Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, na mimi niungane na wenzangu wote ambao wanamshukuru Mungu kwa kuponywa kwa Mheshimiwa Tundu Lissu na anaendelea vizuri na afya yake inazidi kuimarika. Lakini nianze na mambo machache ya jumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza kwenye vipaumbele hivi vilivyopangwa, nimeona vipaumbele vipo kumi, ile kaulimbiu ya Serikali ya Tanznaia ya viwanda hai- reflect kwenye vipaumbele. Kwenye mpangilio huu viwanda ni kipaumbele cha kumi, maana yake kwenye mpangilio ni cha mwisho kwa hiyo maana yake ni kwamba inawezekana tunaendelea kuibadilisha hiyo kaulimbiu ya Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo jinginela jumla ambalo nadhani ningemshauri Mheshimiwa Waziri Mpango alipokee ni kwamba mwaka wa jana mpango ulikuja wa mwaka mmoja, na vipaumbele vilikuwepo na mwaka huu vimekuja tena. Tulishauri na mimi ningeomba nirudie tena, kwamba Mheshimiwa Waziri ni muhimu tukubaliane kwamba hivi sisi kama Watanzania, kama Taifa tunaweza kupata kiasi gani kwa ajili ya miradi yetu ya maendeleo? Ukishapata kiwango ambacho unaweza kupata kutoka whatever the sources kama ni nje, ndani, vyovyote vile tukubaliane ni mambo gani machache ambayo yanaweza kutekelezwa yakakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na utakumbuka kwenye bajeti ile ilikuwa shilingi trilioni 29.5 lakini haikufika hata asilimia 70 katika utekelezaji wake. Mwaka wa jana tena imekuja shilingi trilioni 31.4 hatutafika asilimia 70 mpaka 80 kwa mwenendo ulivyo mpaka sasa. Sasa maana yake ni kwamba mipango mingi tuliyopitisha itakwama na hiyo kimsingi ndiyo inazua malalamiko mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu la jumla ambao nashauri hapa, inawezekana watu wanapotoa maoni kuna tafsiri tofauti, watu wanaleta hisia za ukanda na nini, lakini ukweli ni kwamba kama kuna mipango, miradi mbalimbali inatekelezwa ambayo miradi hiyo haikujadiliwa kinagaubaga kwa uwazi Bungeni hapa watu watalalmika hakuna namna, yaani hiyo msikwepe. Mwambieni Mheshimiwa Rais wazi kama analazimisha mipango tunayotaka itekelezwe ni hii mliyoleta hapa tukapitisha, mkitekeleza hii hakuna atakayelalamika. Kwa hiyo, watu wasikwepe wasikimbie kivuli chao. Ni kwamba mipango iliyopangwa itekelezwe, kama kuna mapungufu sheria inaruhusu na Katiba inaruhusu tuje tubadilishe mlete maombi inaruhusuiwa. Fedha kama ikipungua usitumie kinyemela, rudini Bungeni hapa, lete mapendekezo tutaridhia hicho ndicho ambacho Wabunge wanasema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kumekuwa na kauli mkanganyiko sana na hizo kauli ni jambo la jumla sana.

