Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja zetu mbili zilizopo hapa mezani, hoja ya Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa na Kamati Hesabu za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa niwapongeze sana Wenyeviti wetu, niwapongeze Wajumbe wa Kamati wote wa Kamati zote mbili, lakini nisiwe nimepungukiwa fadhira niishukuru sana Ofisi ya CAG kwa jinsi inavyotusaidia Wajumbe wa Kamati hizi mbili kutuwezesha kiutaalam lakini kutusaidia kutuongoza namna gani tunaweza kuisimamia Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kuchangia hoja ya Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa. Halmashauri mbalimbali zimekaguliwa nasi tumejaribu kuwahoji Maafisa Masuuli kama taarifa zetu zinavyoonesha, tumetembelea baadhi ya Halmashauri, lakini jambo kubwa ambalo
ningependa nilizungumzie zaidi hapa ni tatizo kubwa la maji. Kwanza kabisa naomba mtambue ndugu zangu, Wabunge wenzangu pamoja na Serikali kwamba kimsingi maji hayana mbadala, panapotakiwa maji lazima yapatikane maji, tatizo kubwa la nchi yetu mpaka sasa hivi tuna shida kubwa sana ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu cha ajabu kuliko yote maji ndiyo kitu ambacho kina teknolojia rahisi, sasa najiuliza tatizo liko wapi! Kama maji hata kwa asili tu watu walichimba visima, walitengeneza mifereji wakapata maji wakatumia, leo hii pamoja na maendeleo tunayosema tunayo tunashindwa kupata maji katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda katika Halmashauri unakutana na shida mbili kubwa, shida ya kwanza unakutana na matatizo ya usanifu wa miradi ya maji, shida ya pili unakuta kwamba mwenye mfuko wa pesa yuko Wizarani Halmashauri imekaa tu pale, mradi unapotekelezwa yuko mtu hapa katikati anaitwa Mhandisi Mshauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mhandishi Mshauri anaajiriwa na Halmashauri, lakini mradi unapoharibika Halmashauri hana cha kusema, ukiwauliza wataalam wa Halmashauri wanasema Mhandisi Mshauri alishauri hivyo na alisimamia hivyo. Sasa unajiuliza kwa mfano, tumeenda mradi mmoja kule Tanga unaitwa Changarikwa, mabomba mita 300 yanapasuka siyo hiyo tu, hata katika Halmashauri yangu ya Mji Njombe mradi wa maji wa Utengule mabomba yanapasuka. Ukiwauliza wataalam wa Halmashauri wanasema Mhandisi Mshauri ndio aliyesimamia huu mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tujiulize sasa kama Mhandisi Mshauri kimekuwa ni kichaka tutafute njia nyingine ya kufanya. Kama Mkoani kuna Injinia wa maji, Halmashauri yenyewe ina Injinia ya maji kwa nini miradi wasisimamie wenyewe, teknolojia ya maji ni ndogo sana. Tunagawa fedha hizi kidogo kuwapa Wahandisi Washauri wakati tumeajiri Wahandisi ndani ya Halmashauri wapo na miradi inakwama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kwenye upande wa ubunifu wa hii miradi, unakwenda mahala unakutana na mradi umebuniwa ni borehole wamechimba kisima, lakini umefungwa mashine ya diesel ifue umeme halafu ule umeme uingie kwenye submersible pump uendeshe ile pump ya maji. Mwananchi wa kawaida hawezi kulipa maji hayo, hawezi kulipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeenda kutembelea mradi wa Mkonze hapa Dodoma tumeona hali hiyo, kwamba imefikia mahali wananchi kisima wanacho, miundombinu ipo lakini wanashindwa kuuhudumia ule mfumo wakaamua kumpa mtu tu aendeshe. Mtu yule amevuta umeme zaidi ya kilometa mbili. Sasa unajiuliza Serikali imeshindwaje kuvuta umeme ukaingia kwenye ile pampu ya maji mpaka mtu binafsi amefanya?(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi mingi ya maji inaharibika kwa sababu wabunifu wa miradi au mafungu yanayoletwa yanakuja na maelekezo kwamba huyu ndio Mhandisi Mwelekezi, atasimamia mradi huo ama atawabunia huo mradi. Nitoe ushauri kwa Serikali, tufanye haraka tuanzishe Wakala wa Maji Vijijini ili kusudi jambo la Maji lishughulikiwe na Wizara. Kama ni Wizara ishughulikie Wizara, kuanzia mwanzo ubunifu, usimamizi, utekelezaji, ulipaji na kila kitu. Kusiwe na kusigana kwamba Halmashauri mara Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii certificate nyingi za maji hazijalipwa. Wapi zimekwama? Haijulikani! Wakandarasi wamefanya kazi hawalipwi. Miradi ya maji inaharibika kwa sababu Mkandarasi anakuwa amefanya kazi lakini hajalipwa. Matokeo yake muda unakwenda mrefu halafu gharama zinaongezeka za mradi Mkandarasi anakuwa hayuko tayari kuendelea kutengeneza ule mradi. Kwa hiyo naiomba sana Serikali harakisheni huo mchakato wa kuunda Wakala wa Maji ambao mwaka jana tumelalamika sana hapa Bungeni, nina imani Serikali ni sikivu italifanya hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni Idara ya Uhandisi, unatembelea miradi ya ujenzi wa majengo mbalimbali ya Serikali unashindwa kuelewa kwamba hivi huyu ni Mhandisi kweli ambaye anastahili kuitwa Mhandisi? Kwa mfano, tulienda Tanga kutembelea Shule moja ya Msingi unakwenda kuangalia limejengwa jengo la msalani kwa ajili ya wanafunzi, lakini wote tunajua msala wa wanafunzi unatakiwa uweje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unamuuliza Mhandisi anasema aah! mchoro uliletwa hivyo. Sasa unajiuliza wewe Mhandisi ulishindwaje kushauri? Kwa hiyo, tuna shida kubwa sana hata kwa hawa Wahandisi wetu wa Halmashauri, fedha nyingi inakwenda lakini uwezo wao wa kusimamia hiyo fedha ya kusimamia miradi ni mdogo sana.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo linaleta shida kwenye Halmashauri zetu ni uchache wa wataalam hasa Wakuu wa Idara. Halmashauri nyingi ambazo tumepitia mahesabu yake kuna upungufu mkubwa sana wa Wakuu wa Idara. Kwa hiyo, inapokuwa kwamba Halmashauri haina Mkuu wa Idara au Idara fulani Mkuu wake anakaimu, matokeo yake ni kwamba hata maamuzi yake yanakuwa na sura hiyo ya kukaimu kaimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza anakuwa hajiamini, anashindwa kutoa maamuzi, anashindwa kufikiria kwamba idara yangu hii iendeje na niipangeje. Naomba kama TAMISEMI tunataka tuende vizuri, hawa wataalam wetu basi tuwathibitishe mapema. Tutoe maelekezo kwa Wakurugenzi kwamba ikiwa kuna mazingira ya kukaimu yanatakiwa yawepo, basi wawepo Wataalam ambao wana sifa ndio wakaimu hizo nafasi halafu muda ukifika wathibitishwe ili kuondoa hiyo nafasi ambayo inakuja kuleta ombwe hapo baadaye kwamba maamuzi hayafanyiki, shughuli zinachelewa ni kwa sababu tu kwamba mtu hajathibitishwa, lakini tukumbuke kwamba wananchi wanakosa huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ukiangalia ushirikishaji wa kiidara. Idara ya ujenzi inapokuwa inatekeleza mradi kwa mfano tunataka kutekeleza mradi wa afya, watu wa afya hawashirikishwi. Tumekwenda Tanga tumekuta Idara ya Maji inatekeleza mradi kwa ajili ya wananchi, lakini wakati huohuo kuna sehemu ya kunyweshea ng’ombe wanaita hozi, hozi za kunyweshea ng’ombe mtu wa mifugo hajui kabisa. Imejengwa hozi, ng’ombe hawezi kunywa yale maji. Sasa unajiuliza, hili hozi alikuwa anajengewa nani? Kwa hiyo hapo kuna tatizo la ushirikishwaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekwenda mahali tumekuta kituo cha afya kimejengwa kizuri sana, lakini ukiangalia mahali lilipowekwa jengo la upasuaji inaonekana kwamba kwenye mpango wa ujenzi kulikuwa hakuna ushirikishwaji. Wamejenga lakini hakuna miundombinu sasa inayoweza kuunganisha kati ya jengo la upasuaji na majengo mengine ya kile kituo cha afya, matokeo yake jengo hilo la upasuaji halitumiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niseme kwenye mipango yetu ya wataalam wetu wa Halmashauri pamoja na wataalam elekezi wanaanzisha miradi lakini matokeo yake mradi unafika mwishoni, mradi ni wa maji unafika mwishoni wanapotaka kuwasha pampu za maji zianze kufanya kazi unaambiwa hapa pana low voltage. Sasa unajiuliza jamani hivi kuna maana gani ya kumweka mtu msomi hapa? Kama hakuweza kuliona hilo kabla akaona kwamba hapa pana low voltage, naleta pampu za maji zenye uwezo huu, niwasiliane na wanaohusika na