Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa 2018/ 2019. Pamoja na kazi nzuri na jitihada kubwa ambayo inafanywa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kuleta maendeleo katika nchi yetu. nimepongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji kwa wizara kwa kazi mnayofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango huu umeletwa hapa ili tuuboreshe, tutoe mawazo yetu ambayo yanaweza kutumika kuboresha ili tufikie lengo la kuleta maendeleo katika nchi yetu. Na mimi nina amini Waziri na wenzake watatusikiliza na watachukua mawazo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma haya mapendekezo ya Mpango, utagundua humu ndani imeorodheshwa miradi mikubwa ya aina mbili; unaweza uka- group unavyoweza lakini iko ya aina mbili. Iko miradi ambayo ni ya kihuduma, miradi ambayo inahusiana na maji, afya, elimu, utawala na maeneo mengine. Miradi ambayo kwa asili yake haiendeshwi kibiashara, lakini upande wa pili kuna miradi ambayo kwa asili yake inaweza kuwekezwa na kuendeshwa kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa huu mgawanyo wa aina hizi mbili za miradi, niliposoma nilishtuka kidogo kuona Serikali inapendekeza kuwekeza pesa za Serikali kwenye miradi ambayo inaweza kuendeshwa kibiashara. Nilitegemea miradi hii tungeruhusu sekta binafsi, tukatengeneza mazingira mazuri ya sekta binafsi kuwekeza kwenye miradi hii badala ya kuchukua pesa za Serikali na kuipeleka kule kwa sababu madhara yake ni makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Mpango huu utatekelezwa kama ulivyo, miradi hii inakwenda kuua uchumi wa nchi yetu. Nitatoa mfano, miradi hii mikubwa ambayo ninaizungumzia ni miradi kama ya uzalishaji wa umeme na hapa imekuwa ikizungumzwa Stiegler’s Gorge kwa mfano, miradi ya ujenzi wa reli, uboreshaji wa Shirika la Ndege, mradi wa bandari na baadhi ya barabara ni miradi ambayo kwa asili yake inaweza kuwekezwa kibiashara, kuendeshwa kibiashara na ikajilipa kibiashara. Sababu ya kuchukua hela za Serikali kupeleka kwenye miradi hii kwa kweli sijaiona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sifa ya miradi hii kwanza ni miradi mikubwa sana, lakini ya pili kwa ukubwa wake ni miradi ambayo ina gharama kubwa; ukiingalia ni mabilioni kadhaa ya dola kwa asili yake, lakini sifa ya tatu miradi hii niliyoitolea mfano hapa ni miradi ambayo uwekezaji wake utachukua muda mrefu na hivyo payback period yake ni ya muda mrefu sana. Sio miradi ya kulipa kesho, ni miradi ambayo itachukua muda mrefu kwa vyovyote vile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi siipingi miradi hii naomba niweke rekodi vizuri isipokuwa ninapingana na mapendekezo ya Serikali ya namna ya kuiwekeza na kuiendesha miradi hii kwa kutumia pesa za Serikali. Tafsiri ya uamuzi wa kutumia pesa za Serikali kwenye miradi hii ni hii ifuatayo:-

Moja, itailazimisha Serikali kukopa hela nyingi kwa vyovyote vile kwa sababu ni miradi mikubwa, gharama yake ni kubwa, kwa hiyo ni lazima Serikali iende ikakope. Serikali ikienda kukopa na kwa sababu miradi hii inachukua muda mrefu, maana yake ni moja tutaanza kulipa deni hilo lililokopwa kabla ya miradi hii haijaanza kulipa faida kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na tafsiri yake ni kwamba tutachukua hela kwenye maeneo mengine tuilipie deni miradi hii. Hapo maana yake ni kwamba tutaendelea kufunga mikanda muda mrefu, sasa tunafunga mkanda kwa nini? Ndio maana nahoji kwa nini Serikali inafikiri kwamba kuwekeza pesa za Serikali kwenye miradi ambayo ingeweza kuwekezwa kibiashara na sekta binafsi ni jambo la tija kwa uchumi wa nchi yetu, mimi nadhani hapana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vyovyote vile ukichukua pesa za maeneo mengine maana yake utaathiri maeneo hayo, maana yake utaathiri miradi ile ya huduma kama maji, afya, elimu na utawala na mtafika mahali hata malimbikizo ya wafanyakazi itashindikana kulipa kwa sababu tunachukua pesa za Serikali kuzipeleka kwenye miradi ambayo ingeweza kujiendesha kibiashara. Kwa hiyo, mimi nadhani hili la kwanza sio sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna madhara makubwa kwa Deni la Taifa kuchukua hela za Serikali ambazo nyingi kama nilivyosema itabidi tuzikope kuziwekeza kwenye miradi hii. Na hapa Waheshimiwa Wabunge nataka twende kwa takwimu vizuri kwa mahesabu na ndipo hapa ninapohoji uzalendo wa wachumi wetu kuishauri Serikali na Mheshimiwa Rais kuwekeza hela za Serikali kwenye miradi hii, hapa mimi napata taabu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa ripoti uliyotupa hapa Mheshimiwa Waziri, deni letu la taifa limefikia dola bilioni 26 ambayo ni sawa na asilimia 32 ya ustahimilivu wa deni la taifa. Ukomo ni asilimia 56, sasa kama 26 imetupeleka kwenye 32 unahitaji dola bilioni 45 kufikia ukomo