Kwenye miradi mbalimbali, Mheshimiwa Rais akisema kauli maeneo mbalimbali watu wanashituka kwa sababu Watanzania wanajua kwa mujibu wa Katiba hii Rais anapatikana kwa kura nchi nzima na kanda zote zimemchangua. Kwa hiyo, unapoona kiongozi mkuu wa nchi anakwenda mahali anatamka kauli ya kiupendeleo hiyo watu hawawezi kuishangilia, wataipinga, watalalamika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninyi cha muhimu ni kupokea mambo, mwambieni Mheshimiwa Rais kwamba huyu ni kiongozi wa nchi akizungumza tunataka atoe suluhu na tiba kwa kero za Watanzania hayo mahitaji ya Watanzania, kwa hiyo msikimbie kivuli chenu na wala msilalamike hapa kuna mjadala wa ukanda hakuna ukanda. Maneno yanayozungumzwa aidha na Mawaziri na viongozi mbalimbali na Mheshimiwa Rais yanawagawa Watanzania. Kwa hiyo, mkifuta hiyo kauli, mshaurini kimya kimya ni muhimu abadilishe kauli za namna hiyo, azungumze kama Rais wa nchi. Hayo ni mambo ambayo kimsingi hayana upendeleo wowote myapokee na kuyafanyia kazi ni ushauri tu
nilisema natoa ushauri wa mambo ya jumla sasa nakwenda kwenye Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, habari ya umeme kipaumbele cha kwanza, mimi Mheshimiwa Mpango nakushauri, kwa sababu kumekuwa na mpango wa umeme wa REA na Watanzania wote na Wabunge wote wanasubiri umeme utekelezwe; umeona kuna malalamiko hapa wanasema wakandarasi walitangazwa lakini baadhi ya maeneo hawaonekani tena, walizindua miradi haijatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni muhimu litekelezwe likamilike kila mahali, kwa maana ya nchi nzima. Hauwezi kuzungumza habari ya viwanda; yaani umeme kwa matumizi ya kawaida haujakamilika, haupo maeneo mengi ni giza, kwenye shule ni giza. Kuna visima vya maji vimechimbwa maeneo mbalimbali hauwezi kutumia maji kwa sabbau hakuna umeme na hakuna uwezo wa kununua jenereta. Pelekeni umeme wa kawaida kwanza halafu hiyo ziada iende kwenye viwanda, watu watakuelewa Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni ujenzi wa miundombinu. Hawa Wabunge wanasema kuna maeneo ambayo mpaka leo Mkoa kwa Mkoa haujaunganishwa, Wilaya kwa Wilaya haijaunganishwa, hilo jambo limezungumzwa mara nyingi. Kama unazungumza habari ya ujenzi wa miundombinu nendeni mkamilishe uhakikishe kwamba Mkoa kwa Mkoa kuna mawasiliano ya kutosha, Wilaya kwa Wilaya halafu uhamie kwenye ajenda nyingine msiguse guse hapa na pale mnahama mnaacha viporo vingi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la mifugo. Kumekuwa na malalamiko, kwa kweli hii ni lana kubwa katika Taifa hili. Watu wote hapa mnategemea kula nyama na mifugo kwa kweli ni mali kubwa sana. Viatu ni humo humo, ni kila kitu lakini inawezekanaje sasa hivi mtu akiwa na mifugo inaonekana kama ni uadui? Yaani kuna ugomvi mkubwa kati ya wakulima na wafugaji. Hakuna malisho ya wanyama, hakuna mahitaji muhimu katika maeneo yale, mifugo inakufa, mifugo inachomwa na hili jambo mnalifahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa mfano pale Dar es Salaam kuna mnada mkubwa sana wa Pugu ambao unaitwa mnada wa kimataifa, lakini ukienda katika eneo hili ukimwambia mtu wa kawaida kwamba ni mnada wa kimataifa hawezi kukuelewa. Hata kama lile ndilo eneo pekee ambalo Dar es Salaam wanalitumia kwa nyama lakini ni eneo la hovyo. Hakuna josho, hakuna mabwawa, hakuna vyoo, hakuna uzio, ratiba haijulikani, rushwa nje nje! Sasa mambo haya ukiyazungumza watu wanasema kwamba labda ni kuituhumu Serikali, si kuituhumu Serikali tunasema ili mkayafanyie kazi, mkarekebishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna ugomvi mkubwa kati ya wafugaji na wakulima, ugomvi kati ya wafugaji na hifadhi za wanyama. Wale watu wa hifadhi wanachukua mifugo ya wananchi, wanaitoa nchi kavu wanapeleka kwenye mapori, wanawatoza fedha nyingi kweli kweli. Kwa hiyo, mpaka wale wananchi wanaofuga wanaona kwamba kufuga ni laana wanaamua kuachana na ile biashara lakini watu wa vijijini ng’ombe ndiyo benki yao. Ukitaka kuzungumza hapa elimu