Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii na mimi nichangie Mpango wa Serikali uliokuwa mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nichukue nafasi hii nimpongeze Mheshimiwa Mpango, Naibu Waziri wake na watendaji wote wa Wizara ya Fedha na Mipango wakiongozwa na Katibu Mkuu Ndugu Doto kwa kuandaa Mpango huu na kuletwa hapa Bungeni ili sisi Wabunge tuweze kutoa mchango wetu na pale kwenye mapungufu tuweze kuongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze sana Serikali kwa kuanzisha Wakala wa Barabara Vijijini (TARURA). Ni wakala ambaye anaenda kutatua changamoto za miundombinu, hususan kule vijini kwetu tunakotoka. Hii maana yake nini kwamba, mawasiliano kati ya wakulima kutoka sehemu moja mpaka sehemu nyingine yanakuwa ni rahisi zaidi, lakini pia wakulima tunapata nafasi nzuri ya kupeleka mazao yetu sokoni na kupunguza gharama na kuongeza vipato kwa wakulima wetu. Nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze Serikali kwa kuanzisha na kuihamasisha Mifuko ya Jamii kuingia kwenye kuwekeza katika viwanda, hususan kiwanda cha kielelezo, Kiwanda cha Mkulazi. Nawapongeza sana, kwa sababu kinaenda kujibu tatizo la nchi la upungufu wa sukari. Baada ya kiwanda hiki kuisha matatizo ya sukari yatapungua sana nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo nianze kuchangia kwenye Mpango, na mi mi kwa sababu natoka kijijini, ninatoka Wilaya ya Morogoro Vijijini lazima nitajikita zaidi kwenye suala la kilimo kwa sababu ndiyo suala linalogusa wananchi walio wengi katika maeneo yangu ni suala linalogusa Watanzania wengi. Kwa sababu zaidi ya Watanzania asilimia 70 wako vijijini na wanategemea kilimo kwa chakula pamoja na shughuli zao za kiuchumi.

Mheshimiwa Mawenyekiti, nataka tu ni-quote vitu kidogo kwenye Azimio la Arusha, kule mwanzo kabisa. Azimio la Arusha lilizungumza kabisa maendeleo ya nchi yataletwa na watu, hayaletwi na fedha. Fedha ni matokeo sio msingi wa maendeleo. Ili tuendelee tunahitaji vitu vinne, watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora. Watu tunao zaidi ya milioni 55, ardhi tunayo tena yenye rutuba na mito inayotiririka, siasa safi tunayo ambayo ni siasa ya ujamaa na kujitegemea, uongozi bora tunao, uongozi wenye sera nzuri za Chama cha Mapinduzi. Tatizo ni nini tunakwenda kwa taratibu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo ni kwamba tumewaacha watu wengi katika ushiriki wa kiuchumi katika Taifa letu. Watu hao ni nani? Ni wakulima wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najikita kwa wakulima kwa sababu kama nilivyosema ndiko ninakotoka huko, huwezi kusema nchi hii tutaendelea kama hatujaweza kuongeza kipato cha watu walio wengi wa Tanzania ambao ni wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nayasema haya kwa sababu kilimo chenyewe kinakua taratibu sana, lakini pia hata uwekezaji wa kilimo kwa Serikali bado uko chini sana kwa hiyo, maana yake ni nini, tunawa-sideline watu wengi Watanzania wako nyuma. Kama kilimo kinakuwa taratibu maana yake kipato cha Watanzania wengi nacho kitakua taratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya Azimio la Arusha liliwahi kuzungumza kwamba tusipotahadhari kwa sababu watu wanasema ukizungumza unyonyaji watu wengi wanafikiria ubepari, lakini Azimio la Arusha lilizungumza kwamba, kuna unyonyaji mwingine kama hatukuchukua tahadhari na Serikali isipochukua tahadhari tunaweza kuzalisha unyonyaji mwingine ndani ya nchi kati ya wafanyakazi tunaoishi mjini na wafanyabiashara tunaoishi mjini na wakulima wengi wanaoishi vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu wakulima hawa ndio tunawategemea kwa ajili ya uzalishaji wa chakula. Wakulima hawa ndio tunawategemea kwa ajili ya uzalishaji wa malighafi za viwanda vyetu, lakini tutapata dhambi kama hatuwaangalii, hatuwatengenezei mazingira mazuri ya mazao yao kupata bei nzuri zaidi ili waweze kuwainua kimapato kule vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano mmoja, mimi natoka Morogoro ni wakulima wazuri sana wa mpunga, mahindi na mbaazi, lakini leo hii wakati wa msimu wakulima ukianzia kule Mikese, Tomondo, Kikundi na sehemu zingine tulikuwa tunauza mahindi debe moja zaidi ya shilingi 10,000, kilo zaidi ya shilingi 600, lakini leo hii mahindi ni shilingi 450. Wakati ule tunavuna ambapo kila sehemu Tanzania watu wanavuna sisi mahindi yalikuwa ni shilingi 600 leo hii hakuna msimu mahindi shilingi 450. Ndiyo maana ninaishauri Serikali kwamba tusipokuwa waangalifu tunazalisha unyonjaji, watu wa mjini kuwanyonya watu wa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazao ya wakulima yanayozalishwa mahindi tunawalazimisha wauze bei ya chini ili watu wa mjini na wafanyabisahara tupate chakula kwa bei nafuu, lakini wenyewe wakulima bidhaa zinazozalishwa mjini kwenda vijijini bei zake ziko palepale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukizungumzia sukari bei iko palepale, tukizungumza sabuni bei iko palepale, tukizungumza nguo bei ziko palepale, tukizungumza mafuta bei iko palepale, tukizungumza tiles bei ziko palepale. Mkulima anachotoka kununua bei zinapanda, mkulima kitu kinachomuingizia kipato bei zinashuka, bora zingeshuka kwa nguvu za soko kuliko kushuka kwa kutengeneza mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima hawa hawakulima mahindi haya kwa bahati mbaya, walilima kutokana na bei nzuri ya mwaka jana ambayo mahindi yalifika zaidi ya shilingi 2,000 ndiyo maana watu walihamasika mpaka wengine walichukua mikopo kwenda kununua, lakini leo kuna watu wanasema kuna wafanyabiashara wamenunua mahindi ndio wanaolalamika wanataka kufaidika, hili sio kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali ina dhana kwamba, wamepiga marufuku kwa sababu wafanyabishara wamenunua mahindi wameyahifadhi watafaidika sio sahihi, kwa sababu mkulima huyu anayelima kama nilivyosema mwanzoni anategemea kilimo kwa sababu ya chakula, anategemea kilimo kwa sababu ya kipato chake, anachokihifadhi ni chakula tu. (Makofi)

Kwa hiyo, ukikataza kwamba mahindi yasiwe na bei nzuri unamuumiza mkulima auze bei ndogo kwa wafanyabiashara na watu wengine. Hamna namna yoyote ataacha kuuza kwa sababu ndio kipato chake, lakini pia hana mahali pa kuhifadhi. Mtu amelima amepata gunia 200 ama 300 kuna mkulima gani wa kijijini ana uwezo wa kuhifadhi gunia 200? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama Serikali inaona kwamba kumsaidia mkulima ni kuzuia mahindi yasiende nje ya nchi, basi ni kumuumiza kwa sababu wakulima ni lazima wauze. Ni kweli mahindi mengi yapo kwa wafanyabiashara na mahindi machache yako kwa wakulima, tangu lini imekuwa dhambi kufanya biashara kwenye nchi hii, tangu lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ajira hamna tunawahamasisha watu wakafanye biashara, wamechukua mikopo, wamechukua hela zao wamekwenda kununua, kwa mkulima anamuona ndio mwokozi wakati wa msimu ili kutatua changamoto zake, amemuuzia mahindi, ameyahifadhi, ana mkopo, leo unamwambia asiuze. Ndio maana Mheshimiwa Dkt. Mpango leo unaona mikopo chechefu inaongezeka kwenye mabenki. Inaongezeka kwa sababu miongoni mwa watu waliokopa benki ni hao wafanyabiashara wa mahindi na hao wafanyabiashara wa mazao tuliyopiga marufuku yasiweze kuuzwa nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kwa Serikali, na ushauri wangu kwa Serikali ni kwamba, tutumie fursa ya mahitaji makubwa ya mahindi yetu Kenya, fursa ya mahindi yetu Sudan Kusini, fursa ya mahindi yetu kuhitajika Uganda, tuziangalie kama fursa tusiziangalie kama changamoto. Tutanue soko letu la mahindi tupeleke zaidi ili tuongeze uzalishaji zaidi miaka ijayo na mwakani, kwa sababu vuli hizi tukifika mwezi wa pili/tatu mahindi watu wakianza kuvuna vuli, mahindi yatakuwa zaidi ya shilingi 300, sijui kama tumemsaidia mkulima, hatujamsaidia mfanyabiashara zaidi ni kuwarudisha watu kimapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu