Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema, lakini kipekee kabisa niwapongeze wenzetu waliopata nafasi za uteuzi. Kipekee kabisa nimpongeze pacha wangu Mheshimiwa Ikupa Stella Alex kwa nafasi uliyoipata, nina imani na wewe na nina amini kabisa utasaidia kuishauri Serikali hasa katika masuala ya watu wenye ulemavu. Waswahili wanasema; kitanda unachokilalia ndio hapo utakapojua kunguni wake. Kwa hiyo wewe unajua, unajua adha na shida mbalimbali zinazowakabili watu wenye ulemavu. Hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze pia Serikali kwa sababu hata wale wanaochangia ni wanachangia kwa nia njema kuona kwamba ni kwa namna gani mpango huu utakwenda kunufaisha Taifa la Tanzania na kufanya uchumi wetu uendelee kukua. Kwa mujibu wa Benki ya Dunia ni kweli kwamba katika Bara la Afrika uchumi wa nchi ya Ethiopia unakua kwa kasi sana lakini pia Tanzania tunakua kwa uchumi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba Tanzania kuwepo katika ukuaji wa uchumi, bado pato la wananchi wa kawaida ni dogo sana kwa maana kwamba maisha ya wananchi wa kipato cha chini hali zao bado ni duni sana. Kwa hiyo, katika mpango huu tulitarajia kuona kwamba mikakati madhubuti ambayo itakwenda kusaidia mbali ya kukua kwa Pato la Taifa, lakini tuone ni kwa kiasi gani kwamba mpango huu unasaidia kukuza pato la mwananchi wa kipato cha chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona pia imezungumzia mfumuko wa bei, lakini katika mfumuko wa bei huu pamoja na kwamba wanasema umeshuka, lakini je, kwa kipato cha mwananchi wa kawaida pato hili limeshuka kwa kiasi gani. Tunaona kwamba bado hali iko pale pale. Kwa hiyo tuone kwamba ni kwa jinsi gani tunaboresha maisha ya wananchi wetu, kwa mfano kwa kuangalia ni vitu gani ambavyo ni muhimu kwa mwananchi wa kawaida. Bei ya mafuta inapokuwa juu ni dhahiri kabisa kwamba inaumiza watu wengi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tumeona kwamba katika muda wa mwaka mmoja, bei ya sukari imekuwa ni tatizo kubwa sana ambapo bei yake pia imekwenda mpaka wakati mwingine imefika shilingi 3,500 mpaka shilingi 4,000. Sukari inategemewa na kila mwananchi wa kawaida, kwa hiyo tunapozungumzia kwamba mfumuko wa bei umeshuka, tuangalie kwa huyu mwananchi wa kawaida umeshuka kwa kiasi gani, tunawasaidiaje wananchi wa kawaida ili uchumi wao na wao pia uweze kukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite katika suala zima la watu wenye ulemavu. Hapa katika ukurasa wa 53 ambapo wameweka vijana, ajira na wenye ulemavu nilitarajia kuona mambo mengi ambayo yangekuwa na manufaa, mpango huu ungeeleza ni kwa jinsi gani unakwenda kujikita kusaidia kundi zima la watu wenye ulemavu. Kwa mfano, hatuna idadi kamili ya watu wenye ulemavu na ili upange mpango wako uweze kukamilika kwamba utafanya nini kwa kundi fulani au kwa vijana ni vema basi tujue kwamba je, tuna watu wangapi mfano walemavu wasioona, kwa mfano tuna walemavu wa viungo, viziwi na wengine wengi. Kwa kujua idadi yake tunapanga mipango kulingana na idadi ya watu ambao tunakwenda kuwasaidia kukwamua kipato chao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unavyofahamu tunapozungumzia pato la chini na hasa kwa kundi la watu wenye ulemavu ni watu ambao maisha yao ni ya duni sana. Hasa unapokwenda vijijini, hali zao bado ni duni. Katika mpango huu nilitarajia tuone kwamba kulingana na idadi hii ni mikakati gani Serikali mpango huu unakwenda kuwasaidia vipi watu wenye ulemavu.