mtoto asomeshwe hawa ambao wamekosa mikopo ya Bodi ya Mikopo maana yake mtu kama ana ng’ombe wake atauza ili asomeshe mtoto. Sasa ng’ombe mmechukua, mmewatelekeza, wamekufa, wanachomwa na wananyang’anywa. Kwa hiyo nadhani jambo hili lazima pia lifanyiwe kazi vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nimeliona hapa ni miradi ya maji. Mheshimiwa Kiwanga amesema hapa kwamba Mheshimiwa Waziri unatakiwa uwe na akili ya kawaida, yakiulizwa maswali hapa na wewe Mwenyekiti asubuhi umesaidia maswali mengi kwenye upande wa maji ni kwamba kama watu wanahoji sana maana yake maji ni shida karibu kila kona. Ukisema hivi Mbunge wa Dar es Salaam Ukonga utafikiri kuna maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kuna watu mpaka leo wanachota maji kwa kutumia zile kata, mvua ikinyesha ndiyo maji wanayokunywa. Sasa jambo hili limekuwa wimbo wa kila siku. Mheshimiwa Mpango wewe kama Waziri legacy yako itakuwa ni nini? Tuambie basi angalau katika mpango huu umeweka miradi ile yote ya maji ambayo imeanzishwa ikamilike, uibue miradi mingine mipya, Wabunge wakija hapa tuache kupiga story ya maji kila siku kama watu ambao hatuna uelewa, tuzungumze jambo lingine. Ile miradi mliyoanzisha kamilisheni, ile miradi mikubwa angalau basi mwaka ukiisha utuambie mimi kama Waziri wa Mipango na timu yangu nimetekeleza mpango huu umekamilika tukose maswali. Hilo nafikiri ukilifanya utakuwa umetenda haki sana kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani kila mwaka, kila Mbunge hapa, hakuna Mbunge ambaye halilii maji katika eneo lake, umekuwani wimbo wa Taifa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mpango utusaidie, pangeni vipaumbele, kilio cha Wabunge kipokee, tekeleza ili maneno humu ndani yaweze kupungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, susla la utawala bora. Mimi nilikuwa nataka nishauri, maendeleo haya hayawezi kuja kama kuna hofu katika Taifa, kama watu hawana amani katika shughuli zao, kama mtu anafunga duka. Hivi ni mfanyabiashara gani mjinga ambae atakwenda kukopa mkopo wa Benki, afungue biashara halafu mwanaume mmoja anasema kuanzia leo funga maana yake ukifunga duka lake akafungwa na yeye hawatawekeza Mheshimiwa Mpango, na wewe unajua ni mtaalam, hawatawekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna watu ambao ni very sensitive kama matajiri ambao wana fedha zao. Anataka mahali ambapo kuna amani, utulivu na kuaminiana, anakuwa confortable na anawekeza katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika Taifa hili utawala bora na demokrasia imekuwa ni shida. Sisi hata haya mambo tunayozungumza hapa tukitaka kukosoa tu kwamba data hizi si za kweli, Pato la Taifa figure hizi si za kweli unaambiwa ukamatwe uwekwe ndani. Sasa lazima tujadili, maendeleo ni pamoja na demokrasia, maendeleo maana yake ni uhuru wa kuzungumza, kupokea maoni. Kama mnafanya kazi nzuri kwa nini mnakamata watu? Kwa nini watu watishiwe maisha? Kwa nini watu wapigwe risasi? Kama kunafanywa maendeleo, sisi tuacheni tuseme tunavyosema bila kuvunja sheria, bila ku-personalize mambo halafu ninyi mtende kazi. Muwaambie ninyi CHADEMA, CUF mlikuwa mnapiga kelele sisi tulitekeleza hiki na hiki, tushindane kwa namna hiyo. Fanyeni kazi tukose hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hoja zipo nyingi kweli kweli tunazoweza kuzijibu. Hoja zipo na hazina majibu, ni kwa sababu ninyi mna-concentrate kutushughulikia hapa, ni muhimu huu utaratibu uishe. Wekeni uhuru wa kutoa maoni, tuikosoe Serikali, tukosoe mipango ya Mheshimiwa Mpango halafu mkatekeleze mtuambie ninyi mlipiga kelele sasa sisi tumefanya moja, mbili, tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ya bure, bahati nzuri mimi ni mwalimu kitaaluma. Hili jambo ni jema, wanafunzi wameandikishwa darasa la kwanza wengi sana. Sasa shida iliyopo umezuka ugomvi sasa kati ya wazazi na walimu.
Serikali ilisema elimu ni ya bure sasa…

(Hapa kkengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)