Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Mbaraka Kitwana Dau

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MBARAKA K. DAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetujalia uzima na uhai kwa siku ya leo. Nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa wasilisho lake zuri. Mimi kwa haraka haraka nitaanza na hili ambalo Senator Ndassa jana alilizungumza kwa undani sana hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda wa siku nne hapa tumekuwa tukijadili huu Mpango wetu, lakini wengi waliojikita katika kujadili hili wamezungumza suala la ubia kati ya sekta binafsi na sekta ya umma. Sasa mimi sitaki kurudia kwenye mjadala huo kwa sababu mengi yameshasemwa. Huu Mpango na Waziri mwenyewe anakiri kwamba katika hili hatukufanikiwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nimuombe tu Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind up hoja yake pengine Bunge hili linasubiri sana kusikia kauli yake moja tu akisema kwamba anakivunja kile Kitengo cha Sekta Binafsi pale Wizarani. Aweke timu mpya pale, tuanze upya na hata kama ikiwezekana tumtafute mtaalam wa nje aongoze kile kitengo na hili wala sio jambo geni. Tulipoanzisha TANROADS lilikuwa ni jambo jipya, lilikuwa jambo gumu, tukamuweka raia wa Ghana pale akaanzisha kile kitengo na sasa wenyewe tumeweza kukiendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa namuomba sana Mheshimiwa Waziri, vunja Kitengo cha Sekta Binafsi pale kwenye Wizara yako, tafuta wataalam hata kama ikibidi kutoka nje, tuanze upya, haiwezekani huu mwaka wa tano tunaimba tu sekta binafsi, sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri katika hali ya kawaida hata wewe mwenyewe unatakiwa uwe embarrassed katika situation inavyokwenda sasa hivi. Kila siku tukisoma makabrasha hapa UDART! Hivi UDART ile kweli unaweza sema kwamba ni mfano mzuri wa ushirikiano baina ya sekta ya umma na sekta binafsi? Mheshimiwa Waziri kama ninakuuliza pale, hiyo sekta binafsi mle kwenye UDART imeingiza kiasi gani unaweza ukanijibu? Katika hali ya kawaida zile pesa ni za World Bank na yule aliyeingia pale sijui Simon nani sijui ndiyo sekta binafsi pale ni ubabaishaji mtupu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila siku mimi toka niko Chuo Kikuu nasikia habari ya Chalinze - Dar es Salaam Road Toll mpaka leo iko kwenye makaratasi. Sasa anzisha kitengo kile upya, wape malengo walau kwa mwaka basi hata tukipata mradi mmoja mkubwa mimi naamini tutasonga mbele sana. Haiwezekani Chalinze - Dar es Salaam miaka sijui sita, hiyo UDART mimi kwangu wala siihesabu kama ni mfano mzuri wa ushirikiano baina ya sekta binafsi na sekta ya umma. Lakini katika hali ya kawaida hata hiyo habari inayoitwa kiwanda sijui ya madawa katika hali ya kawaida hicho nacho pia hakiwezi kuwa ndiyo mfano mzuri. Mheshimiwa Waziri tunakuomba sana utakapokuja hapa uanze na kuvunja kile kitengo tuanze upya, wape malengo wakishindwa toa weka wengine mpaka tutafanikiwa, hilo lilikuwa la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nimeangalia huu Mpango, kuna eneo umesema eneo la kuimarisha utalii, biashara na masoko, ujenzi na ukarabati wa kutengeneza miundombinu na kutangaza vivutio vya utalii hususan kile kinachoitwa Southern Circuit, kwa maana ya kwamba utalii wa maeneo ya Kusini. Mimi nitagusia sehemu ndogo tu. Najua eneo la Kusini ni pana sana, nitagusia Kisiwa cha Mafia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kisiwa cha Mafia ni maarufu sana kwa utalii, tuna samaki pale anaitwa potwe (whale shark), ni samaki ambaye ni wa ajabu na ni mkubwa kuliko samaki wote ukiondoa nyangumi ambaye si samaki na samaki huyu hajatangazwa. Lakini hata kama mkitangaza bado kuna suala la miundombinu. Kwa masikitiko makubwa sana Bandari ya Nyamisati huu sasa ni mwaka wa pili bajeti ya mwaka 2015/2016 zimetengwa shilingi bilioni 2.5 mpaka mwaka umekwisha bandari haijajengwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)