Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Grace Victor Tendega

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa Sheria ya Fedha za Umma ya mwaka 2001 (The Public Finance Act, 2001 No.4) inaitaka Serikali kuleta Bungeni bajeti ya nyongeza kwa ajili ya kupata idhini ya Bunge ikiwa fedha za awali hazikutosha. Kwa sasa kuna baadhi ya miradi ya maendeleo inatekelezwa nje ya bajeti na hatujaona Serikali ikiomba bajeti ya nyongeza, mfano, ujenzi wa mabweni ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ujenzi wa barabara za juu Dar es Salaam, ni baadhi tu. Kitendo cha Serikali kuamua kufanya matumizi bila kupata idhini ya Bunge ni uvunjaji wa Katiba na sheria na kitendo hicho kinaweza kuruhusu mianya ya rushwa na ubadhirifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mikopo ya elimu ya juu, katika mwaka wa fedha 2016/2017 wanafunzi waliopata mikopo walikuwa 20,183 na wanafunzi takribani 27,053 walikosa mikopo. Mheshimiwa Rais katika kampeni za mwaka 2015 alisema yeye atakuwa muarobaini wa mikopo ya elimu ya juu. Utolewaji wa mikopo umekuwa na ubaguzi na usumbufu mkubwa, ni vyema Serikali katika Mpango wake iweke commitment ya kuandaa mfumo bora wa utoaji mikopo ili kuondokana na tatizo hili. Vilevile kumekuwa na tatizo au hakuna mfumo mzuri wa urejeshaji mikopo kwani sheria iliyopo inawaumiza sana waliopo katika ajira kukatwa asilimia kubwa kulingana na kipato wanachopata na kushindwa kuhimili maisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haionyeshi uwezo katika kuziwezesha sekta binafsi kukua ili ziweze kuipunguzia Serikali mzigo wa walio wengi kukosa ajira. Wafanyabiashara walio wengi wamefunga biashara zao au kupunguza wafanyakazi kutokana na kushindwa kumudu gharama za uendeshaji, kushuka kwa mapato kwa baadhi ya makampuni, mfano, viwanda vya vinywaji, makampuni ya kitalii, nyumba za starehe zikiwemo baa na hoteli. Mfumo huu unaangamiza kabisa sekta binafsi. Sekta binafsi ndiyo inayochangia mapato ya Serikali kupitia kodi inayokusanywa kwa bidhaa na waajiriwa. Vilevile kumekuwa na tabia ya kuwatishia wafanyabiashara kufunga makampuni kiholela, hii inaongeza umaskini kwa Watanzania walio wengi. Hivyo, nashauri Mpango huu uzingatie na uweke kipaumbele katika kuwezesha sekta binafsi kufanya kazi bila bughudha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa viwanda, kama Tanzania ya viwanda ni uhalisia na siyo ndoto basi suala hili lisingekuwa ni la matamko kwani hivi karibuni Waziri wa TAMISEMI amenukuliwa na vyombo vya habari akieleza kuwa kila mkoa kujenga viwanda 100 ambapo hadi Desemba, 2018 katika Mikoa yote Tanzania Bara inatakiwa kuwa na viwanda 2,600. Kama miaka yote iliyopita imeshindikana kufufua tu viwanda vilivyokuwepo hii leo ya mwaka mmoja itawezekana? Kwa Mkoa wangu wa Iringa tu kulikuwa na viwanda vifuatavyo:-

1. Kiwanda cha Vifaa vya Nyumbani kama masufuria kiliitwa IMAC;

2. Kiwanda cha Nyuzi na Nguo (COTEX);

3. TANCUT Almasi;

4. Kiwanda cha Magurudumu ya Magari (VACULUG);

5. Kiwanda cha Tumbaku;

6. Kiwanda cha Coca cola; na

7. SIDO

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyote hivyo havipo tena. Maelekezo hayo ya viwanda 100 yanashangaza kwa sababu kama mikopo kwa sekta binafsi imepungua na kama Serikali haifanyi biashara hivyo viwanda vitajengwa na nani? Serikali inabidi ijipambanue ili kujua mfumo upi inaufuata kama ni uchumi wa kijamaa au uchumi wa kibepari au soko huria ili ijikite madhubuti katika mfumo itakaoamua kuufuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ndicho kinachotoa ajira kwa Watanzania zaidi ya asilimia 70. Katika Mpango huu bado sekta hii inaendelea kupuuzwa na matokeo yake ni kudorora kwa uchumi na hiyo Tanzania ya viwanda inaendelea kuwa ndoto. Kuna changamoto kwenye kilimo kwani wakulima hawapati pembejeo kwa wakati, kilimo cha umwagiliaji hakitiliwi mkazo, Maafisa Ugani hawako wa kutosha, baadhi ya mabenki kutokopesha wakulima kwa madai kwamba mikopo katika sekta ya kilimo huwa haina uhakika wa kurudi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango huu Serikali inatakiwa kubuni utaratibu maalum wa kuziwezesha benki za biashara kuweza kutoa mikopo hiyo. Wanawake na vijana wakiwezeshwa hasa katika mikopo ya kilimo na ufugaji ukosefu wa ajira utapungua.