masoko wenyewe, hivi mkulima mmoja mmoja aanze kwenda Uchina, Indonesia, wapi, kutafuta soko, haiwezekani, maendeleo gani hayo tunayataka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa muda si mrefu tutaanza kusimama majukwaani kuwaambia acha kulima tumbaku. Nitawaambia watani zangu Wasambaa na Wadigo leteni katani tuanze kulima katani kwa sababu sasa tumbaku haitusaidii. Watu wetu wamekuwa maskini, sio vizuri na Serikali muangalie kule ambako Serikali inapata mapato, nayasema haya kwa uchungu. Jimbo la Ulyankulu ndio linalotoa mahindi kwa wingi, tumbaku kwa wingi. Aah, hii kengele tayari? (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya maji, tumesema hapa leteni mpango kuhakikisha nchi nzima inapata maji kama ilivyo REA I, REA II na sasa tunakwenda kwenye REA III, shida gani ipo? Maji yakipatikana hayo mambo mengine yanakwenda vizuri, lakini maji haya imekuwa tatizo, maji ya Ziwa Viktoria wanatumia wenzetu kule Misri, wanatumia Ethiopia, wanatumia sijui Sudan, wapi, sisi eti tukitaka kutumia, tayari kaja mtu hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tu miradi hiyo amekuja mtu kutembelea Tanzania, hatujui walichonong’ona, lakini tetesi ni kwamba wanapata hofu. Maji tunayo tele yanaweza yakasambaa nchi nzima, kwa nini tusifanye hivyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Malagarasi pale kuna maji, ingawa yana shida, lakini maji ya Ziwa Victoria ni maji mengi sana, leteni huku. Tunakaa tunahangaika ooh, mvua, kwa nini tusipate maji kutoka Ziwa Victoria?

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara. Barabara tumekuwa na mipango. Ukiangalia Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ziko barabara nyingi sana, acha mbali ahadi za Mheshimiwa Rais, lakini je, utekelezaji wake uko kwa kiwango gani? Leo tuna miaka miwili tunazo barabara nyingi, mojawapo barabara kutoka Mpanda – Ulyankulu mpaka Kahama, tunazungumzia ujenzi wa lami, barabara ni pori, hata upembuzi yakinifu hatuoni, mipango gani hii sasa?

Kama hatuna barabara zinazopita kwenye maeneo ya uzalishaji tunajidanganya. Ndio hii sasa mazao yanabaki sehemu yana bei ndogo, tunapiga kelele. Mheshimiwa Mpango jaribuni kuliangalia hilo barabara zetu zikae vizuri. Kuwe na nia ya dhati kwamba, sasa tunataka kutengeneza barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini reli hiyo standard gauge sina hakika tutachukua miaka mingapi, hapajaelezwa, lakini lazima kama ni hivyo reli zetu tuziimarishe. Tunayo reli ya kati, tunayo reli ya Singida, tunayo reli ya Moshi – Tanga, hebu tuingize nguvu zaidi kule wakati tunaendelea na mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Umeme REA III. Aah, speed imekuwa ndogo kabisa, Mheshimiwa Kalemani sijui speed yake imeshia wapi. Sijui baada ya kufika huko aliko, speed ya REA III ni ndogo sana. Tuiombe Serikali iongeze speed kwenye huu mradi, lakini kuhakikisha vijiji vyote ambavyo havikupitiwa, lakini taasisi zote, lakini na sisi wanasiasa tusiweke fitina maeneo mengine. Huko kuna uhakika kwamba, wanasiasa wakati mwingine tunapindisha maeneo mengine yasipate umeme kwa sababu za kisiasa, hebu tuache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha za maendeleo kwenda kwenye Halmashauri bado ni tatizo. Iko Halmashauri moja ilipangiwa kupelekewa bilioni 11 imepelekewa bilioni moja, hebu tuone hivi kweli kuna jambo litaendelea? Kutoka shilingi bilioni 11 inapelekewa shilingi bilioni moja, shilingi bilioni nyingine shilingi bilioni 10 hazijaenda, unategemea nini katika eneo hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri zetu bado ziko tete haziwezi kujiendesha. Ziko Halmashauri hata kulipa posho ya Madiwani haziwezi kumudu, ningeomba sana uwepo utaratibu wa kuwahisha pesa. Mbona tunazungumza tunakusanya sana, sasa kama tunakusanya pesa inaenda wapi? Kama pesa kila siku tunasema makusanyo yamepanda, eeh, mbona pesa haziendi Halmaashauri? Iko nini? Iko shida gani? Pelekeni hela kule tuone tutakachokwama, bahati nzuri Wabunge wote sisi ni sehemu ya Halmashauri. Bila shaka Mheshimiwa Mpango utakuwa umenipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari? Aah, bado bwana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwe na upendeleo kwa machifu.