Kwa hiyo, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha kuona kwamba ni kwa jinsi gani mnapokwenda kuongezea zile nyama ambazo zimechangiwa na Wabunge tuone kwamba basi mpango huu unakwenda kuwasaidiaje watu wenye ulemavu badala ya jinsi mlivyoweka hapa kwamba vijana, ajira na wenye ulemavu. Wenye ulemavu wana mahitaji yao muhimu tofauti ni vijana, lakini wana mahitaji yao muhimu tofauti na wengine. Huwezi kulinganisha na kijana wa kawaida. Tunawawekea mipango gani, mikakati gani ya kuwasaidia watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali kwa sababu suala la chakula limezungumziwa sana, naomba nizungumzie kwangu mimi hasa katika suala la kuboresha kilimo. Kilimo ndiyo uti wa mgongo. Wengi wetu hapa tumesomeshwa na kilimo, pia na mifugo tumetoka huko. Sasa tunapoelezea katika mpango huu tungeona kwamba katika kilimo tunaboresha vipi kilimo chetu. Ni kweli wananchi wanalima, lakini kilimo chenyewe bado ni kilimo duni. Kutokana na mabadiliko ya tabianchi hali ya hewa hivi sasa baadhi ya maeneo mvua zimekuwa shida. Je, tunawashauri vipi wananchi wetu ili walime kulingana na hali halisi ya mabadiliko ya tabianchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunaangalia suala la pembejeo ambalo kwa wakati mwingine limekuwa likifika kwa muda ambao sio sahihi, je tunajipangaje? Miundombinu ni suala muhimu sana kwa sababu hata wanapozalisha kama miundombinu sio rafiki, sio mizuri mfano barabara. Kule kwetu ukienda kuna baadhi ya maeneo vijana wanalima nyanya sana, lakini kwa sababu barabara ni mbaya na wachuuzi wanaokwenda kuchukua katika maeneo yale wananunua kwa bei wanayotaka, kwa hiyo, bado hatujawasaidia vijana wetu kuwakomboa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo katika mpango huu, tuone kwamba kutakuwa na mikakati ya elimu kwamba katika eneo fulani kwa mfano yanajulikana maeneo ambayo ukienda Mkoa wa Rukwa, Katavi, ukienda Ruvuma ni baadhi ya maeneo ambayo wanapata mvua nyingi. Je, maeneo yale ambayo hawapati mvua tunawaandaaje wananchi wetu ambao tunajua kabisa kwamba kilimo ndiyo uti wa mgongo, tunawaandaaje ili wao waweze kulima mazao kulingana na mvua. Waweze kulima mazao ambayo yataendana na eneo husika, katika mpango huu sijaona kwamba ni kwa namna gani tunaweka hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mitaji ni muhimu, siku hizi kila kitu kinahitaji mitaji, je, tunaandaaje kuhakikisha kwamba tunawawezesha. Mfano, kama ni vijana ambao ndiyo nguvu kazi tunawaandaaje kwa mitaji ili vijana hawa tunataka kwamba wajiajiri wao wenyewe na kwa sababu tunakwenda katika sera ya viwanda, tunawaandaaje kwamba ili hizo malighafi hao vijana wanaokwenda kujiajiri wenyewe, je, mitaji wanapata wapi. Katika mpango, mpango haujaeleza wazi kwamba vijana hawa tunawaandaaje katika suala la kilimo na kwa sababu kilimo ndiyo ajira pekee ambayo inaweza kuwaajiri vijana wengi wakajiajiri wao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wawekezaji pia kwa sababu hata hawa wakulima wadogo wadogo bado wanahitaji wawekezaji wakubwa ili kwa namna moja kila mmoja anamuhitaji mwenzake. Mipango gani inawekwa ili kuvutia hawa wawekezaji ambao na wao pia waweze kuwasaidia hawa wakulima wadogo wadogo. Vyote hivyo ni vitu ambavyo Mpango ungeweza kueleza kwa uwazi ili basi yeyote yule anayekamata Mpango huu na yeye anasoma anajua kabisa kwamba nchi imeandaa kitu fulani, kwa hiyo vijana au wananchi tujiandae kwa jambo hili kutokana na Mpango jinsi ulivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuboresha ufugaji na kwa mfano, tuliona hivi karibuni bilionea mmoja Bill Gates ambaye anaamini kabisa kukuza uchumi wa wananchi ukiwawezesha katika suala zima la ufugaji kwa mfano kuku. Kuku hivi sasa ni mali, kuku ni pesa. Tunawaandaaje wananchi wetu ili kuhakikisha kwamba na wao wanajiingiza huko kwa kuamini kabisa kwamba ukiwa na kuku hata watatu, nakumbuka siku moja Mheshimiwa Waziri Mkuu alipofika kijijini kwetu alisema kwamba wananchi ili kulipia umeme wa REA ukifuga kuku watatu tu tayari umeshalipia gharama ya kupata umeme wa REA. Je, sasa katika mpango ambao ndiyo tunategemea huku tunawaandaaje wananchi ili hawa wananchi waweze kujikita zaidi katika suala zima la ufugaji kwa sababu ufugaji kama nilivyosema kuku ni pesa. (Makofi)

