Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nichangie hoja hii ya Kamati hizi mbili. Kwanza nizipongeze sana hizi Kamati mbili kwa kazi nzuri wanazozifanya lakini tatizo lipo, hawapewi fedha za kwenda kukagua miradi, wanakagua makaratasi tu. Sasa bila kwenda kuona miradi ile value for money kwa kweli inakuwa ni kazi bure tu. Unaweza kukuta shule imejengwa lakini kama haikukaguliwa madirisha mabovu, kuna nyufa na mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuchelewa kwa fedha za miradi ya maendeleo. Bunge kama Bunge sisi ndio tunaopitisha bajeti hapa. Bajeti za Halmashauri za Wilaya pamoja na bajeti ya Serikali Kuu, lakini jambo la kusikitisha fedha hazifiki kwa wakati. Hakuna Halmashauri hata moja hapa ambayo imeshapata fedha za ruzuku zaidi ya asilimia 40 hakuna. Sasa nauliza huko Hazina kuna nini, kama TRA wanakusanya kila mwezi hela za kutosha kwa nini fedha hizi zisipelekwe Wilayani. (Makofi)

Mheshiniwa Mwenyekiti, miradi ya maji kuchelewa, nina masikitiko makubwa sana kuna visima sita vimechimbwa Wilaya ya Mpwapwa tangu Agosti, 2016, lakini mpaka leo hakuna pump, hakuna bomba wala hakuna nini. Kwa hiyo, visima vile vimechimbwa vimekuwa kama ni white elephant wananchi wanaangalia tu. Sasa namshukuru sana Waziri wa TAMISEMI, MheshimiwaJafo anajitahidi sana kutembelea miradi hii, tulifika naye Kijiji cha Mima akaona huu mradi maji, akaona ujenzi wa kituo cha afya kinavyoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mawaziri mtembelee miradi hii, bila kutembelea ndugu zangu, msikae maofisini mkadhani kwamba miradi inakwenda vizuri, kumbe miradi imekwama. Hata hivyo, awamu hii niwapongeze Mawaziri wanajitahidi kutembelea miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halmashauri nyingi zilikuwa zinapata hati chafu, lakini baada ya kuunda hii Kamati ya LAAC imefanya kazi nzuri sana, sasa hivi ukifanya utafiti ni Halmashauri chache tu wanapata hati chafu, kwa hiyo, niwashukururu sana lakini kama nilivyosema wapewe fedha kwa ajili ya kwenda kuona ile miradi value for money sio kukagua makaratasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, kodi ya majengo bado tunasistiza sisi Wabunge kodi ya majengo irudishwe kwenye halmashauri zenyewe sasa kodi ya majengo (property tax) wanakusanya TRA ni kweli wanakusanya lakini wanakusanya mwaka mzima ndiyo waanze kugawa kwenye Halmashauri miradi hiyo si imekwama?

Mheshimiwa Mwenyekiti, halmashauri zilikuwa zinakusanya property tax kila quarterly wanaanza kutumia zile fedha. Kwa hiyo, nashauri kwamba kwa sababu ni chanzo kimojawapo cha mapato ya halmashauri kwa sababu halmashauri nyingi hazina vyanzo vya mapato kwa hiyo kodi ya majengo ndio kilikuwa chanzo kimojawapo. Kwa hiyo, ombi langu chanzo hiki cha mapato kirudishwe Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watumishi kukaimu muda mrefu katika Halmashauri; ni kweli wanakaimu muda mrefu sana. Ukienda kila Halmashauri ukimuliza huyu, mimi ni Afisa Elimu Kaimu, mimi ni Mhandisi wa Maji Kaimu, mimi sijui nani Kaimu. Sasa nashauri Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI kama hawa watu wana ujuzi wa kutosha wana-qualification za kupandishwa vyeo kwa nini wasithibitishwe kushika nafasi hizo. Waendelee kukaimu miaka miwili, miaka mitatu hapana. Kwa hiyo, wasikaimu muda mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro kati ya Madiwani na Watendaji wa Halmashauri; bahati nzuri nilikuwa Diwani, Mwenyekiti wa Halmashauri na Mbunge nimejifunza mambo mengi sana. Sisi ndiyo tumeanzisha Halmashauri ya Wilaya mwaka 1984, kulikuwa na matatizo makubwa sana, lakini sasa yanaanza kupungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, semina au mafunzo kwa Madiwani ni muhimu. Sisi tulikuwa tunakwenda mafunzo Hombolo tunapewa mafunzo ili kupunguza migogoro kati ya Watendaji na Madiwani. Utakuta Madiwani wanamkataa Mkurugenzi inawezekana hakuna sababu zozote za msingi au Madiwani kuingilia utendaji, hilo nalo ni tatizo, lakini Madiwani wakipewa mafunzo nina hakika kabisa hii migogoro itapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache naunga mkono hoja hizi zote mbili za Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC).