Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Waziri Mpango pamoja na timu yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia mapinduzi ya viwanda pia hutoacha kuzungumzia mapinduzi ya kilimo. Niishauri Serikali yangu ipeleke wataalam wa kutosha katika sekta nzima ya kilimo kama Maafisa Ugani pamoja na Maafisa Maendeleo ya Jamii washirikiane kuhakikisha kuwa wanatoa elimu yenye tija kwa wakulima wetu pamoja na Serikali kupeleka pembejeo na mitaji kwa walengwa ambao ni wakulima kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yote haya ni kutaka kuboresha kilimo chetu ili kuwezesha malighafi nyingi zitoke kwenye kilimo ambazo zitatumika katika viwanda vyetu kuliko kutegemea malighafi kutoka nje. Pia katika viwanda vyetu Serikali ihakikishe inasimamia viwanda vyetu vizalishe bidhaa bora zenye viwango kuhakikisha tunashindana na ubora wa masoko ya ndani na nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ndiyo njia kuu pekee ya kiuchumi. Kwa hiyo, niishauri Serikali yangu Tukufu ipeleke fedha za kutosha na kuhakikisha barabara zinaunganisha Mikoa hadi Mikoa na Wilaya hadi Wilaya. Pamoja na barabara hizi muhimu ambazo ndiyo zinazotoa malighafi kutoka vijijini, Serikali ipeleke pesa za kutosha na kuwa na usimamiaji wa karibu kwa kuhakikisha zinapatikana kwa mwaka mzima kuliko ilivyo sasa hasa barabara za Jimbo la Lushoto zimeharibika sana. Kwa hiyo, niiombe Serikali katika Mpango wake huu iangalie kwa jicho la huruma barabara za Lushoto ili wakulima wetu mazao yao yasiozee shambani kama ilivyokuwa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila afya hakutakuwa na maendeleo katika sekta zote hapa nchini. Wananchi wengi wameitikia wito wa kujitolea kujenga zahanati pamoja na vituo vya afya, lakini Serikali haipeleki mafungu kwa ajili ya kumalizia majengo hayo. Niishauri Serikali yangu ipeleke pesa za kutosha ili majengo yale yaweze kukamilika na Watanzania waweze kupata afya njema na kuweza kulitumikia Taifa lao. Hii iende sambamba na kupeleka vifaa vyote vya afya ili kupunguza mlundikano mkubwa katika hospitali zetu za Mikoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ndiyo kila kitu katika maisha ya binadamu. Kwa hiyo, niiombe Serikali katika Mpango wake huu wa mwaka 2018/2019 ihakikishe inamalizia maabara zote ambazo zimeanza kujengwa bila kumaliziwa pamoja na kuongeza vyumba vya madarasa, kujenga vyoo pamoja na kujenga nyumba za walimu na elimu hii iendane na kujenga vyuo vya VETA kila Wilaya. Wilaya ya Lushoto tokea mkoloni hakujawahi kujengwa Chuo cha VETA. Kwa hiyo, Mheshimiwa Dkt. Mpango katika awamu hii naomba utenge pesa za kujenga Chuo cha VETA katika Wilaya ya Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia mazingira tuwe tunahakikisha tunapanda miti nchi nzima pamoja na kusimamia sheria kikamilifu ili wananchi wetu wawe wanatunza vyanzo vyetu vya maji na Serikali ihakikishe inawawezesha wananchi kwa kuwapatia miche ili wapande
katika mashamba yao. Kwa mfano, katika Jimbo la Lushoto kuna misitu imeungua moto lakini kuna kikundi cha vijana kinaitwa Friends of Usambara mpaka sasa kina miche zaidi ya milioni 10 na wao wenyewe wameamua kupanda miti katika maeneo yote ya misitu yaliyoungua. Kwa hiyo, niishauri Serikali iweze kusaidia vikundi kama hivi ambavyo vipo hapa nchini na vikundi hivi ikisimamiwa vizuri tutarudisha uoto wetu wa asili uliopotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyoanzishwa TARURA, niishauri Serikali ije na mpango wa kuanzisha pia wa Wakala wa Maji Vijijini na Serikali ipeleke kwa wakati umeme vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.