Vilevile katika suala zima la uvuvi kuna ufugaji wa samaki hivi sasa. Ufugaji wa kisasa ambao ili kukuza mitaji yao na kipato cha wananchi pia nilitarajia kwamba Serikali yenyewe imejiandaa vipi. Kwa hiyo, katika Mpango huu tungeweza kuona kwamba wananchi watasaidiwaje katika ufugaji wa samaki ili kuhakikisha kwamba tunapunguza makali ya maisha jinsi yalivyo kwa hivi sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeona kuna uvuvi katika Bahari Kuu. Mfano, zipo meli nyingi zinakuja hapa nchini na zinakwenda katika bahari kuu kuvua. Je, zile leseni ambazo wanapewa je leseni hizo zinatolewa kulingana na ukubwa wa meli jinsi ulivyo au watu wanapewa tu wanakwenda kuvua kadri yeye anavyoweza na ukubwa wa meli yenyewe. Kwa hiyo, kama tunataka kukuza uchumi wetu katika suala la uvuvi, kwenye Bahari Kuu basi tuone kwamba hizo leseni ziendane kulingana na ukubwa wa meli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa sababu Serikali yetu hivi sasa imeweza kununua ndege, basi tuone ni wakati sasa wa kufikiria mbali zaidi kuwa na meli ya kwetu wenyewe ya uvuvi ili tuweze kuvua wenyewe kwa sababu mahitaji ya samaki hivi sasa watu wengi wanaondoka katika ulaji wa nyama za ng’ombe na ulaji wa nyama nyingine, kwa hiyo wanakimbilia zaidi kwenye samaki na kuku. Kwa hiyo, hili Mheshimiwa Waziri wa fedha jambo ambalo ningetarajia kuliona katika Mpango pia kwamba Serikali katika miaka miwili/mitatu ijayo pengine tumejikita katika kununua meli yetu wenyewe ili basi nasi katika uvuvi wa Bahari Kuu tuweze kwenda kuvua wenyewe na sio kila siku wavue tu wageni wanaokuja hapa nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ile Sera ya Huduma za Fedha kwa ajili ya wananchi. Tuone kwamba hivi sasa inafanyiwa kazi ili basi wananchi waweze kufaidika na hilo. Kwa mfano hili tuangalie kwenye Halmashauri zetu kwa sababu tayari tunawaandaa wananchi ili wananchi waweze kuzalisha kwa wingi. Mfano, katika viwanda, tunapokwenda kwenye viwanda, je, tumewaandaaje katika suala zima mfano kwenye jamii tumeandaaje katika wataalam wa afya maji vijijini ili wananchi basi wawe na afya njema. Vyote hivi ni vitu ambavyo vinahitaji kuzingatiwa kwa umakini kwa sababu wakati mwingine watu wetu wanaangamia kwa kukosa maarifa. Kwa hiyo, kukiwepo na mipango thabiti na katika Halmashauri zetu, kwa mfano Maafisa Biashara hawa wakawezesha kuandaa vikundi kwa ajili ya watu wenye ulemavu na kwa sababu sasa hivi kuna ile asilima nne kwa wanawake, asilimia nne kwa vijana na asilimia mbili kwa watu wenye ulemavu.

Kwa hiyo, Maafisa Maendeleo Jamii na wao wahakikishe kwamba wanaandaa na kutoa mafunzo kwa makundi yote hayo ili kuhakikisha kwamba kila mmoja anajitegema na kuongeza pato yeye mwenyewe lakini pia katika kukuza uchumi wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala zima la mikopo kwenye mabenki ni kweli kwamba tumeona Benki Kuu kwa mfano imepunguza riba kuanzia asilimia 16 lakini vilevile ikashuka mpaka asilimia 12 na sasa asilimia tisa, lakini bado mabenki yanatoza riba kubwa mfano, mpaka asilimia 20, 22. Sasa tunawaandaaje hawa wananchi kama kweli Benki Kuu imepunguza kutoka asilimia 16 imekwenda asilimia 12, imekwenda asilimia 9 kwanini mabenki yaendelee kutoza riba ya asilimia 20 mpaka 22 huku sio kumsaidia mwananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili naishauri sana Serikali yangu kwa upendo kabisa kuhakikisha kwamba kama kweli na hili pia ndiyo maana tumeona kwamba kutokana na jinsi uhaba hivi sasa biashara nyingi ambazo hazijaenda vizuri lakini pia wananchi wengi hawana fedha. Tumeona jinsi ambavyo watu wanauziwa nyumba. Kwa hiyo, kama Serikali katika Mpango tuweke kwamba ndiyo muda umefika muda fulani mtu aongezewe kulipa ili basi kuepusha watu kuwatia katika umaskini. Tukifanya hivi tutawasaidia sana wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la ufugaji, ninaiomba Serikali na hasa katika mpango huu kwa sababu wakati mwingine tunawatia wananchi umaskini.

Mimi ni mtoto ambae nimekulia kwenye familia ya ufugaji. Tumeona juzi huko Rukwa wakati mwingine wafanyakazi au hawa Watumishi wa Serikali wawe na moyo wa huruma. Tumeona wanawafungia ng’ombe kwenye mazizi kweli? Wanawafungia ng’ombe miezi sita, mwaka ng’ombe wanakufa na wengine bado wanaendelea kuwepo pale wazima jamani! Hivi ni kwa sheria zipi? Je, hawa watu tunawafikiria vipi? Kuna mambo mengine ambayo kwa kweli tunaomba wakati mwingine tutanguliwe na huruma zaidi katika kuwasaidia wananchi wetu. Hali ni ngumu, unaenda tena kummaliza huyu mtu. Tuwe na huruma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe pia na nakupongeza sana Mheshimiwa Kigwangalla, Waziri wa Maliasili, wananchi wa Arusha tumechoka na mgogoro wa Loliondo. Kwa hiyo, miongoni mwa mambo ambayo tunakuomba yaishe sasa ni mgogoro wa Loliondo tumechoka nao. (Makofi)

Mhshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya nakushukuru sana. Ahsante sana.