Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2018/ 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunijaalia afya njema na mimi niweze kuongea katika Bunge lako hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya yote nianze kumpongeza kipenzi cha Watanzania, mtetezi wa wanyonge, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya. Hii ni tunu tuliyopewa na Mwenyezi Mungu na kama huamini hilo au kama kuna wale ambao hawaamni hilo basi wangeangalia leo jinsi anavyotoa somo pale Uganda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Waziri Mpango kwa kuja na mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo 2018/2019. Na mimi nijikite katika kuchangia hususan katika kilimo. Hatuwezi kuzungumzia mapinduzi ya viwanda bila kuzungumzia mapinduzi ya kilimo. Kilimo ni uti wa mgongo katika taifa hili, lakini mimi ninachoamini au nilichoona uti wa mgongo unaelezewa tu kwenye vitabu lakini sio kwa vitendo. Kama kweli tunataka twende kwenye mapinduzi ya viwanda ni lazima tuhakikishe kwamba tunaboresha kilimo chetu hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima walio wengi hapa nchini wanategemea jembe la mkono. Kwa hiyo, nimuombe sasa Mheshimiwa Mpango, hebu panga mipango yako mizuri sasa kuhakikisha kwamba unaweka mipango mizuri katika wakulima wetu hawa kuwawezesha ili waweze kulima kilimo cha kisasa na kuweza kuzalisha malighafi ambayo itasababisha kujenga katika viwanda vyetu. Ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo kuna suala la maji. Maji ni uhai na Tanzania yetu hii bahati nzuri imezungukwa na miito na maziwa makubwa sana. Lakini kuna changamoto sana ya upatikanaji wa maji. Mheshimiwa Waziri Mpango sasa aje na mpango kabambe, naamini kabisa kwenye vitabu hivi kwa kweli mpango wake ni mzuri kuhusu maji lakini apeleke pesa za kutosha katika suala zima la maji kwa sababu maji ndiyo kila kitu. Ukizungumzia kilimo lazima uzungumzie na maji, kwa hiyo naomba sasa katika mpango wake Mheshimiwa Mpango ahakikishe anaandaa pesa za kutosha kupeleka kule kwa wakulima hususan katika suala zima la kujenga mabwawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuingie kwenye suala la barabara. Barabara ndio uti wa mgongo, ndiyo uchumi katika taifa hili. Ili uchumi wa nchi hii ukue unahitaji barabara. Kwa mfano kule kwetu Lushoto, kuna barabara ambazo zinatakiwa kupandishwa hadhi lakini mpaka sasa ni miaka mitano barabara zile hazijapandishwa hadhi, kwa hiyo nimuombe Mheshimiwa Waziri huyu katika mpango wake huu basi zipandishe barabara zile hadhi. Kuna barabara ya kutoka Mlalo – Ngwelo – Mlola – Makanya – Mlingano hadi Mashewa ambapo barabara hii kwa kweli ni barabara ya kiuchumi endapo itafunguliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala tena la barabara kutoka Mombo – Soni – Lushoto – Mlalo – Mlola, barabara hii ni nyembamba mno kiasi kwamba hata juzi mwezi wa nne tulipopata mafuriko kwa kweli wananchi wa Lushoto walipata taabu sana, walikaa zaidi ya wiki mbili bila kupata huduma za msingi. Kwa hiyo, nimuombe sasa Mheshimiwa Mpango katika mipango yake hii basi apange pesa za kutosha ili barabara ile iweze kupanuliwa. Pamoja na hayo kuna barabara za kupandisha hadhi ziweze nazo kupandishwa hadhi. Pia nimshukuru Dkt. Mpango au niishukuru Serikali yangu kwa kuja na TARURA, Mheshimiwa Dkt. Mpango nakuomba sana TARURA ni jambo zuri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)