Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia dakika tano nina mambo mengi lakini nitajitahidi kuongea kwa muda niliopatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kuishukuru Kamati kwa taarifa lakini pia niwashukuru Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia na hususani maeneo ambayo yanahusu sekta ya elimu. Kwa hiyo, nitaanza moja kwa moja kuzungumzia suala la Mlimani City ambalo limezungumzwa sana kwenye Kamati lakini pia limechangiwa na Waheshimiwa Wajumbe wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba Serikali inatambua kwamba katika utekelezaji wa mkataba huu wa Mlimani City yapo maeneo ambayo kuna ukakasi katika utekelezaji, na tayari Serikali ilikwishaanza kuchukua hatua. Kama ambavyo Kamati imeeleza kwamba imekuwa hairidhishwi na mazungumzo kati ya mwekezaji na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ni kweli kulikuwa na ugumu hata wa hawa watu kukaa mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba tarai Serikali imekwishamlazimisha yule mwekezaji kufanya mazungumzo na mwekezaji amekiwshakubali na sasa hivi Serikali inaangalia ni nani awe kwenye timu ya majadiliano ili kuangalia vipengele vya mkataba ambavyo havitekelezwi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilihakikishie Bunge kwamba Serikali ya Awamu ya Tano ina dhamira ya dhati ya kulinda rasilimali na ndiyo maana tulileta hapa Bungeni Sheria ya kulinda rasilimali yetu. Kwa hiyo, hili halina mjadala lazima Watanzania wanufaike na rasilimali yao, pale mwekezaji amechukua ardhi, kwa hiyo, lazima Serikali ihakikishe tunanufaika kama ambavyo imekusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kwamba miaka 13 sasa mradi wa hoteli ya nyota tatu bado haujaanza. Ni kweli kwamba bado haijaanza kujengwa, lakini niseme kwamba Chuo Kikuu cha Dar es Salaam bado kinamkomalia mwekezaji na kwa sababu muda wa kumaliza uwekezaji ni Disemba, 2019. Tutahakikisha kwamba hilo suala tunaendelea kulisimamia kama ambavyo liko kwenye mkataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme tu kwamba baadhi ya wachangiaji wamekuwa wakionesha kwamba huu mradi hauna manufaa kabisa. Naomba tu kwa ajili ya kuweka records vizuri; niseme tu kwamba hwa wa Mlimani city wamekuwa wakikilipa Chuo Kikuu cha Dar es salaam takribani bilioni mbili kwa mwezi na hata zile samani zilizowekwa katika hosteli mpya za Chuo Kikuu cha Dar es salaam zimenunuliwa kwa kutumia fedha ambazo zinalipwa na mwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile pia huu mradi umeweza kutengeneza ajira kwa Watanzania zaidi ya 1,600 ajira za moja kwa moja na ajira ambazo tunasema ni indirect employment. Pia hili eneo limekuwa sehemu ambayo watu wengi wamekuwa wakienda pale kupumzika na kupata burudani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa nataka kusema kwamba si kwamba hakuna manufaa kabisa, lakini kuna vipengele vya mkataba ambavyo havitekelezwi vizuri na hivyo Serikali tayari imeshamlazimisha yule mwekezaji ambaye alikuwa na ugumu wa kuzungumza na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nikuhakikishie kwamba chini ya uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano hakuna mtu yoyote ambaye anataka kuhujumu rasilimali yetu atakaebaki salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala ambalo kaka yangu Paroko Selasini alizungumzia kuhusiana na utekelezaji wa elimu bila malipo. Kwanza nimshukuru sana kwa sababu naona anaelewa vizuri waraka huu ambao ndio unatoa mwongozo wa namna ya kutekeleza elimu bila malipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda niseme tu suala ambalo amelizungumzia ambalo limeleta ukakasi. Baada ya sisi kukemea wale ambao walikuwa wanatoa michango ambayo ni kinyume na maelekezo hayo; sasa kuna watu wengine wanataka kupotosha, wanasema kwamba hata vyakula kwa wanafunzi wa kutwa hawaruhusiwi kuchangia hii si kweli, huu waraka umebainisha bayana majukumu ya wadau mbalimbali; na kwa ridhaa yako na kwasababu hili jambo ni muhimu kwa Taifa naomba uniruhusu nitolee ufafanuzi ili mkanganyiko unaondelea usiendelee kujitokeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, waraka unasema wazi kabisa, wajibu wa Mkuu wa Shule ni kuwapa maelekezo wazazi kuhusu aina na vifaa vinavyohitajika. mfano rangi ya kitambaa cha sare ya shule, idadi ya madaftari, vitabu na kadhalika. Kilichokuwa kinajitokeza baadhi ya walimu walikuwa wanalazimisha wazazi kununua sare shuleni kwa bei ambayo ilikuwa ni kubwa ukilinganisha na vile ambavyo mzazi angeweza kununua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye suala la chakula ambalo limeleta sintofahamu; huu waraka unasema wazi kabisa kwamba ni jukumu la mkuu wa shule kushirikiana na jamii katika kuweka utaratibu wa kutoa huduma ya chakula cha mchana kwa wanafunzi wa kutwa au kutoa chakula na husuma nyingine kwa wanafunzi wa bweni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye Kamati ya Shule pia inasema ni jukumu la Kamati ya Shule kushirikiana na jamii katika kuweka utaratibu wa kutoa huduma ya chakula kwa wanafunzi wa bweni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu ka kusema kwamba, hakuna mahali ambapo ama Serikali kwa kupitia waraka ama ufafanuzi wowote ambao umetolewa na viongozi umekataza wazazi kwa hiari yao kuweka utaratibu wa chakula na michango mingine shuleni. Kwa hiyo niwatake wakurugenzi na watu wote ambao wanasimamia utaratibu huu kuhakikisha kwamba wanazingatia huu waraka kama ambavyo umeainishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.