Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie kwenye hoja hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo ningependa nichangie ni kwamba kwenye hoja hii mwaka jana tulizungumza sana kuhusu uwezo wa baadhi ya Wakurugenzi wa Halmashauri zetu. Tuliishauri Serikali kwa makusudi kabisa ijitahidi kufanya semina, warsha na mafunzo kwa ajili ya kuwajengea uwezo baadhi ya Wakurugenzi ambao wameingia katika kazi hii kutoka kwenye shughuli nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo ya utendaji wao umesababisha migogoro kati yao na baadhi ya Watendaji wa Halmashauri. Wakurugenzi wakifikiria kwamba kule kuwa wasimamizi wa Halmashauri basi wao ndiyo kila kitu, umesababisha migogoro kati yao na Madiwani na baadhi ya Halmashauri migogoro hii inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapokwenda kwenye Halmashauri na kukuta Mkurugenzi hayupo katika maelewano mazuri na Watendaji pamoja na Madiwani, kwa vyovyote vile Halmashauri haiendi. Ikumbukwe kwamba, hizi Halmashauri ni za wananchi, kwa hiyo Mkurugenzi hawezi kusimama kwenye Halmashauri kana kwamba yeye ndiyo mwenye kujua kila kitu, yeye ndiye mamlaka ya kila kitu, akikataa ushauri na mambo kama hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa kwanza kabisa naiomba Serikali iendelee kupitia uwezo wa Wakurugenzi wake na isaidie kuwapa uwezo ili waweze kusimamia shughuli za Halmashauri vizuri, vinginevyo tutapata shida, kazi hazitaenda sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sambamba na hilo tumetembelea baadhi ya Halmashauri, miradi ya maendeleo haisimamiwi sawasawa. Unakuta kuna ile Idara ya Mipango ya Halmashauri ni kana kwamba inajiweka pembeni mambo yanakwenda yenyewe kwenye maeneo mbalimbali ya miradi, lakini unapohoji zile Idara utasikia kwamba ohoo, hili halikupitia kwetu na kadhalika. Ndio maana nasema kama Mkurugenzi yuko vizuri na Wakuu wake wa Idara mambo kama haya yasingeweza kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano tu wa Idara ya Elimu, hivi majuzi Mheshimiwa Rais kwa nia nzuri kabisa ametoa maagizo kwamba michango mbalimbali katika shule ambayo haina tija iondolewe, hiki ni kilio cha Watanzania, lakini sasa kutokana na uwezo mdogo wa Wakurugenzi lazima niseme na hili nawaomba Rais alisikie, uwezo mdogo wa Wakurugenzi umewafanya wakatafsiri lile agizo la Rais vibaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu zipo Halmashauri, zipo Wilaya ambazo wazazi katika kila shule walishakubaliana utaratibu wao wa namna watoto wao, kwa mfano wanavyopata chakula mashuleni, utaratibu huo hauhusiani na Mkuu wa Shule, hauhusiani na Mkurugenzi, wazazi wana chama chao, wana bajeti zao, wao ndiyo wanaopanga watoto wale nini, wao ndiyo wanaopanga bajeti iwe namna gani, kuni zipatikane wapi, chakula kipatikane wapi, kwa hiyo watoto wamekuwa wakila shuleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naelewa upo uhusiano mkubwa kabisa kati ya tumbo na kichwa. Mtoto ambaye hajashiba hawezi hata siku moja akazingatia yale ambayo anaelekezwa shuleni. Sasa Wakurugenzi hawa baadhi yao wamekuwa kama robot, wamekwenda wametengeneza majedwali, wameandika barua, wamekwenda kuzuia wale wazazi ambao kwa nia nzuri kabisa walikuwa wanachanga chakula kwa ajili ya watoto wao. Sasa nashangaa hapa tunaisaidia nchi au tunaibomoa, mtoto anaamka saa 11 alfajiri nyumbani, hajanywa uji, hajanywa chai, anakwenda shuleni hakuna chochote, halafu unasema kwamba tunakuza elimu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa Wakurugenzi walimtafsiri Rais vibaya, yako maeneo, kwa mfano katika Jimbo langu, tulikuwa hatuna tatizo kabisa lakini baada ya tangazo lile wamekwenda wale wazazi wamegawana chakula ambacho tayari walikuwa wamenunua, wamegawana kuni ambazo tayari zilikuwa shuleni, wamegawana pesa ambazo zilikuwa tayari zimeshakusanywa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa sababu Waziri wa Elimu yupo hapa, atusaidie hawa Wakurugenzi waweze kuelewa vizuri agizo la Serikali lilikuwa nini kwa sababu sisi hatuna shida. Rombo kwa mfano, shule zote za Sekondari na za Msingi watoto wanakula shule na huhitaji kabisa kauli ya Mkuu wa Shule wala Mkurugenzi wala nini, wazazi wana vyama vyao, wanaitana wanajichangisha wenyewe, wanatengeneza bajeti wenyewe, wanaajiri mpishi wenyewe, wananunua kuni wenyewe. Sasa leo Mkurugenzi ukifikia mahali ukasema Rais kasema, matokeo yake hata Rais atachukiwa! Kwa sababu Wazazi kule tafsiri ni kwamba anachokula mtoto mchana nyumbani ndicho hicho tunaamishia shuleni, kwa hiyo hakuna tatizo lolote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo narudia kusema la kwangu ni hilo kubwa kwamba, baadhi ya Wakurugenzi wasiwe wanapokea maagizo ya Serikali halafu wanakuwa kama robot, sijui wametiwa hofu ya namna gani! Bila hata maelezo bila hata nini wanaingia katika utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kulisema, hapa tunafanya bajeti, kila Halmashauri inajua kwamba bajeti ya maendeleo katika Halmashauri ni kiasi fulani. Kinachotokea ni kwamba, Halmashauri nyingi ambazo tumezitembelea fedha za maendeleo hazifiki kwa wakati au hazifiki kabisa, matokeo yake ni kama vile Halmashauri zimefungwa mikono na miguu halafu zinaambiwa kimbia, haziwezi kukimbia haziwezi kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba fedha za miradi ya maendeleo katika Halmashauri ziende kwa wakati na kama hazijaenda basi utaratibu uelekezwe ili wajue watafanya nini, vinginevyo ziko Halmashauri ambazo zitaendelea kuachwa tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo ningependa kuchangia kwa sababu Mheshimiwa Gekul ameniomba dakika tano na nataka nimpatie ni kwamba Serikali imejitahidi sana kupeleka watumishi, lakini bado kuna Halmashauri ambazo Ikama haijakaa vizuri, bado kuna Halmashauri ambazo watumishi wengi wanakaimu. Mtu anayekaimu hana hakika na ile nafasi hawezi akatoa maamuzi, kwa hiyo bado tunasisitiza na tunaiomba Serikali kwamba, Wakuu wa Idara katika Halmashauri zetu ifanyike jitihada wale wanaokaimu waweze kuthibitishwa ili waweze kufanya kazi yao kwa uhakika zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti ni hayo, naomba muda wangu uliobaki amalizie Mheshimiwa Gekul.