wa asilimia 56 ambayo ni mwisho wa kukopesheka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa twende tuchukue mfano wa miradi mitatu, acha miradi mingine yote kwamba hatukukopa, hatukukopa maji ambayo tunachukua hela za wahindi, hatukukopa kwenye barabara, elimu na wala kwenye umeme na maeneo mengine yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu chukua miradi mitatu; mradi wa kwanza ni mradi wa ujenzi wa reli ya kati ambao kwa tathmini yake unaweza ukagharimu approximately dola bilioni 15, ziweke dola bilioni 15, chukua mradi wa Stiegler’s Gorge wa uzalishaji wa umeme ambao kama ninavyosema leo ukikohoa wawekezaji wanakuja, tunataka kuweka hela za Serikali, dola bilioni tano, jumla 15 na tano unapata dola bilioni 20. Halafu chukua uboreshaji wa Shirika la Ndege, kwa ujumla wake mpaka umalize karibu dola bilioni moja kwa hiyo unazungumzia dola bilioni 21.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama una dola bilioni 26 deni la taifa ukijumlisha dola bilioni 21 maana yake unazungumzia dola bilioni 47 na ukomo wetu ni dola bilioni 45, kwa vyovyote vile hii ime-burst. (Makofi)

Sasa kama inakwenda ku-burst maana yake tunakwenda kutokopesheka, kama tusipokopesheka ina maana gani kwa uchumi wetu? Kwa nini tunataka kung’ang’aniza kuchukua hela ya Serikali na tumeanza kwenye reli na ndege tumeweka na kwenye Stiegler’s na kwenyewe tunakwenda, mwisho wake uitakuwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nadhani hebu tufikirie upya, hii thinking ya kwamba sekta binafsi tunaiandika kwenye makaratasi kwamba ndio itakayotekeleza mpango huu, lakini kimsingi kwa matendo yetu tumeiweka pambeni, kwa nini tusiitumie? Awamu ya Pili ya Mzee Mwinyi walianza kuiruhusu sekta binafsi na akatengeneza mazingira, inawezekana kuna mapungufu yake lakini sekta binafsi ilianza kupata mwanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Awamu ya Nne Mheshimiwa Waziri Mheshimiwa Rais wa sasa Magufuli alikuwa Waziri wa Ujenzi. Wakati wake waliruhusu wakandarasi kutoka sekta binafsi wakachukua mikopo ya benki, wakaanzisha makampuni, leo hii tunavyoongea hawa watu mortgage zao zinauzwa. Na zinauzwa kwa kuwa wana madeni wanaidai Serikali, lakini Serikali imeamua kuanza kuchukua mkondo wa shughuli zake za ujenzi kutekelezwa na Serikali yenyewe. Kwa hiyo, hawa tuliowatengeneza kwa miaka yote tunawakosesha hela sasa, they are starving and they are dying.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mpango wako mzuri ndio lakini hebu rudini kwenye thinking ya kuruhusu sekta binafsi kufanya kote, duniani kote mambo yanakwenda hivyo. Jana mmesikia mifano hapa na Mheshimiwa Spika alitoa mfano, Warusi ambao walikuwa waumini wakubwa wa ujamaa wameruhusu sekta binafsi mpaka viwanja vya ndege; sisi leo kiwanja chetu cha ndege pale karibu dola bilioni 560 hivi, hela nyingi kweli. Hivi tungeruhusu watu binafsi wakawekeza nani asingekuja pale, kwa vyovyote inalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mradi kama Stiegler’s gorge pamoja na kwamba nauunga mkono, sina hakika kama tumefanya tathmini ya madhara yake ambayo yanatokana na shughuli za kibinadamu zinazoendelea kuuzunguka mradi wenyewe. Tuna miradi mingine ya maji hapa nchini ambayoo yote ina-prove failure; tumechukua tahadhari gani katika mradi huu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu huu wa kuamini kwamba Serikali itafanya kazi ya kuzalisha umeme yenyewe, ndio utaratibu unaotesa Mikoa ya Lindi na Mtwara. Tumevunja Mkataba wa Symbion tunasema tutawekeza mitambo wenyewe pale, leo Lindi na Mtwara tunakaa mpaka siku tatu au nne umeme hakuna, maisha yanasimama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kama hali hiyo ingekuwa inatokea Dar es Salaam kwamba mnakaa siku tatu/nne umeme hakuna Serikali mngevumilia? Hawa watu wanavumilia hali mbaya lakini kwa sababu gani, tunataka kuwekeza wenyewe kwa kutumia pesa za Serikali kwenye suala la kuzalisha umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya Serikali ibaki kutengeneza mazingira mazuri ya uwekezaji badala ya sisi wenyewe kwenda, tunatumia hela hii kidogo kwa uchumi huu mchanga tunataka tuwekeze kwenye miradi mikubwa. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mahesabu ya kawaida kabisa Mheshimiwa Waziri, mipango hii inakwenda kuua uchumi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nilitegemea hebu tufikirie upya pesa kidogo tuliyonayo twendeni tukaboreshe maslahi ya wafanyakazi, twendeni tukawekeze kwenye maji, afya na maeneo mengine ya huduma badala ya kuichukua na kupeleka kwenda kuwekeza kwenye miradi ambayo inaweza ikajiendesha kibiashara. Kila siku sisi tunapeleka sura mbaya, tunaanza kuonekana kama vile hatutaki sekta binafsi ifanye kazi katika nchi yetu. Utaratibu huu mbaya utaua uchumi wa nchi yetu.