Serikali fanyeni tafiti. Waruhusuni wakulima wakubwa na wafanyabiashara wauze mahindi haya ili waweze kulipa mikopo waliyokopa na kurudisha tija kwa uwekezaji wao kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ninalotaka kuzungumzia kwenye suala la mbaazi kwa sababu linatugusa, hapa ndiyo hii dhana ambayo ilikuwepo. Sasa hivi kuna baadhi ya watu wanafikiria kufanya biashara ni dhambi, akiambiwa kuna dalali ni mwizi, akiambiwa kuna wakala ni mwizi, akiambiwa kuna mfanyabiashara ni mwizi! Hatuwezi kujenga, hata hiyo kauli tunayosema kwamba tunataka tushirikiane na wafanyabiashara binafsi maana yake wafanyabiashara binafsi ni wafanyabiashara, sasa ukiwaweka kwenye kundi la wezi hatuwezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna dhana ilijengeka kwamba ukiongea na mnunuzi wa mwisho basi utapata bei nzuri, hili ni kosa kubwa ambalo tulilifanya kwenye mbaazi mwaka jana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, alikuja hapa Waziri Mkuu wa India ambaye ndiye mnunuzi mkubwa na mwenye bei nzuri wa mbaazi. Serikali tukaongea naye, tukamwambia kwamba sisi ndiyo wazalishaji wakubwa wa mbaazi, tunazo mbaazi za kutosha ila walanguzi tu ndiyo wanakuja kutununulia hapa, njooni ninyi wenyewe. Kwa taarifa baada ya pale aliwaita wanunuzi wote 16 hapa nchini wa kununua mbaazi akawaambia naomba muanzishe wakala wenu, umoja wenu wa kununua mbaazi Tanzania na sitaki mtu yeyote anunue mpaka aje kwanza kupata kibali. Tumekiona mwaka huu, mbaazi kutoka shilingi 2,000 mpaka shilingi 150.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali mjue kwamba biashara ni taarifa, kama mimi nina taarifa wewe huna ndiyo mimi nitafanya biashara na kupata faida. Kama mnunuzi wa mwisho amejua kwamba kumbe mbaazi inapatikana Tanzania ana haraka gani ya kuongeza bei? Kwa hiyo, alichokifanya amefanya syndicate kwa wafanyabiashara wote wakubwa akawaambia huwezi kununua, kwa sababu mwanzoni bei zilikuwa zinapanda kutokana na uzoefu, weledi wa hao wafanyabiashara kwa sababu wamewekeza, wamechukua mikopo, wana wafanyakazi lazima wanunue. Wao wanafanya tafiti, wanajua mbaazi hizi zinahitajika lini, nani anahitaji na kwa kiasi gani. Kwa hiyo, wanajua kucheza na yule mnunuzi wa mwisho. Wana uwezo wa kununua bei kubwa kuliko iliyoko katika soko la dunia lakini wanajua nae anahitaji lini, wanazi-hold wanamwambia hatuna mbaazi kama hutaki bei yetu hatuuzi, ndiyo maana bei inapanda. Lakini wafanyabishara wale kwa sababu wanajua wanamdanganya kumbe wakati mwingine mbaazi ni nyingi lakini wanamwambia sharti kwa ajili ya kufanya biashara, hakuna!

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa ushauri katika hilo. Baada ya hapo Dkt. Mpango na Waziri wa Viwanda, kaeni na wadau/wafanyabiashara wa mazao mbalimbali mjue mahitaji ni nini, ubora gani unaohitajika, wakati gani. Kwa sababu wao wana uzoefu wa kutosha, wana mitaji hawategemewi Watanzania peke yake, wanategemewa dunia nzima wanunuzi ndiyo hao hao ukizunguka.

Kwa hiyo, wao wanaweza kujua kwamba kwa nini mbaazi zimeshuka na kwa nini mazao mengine yamepanda. Watu wengi wanataka kupotosha kusema kwamba biashara ya mbaazi imeshuka kwa sababu ya soko holela na biashara ya korosho bei inapanda kwa sababu ya udhibiti wa soko, siyo sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara ya mbaazi inashuka kwa sababu ni zao la muda mfupi, zao la muda mfupi mwaka huu ukipata hela na nchi nyingine zitalima kwa sababu ni zao la miezi mitatu, miezi sita. Kwa hiyo, baadae supply inakuwa ni kubwa kuliko demand. Korosho, hata akikuta 4,000 huwezi kupanda leo ukavuna, tusubiri baada ya miaka mitano au kumi, hizi bei zilizoenda utakuja kuona hali itakuwaje. Ndiyo maana ushahidi unauona, Serikali ya India ndiyo wabanguaji wakubwa wa korosho baada ya Vietnam zaidi ya tani milioni moja lakini uzalishaji wao kila siku unashuka wanazidi ku-import...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.