Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MUSSA R. NTIMIZI: Nashukuru kwa kupata nafasi na mimi pamoja kwamba ni dakika tano at least nichangie katika Mpango huu ulio mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuleta Mpango huu mzuri ambao na sisi kama Waheshimiwa Wabunge tunatimiza wajibu wetu katika kuongeza yale ambayo tunadhani yanaweza kusaidia katika kuleta maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango huu wa Taifa unajumuisha mipango midogo midogo tuliyokuwa nayo katika maeneo yetu, katika wilaya zetu, katika majimbo yetu ndio wanatengeneza mpango mkubwa wa Taifa letu. Mengi yameshazungumzwa lakini na mimi nilitaka niseme mambo machache kwa haraka haraka kwa sababu ya muda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wamezungumzia eneo la kilimo. Eneo la kilimo likitengenezewa mkakati mkubwa linaweza kusidia mapato ya nchi yetu, linaweza kusaidia wakulima wetu, linaweza kusaidia wakulima wetu, wakapata mapato yaliyo bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi najikita katika zao la tumbaku. Serikali lazima, lazima, lazima iangalie Mpango ulio bora wa kuliimarisha zao la tumbaku. Zipo changamoto nyingi; lakini nataka niseme pamoja na juhudi zinazofanywa na Serikali yetu bado zao la tumbaku halijamkomboa mkulima na halijachangia vizuri Pato la Taifa. Kama zao la tumbaku likisimamiwa vizuri linaweza likachinga katika Pato la Taifa kwa kiasi kukubwa sana. Niombe sana Mheshimiwa Waziri katika Mpango wako tuangalie namna ya kupata soko zuri la tumbaku nina hakika kabisa wakulima wetu kule tuna wahamasisha wafanye kilimo ili waondokane na umaskini, wanaweza kuondokana na umaskini kwa kiasi kikubwa kama zao hili la tumbaku litasimamiwa viilivyo vizuri zaidi.

Halmashauri zetu zinategemea sana sana mapato yanayotokana na kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu miundominu. Nipongeze kwa kuanzisha TARURA, lakini kama walivyosema watu wengine TARURA inahitaji iwezeshwe kifedha ili kusaidia ujenzi wa barabara katika maeneo yetu. Unapohamasisha viwanda, viwanda hivi vinatakiwa vipate pembejeo kutokana na mazao ya wakulima wetu. Wakulima wanalima vijijini barabara ni mbovu, kutoa mazao toka vijijini kuleta katika soko ni tatizo kubwa sana. Tukiimarisha TARURA, malengo yake yakatimizwa sawa sawa, mipango yake ikawa mizuri nina hakika kabisa itatusaidia sana katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la afya, hili tunalizungumza kila siku. Tuweke mpango uliothabiti wa kujenga vituo vya afya katika kila kata katika nchi yetu ya Tanzania. Tunapoimarisha Hospitali za Wilaya na za Mikoa hazitosaidia sana kama hatutoimarisha vituo vya afya katika kila kata, vituo vya afya vitasaidia kupunguza msongamano katika Hospitali za Wilaya na katika Hospitali zetu za Mikoa, hili ni jambo la msingi sana. Katika mpango nimeona tunaimarisha sana Hospitali za Rufaa na za Mikoa. Lakini hazitosaidia sana kama wananchi wengi watakuwa wanatoka katika zahanati zetu wanaenda moja kwa moja kutibiwa kwenye Hospitali za Rufaa. Wanatakiwa wakitoka kwenye zahanati waende kwenye vituo vya afya ili kupunguza msongamano katika Hospitali zetu za Wilaya na za Mikoa; hili ni jambo la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni kuhusu wafugaji wetu. Wafugaji wakitengenezewa mpango ulio bora wataleta pato kwa taifa, viwanda vyetu vitapata bidhaa za maziwa, ngozi na tutapata viwanda vya kutengeneza viatu. Hata hivyo leo wafugaji wanaonekana ni adui katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafugaji hawa ndio wapiga kura wetu, lakini kama nilivyosema tukiangalia vizuri na tukawatengenezea mazingira yaliyo bora wafugaji hawa wataleta pato kubwa sana katika nchi yetu na kuchangia katika kuboresha uchumi wetu. Tuwatengenezee mazingira bora ya kufugia badala ya kuendelea kuangaika nao. Kama hawajatengewa mazingira yaliyo bora tutaendelea kusumbuana naona haitotusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani nimetumia muda wangu vizuri nashukuru kwa kupata muda huo, ahsante sana.