maji ili wajue kabisa kwamba pampu za maji zinazoletwa hapa zina uwezo, zinaweza zikatumia umeme huu. Mradi umekamilika lakini wanashindwa kwenda kwa sababu tu pampu za maji hazifanyi kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ni pale ambapo Wataalam wa Halmashauri pamoja na hawa Wahandisi Wasimamizi wanafikia mahala kuwalipa Wakandarasi kazi hazijakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wataalam wa Halmashauri wanathibitisha kazi ya Mkandarasi wakati kazi haijakamilika. Nitatoa mifano hii ya Tanga kwa sababu ndiko ambako tumefanya ziara. Unakwenda pale unamuuliza Mhandisi wewe hapa kwenye tenki lenu umesema kuna level indicator iko wapi hapa kwenye tenki? Yule akiamini kwamba sisi ni Wanasiasa hatujui level indicator anatuambia level indicator ipo kwenye DP.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukimuuliza wewe level indicator inakaa kwenye DP? Ukimbana kidogo na kumtikisa ndiyo anakiri kwamba aah! Mkandarasi hakuweka, lakini ameshalipwa na alishakwenda na muda wa matazamio ulishapita. Kwa hiyo ni jambo la kusikitisha sana unapokuwa na wataalam ambao wanathibitisha na Serikali inatoa fedha halafu kazi inakuwa haijakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningelipenda nilisemee ni kama walivyosema wenzangu. Baadhi ya Halmashauri kweli Wakurugenzi wake hawatilii maanani sana wajibu wao kama Wakurugenzi, wakipewa hoja za Kamati hawajibu. Hii inaleta shida sana wamebuni utaratibu wanajua kabisa kwamba Kamati inakaa miaka miwili na nusu baada ya hapo Kamati itamaliza muda wake itaingia Kamati nyingine. Wanajua kabisa kwamba hoja kwa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali huwa inakwenda kwa muda maalum, muda huo ukipita hiyo hoja inakuwa hoja mfu hakuna atakayekuja kuibua tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naiomba Serikali iangalie ni kwa namna gani sasa iweke utaratibu pamoja na kwamba hizi hoja zingine zinakuwa hazijajibiwa, lakini uwepo utaratibu wa kusema kwamba hoja hizi zinafuatiliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho nisisitize tu kwamba maoni ya Kamati naomba yazingatiwe hasa lile ambalo tunasema kwamba tunaomba Bunge liazimie kwamba sasa iundwe Kamati Maalum, ifuatilie matatizo ya miradi ya maji katika nchi yetu, kwa sababu maji hayana mbadala. Bila maji nafikiri hamna ambaye leo angeweza kutokea humu ndani. Kama wote tungekosa maji tusingetokea ndani ya Bunge leo kwa sababu tumekosa maji. Kwa sababu maji hayana mbadala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiunda Kamati hii ndiyo itasaidia kuieleza Serikali na kuionesha Serikali upungufu ulipo na kuona kwamba nini sasa kifanyike. Kwa sababu hakuna mahali ambapo tuna mradi wa maji mzuri wa mfano kusema kwamba mradi huu kwa kweli umetekelezwa bila matatizo. Mradi utaona umetekelezwa lakini mabomba yanapasuka, mradi umekamilika maji hayatoki, mradi umekamilika wananchi hawawezi kuundesha ule mradi kwa sababu ya gharama zake. Limejengwa bwawa la umwagiliaji hakuna wakulima wanaohusika na kilimo, limejengwa bwawa la umwagiliaji bwawa limepasuka. Kwa hiyo ni matatizo mwanzo mpaka mwisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana mapendekezo ya Kamati Bunge hili liridhie na yawe ni maazimio ili kusudi yaweze kusaidia kutatua tatizo la maji. Tatizo la maji katika nchi yetu ndio tatizo kubwa na linamgusa kila mwanachi, tukitatua tatizo la maji tutakuwa tumetatua matatizo mengi sana, magonjwa yote ya matumbo yatakuwa yamekwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tuangalie bajeti ya dawa za matumbo ni kiasi gani, matumbo wananchi wanaumwa kwa sababu tu ya kukosa maji, lakini wakipata maji safi maana yake tumeokoa hiyo fedha wananchi wote watakuwa na afya tutaendelea na miradi mingine. Kwa hiyo, niombe sana hilo lizingatiwe tutatue tatizo la maji kwa wananchi ili kusudi wananchi wetu wawe na maji na waweze kufanya maendeleo vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.