Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. BALOZI DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii muhimu ya kuchangia mjadala unaoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kukiri kwamba mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira. Pamoja na kuwa Mjumbe wa Kamati, hainiondolei haki ya kutoa maoni yangu pale ambapo kuna jambo naliamini, nalielewa vizuri na kuna jambo ambalo nilishawahi kulisimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja kwamba asilimia 10 kwenye mafuta ya michikichi, ile ambayo wanaita crude palm oil kutoka nje iondolewe. Kama unavyokumbuka jambo hili tulishalifanyia kazi kwa muda mrefu, tunalielewa, kwamba ukitaka kuendeleza viwanda vidogo vidogo vinavyosindika mafuta, kwa mfano vya alizeti na vinginevyo lazima udhibiti haya mafuta yanayotoka nje yanayoitwa crude wakati si crude. Nisingependa kuingia kwenye mjadala huo, Wizara ya fedha wanaelewa na walishafanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwa maoni yangu nafikiri asilimia 10 iendelee kuwepo ili kuweza kusaidia viwanda vidogo vidogo vinavyosindika alizeti na vinginevyo. Nilisimamia hili nikiwa Naibu wako, unakumbuka, jambo hili nililisimamia nikiwa Waziri, nilisimamia pia nikiwa Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri la Afrika Mashariki na naendelea kuamini hivyo nikiwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa vyovyote vile sitakuwa sehemu ya maoni tofauti na hayo ingawa huwezi ukazuia watu wengine kutoa maoni yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niseme suala la kongano la ngozi kule Zuzu…

(Hapa kulitokea hitilafu ya umeme)

MWENYEKITI: Hebu subiri kidogo Mheshimiwa Balozi. Jamani kuna shoti huko juu. Wataalam! Imeungua pale juu. Imeungua tu, hakuna kitu cha kuhatarisha hapo. Tuendelee.

MHE. BALOZI. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kwenye hilo. Kama nilivyosema, nadhani licha ya hiyo changamoto, hoja yangu ibaki pale pale na Hansard wachukue kama nilivyosema kwa sababu siku zijazo watu watasoma hiyo Hansard na naomba msimamo wangu ubaki vile vile kwa sababu ndivyo ninavyoamini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu ukienda mbele ya Kamati ukaeleza changamoto zako tutazipokea changamoto hizo, lakini kupokea changamoto zako si kwamba tumepokea ziwe zetu, changamoto zako zitaendelea kuwa changamoto zako hadi pale tutakapoona uamuzi wa maana unaotakiwa kufanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Zuzu, kongano la ngozi la Zuzu ni jambo jema, limeelezwa vizuri na Wizara inafanya kazi nzuri, Wizara yetu ya Biashara na Viwanda na kwenye taarifa yetu tumeshauri ni jambo jema. Hata hivyo napenda nishauri, kama wenzetu wa Ethiopia walivyofanya; Ethiopia walivyofanya ili kusaidia Sekta ya Ngozi, wao walitoa temporary Government guarantee, ni temporary. Maana changamoto kubwa hata pale Zuzu tukiwatengea eneo tukasema sasa wanaotaka kuwekeza kwenye ngozi waje wawekeze hatimaye hawa wawekezaji wadogo wadogo tatizo kubwa ni mtaji. Mtaji wa kununua mitambo na mashine na mengineyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Ethiopia walivyofanya wao wana ngozi kama tulivyo na ngozi sisi huku, wanatoa temporary guarantee; kwa maana ya kwamba kama wewe ni mfanyabiashara wa ngozi unataka kuwekeza kwenye viwanda vidogo vinavyozalisha bidhaa za ngozi basi Serikali inaku-guarantee unapata hizo mashine, unajenga jengo zuri, unaweka mitambo yako, ukimaliza kuweka hivyo basi ile guarantee ya Serikali inaondolewa kwa sababu unakuwa sasa unaweza kusimama kwa miguu yako sasa Seriakli inasema tembea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ethiopia wamefanya hivyo na sisi kuna sababu ya kujifunza kutoka Ethiopia, tukifanya hivyo, nina uhakika hii Zuzu, tunasema kongano la ngozi la Zuzu litakuwa la manufaa lakini tusipofanya hivyo tutakuwa na kongano la ngozi la Zuzu na litaendelea kuwa hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nihamie kidogo kwenye Wizara ya Mazingira. Tulienda kule Kihansi, kule kuna Maprofesa wazuri kutoka SUA. Walitufundisha mambo mengi, wanafanya kazi nzuri kuhusu masuala ya mazingira, ni wataalam wa kuhakikisha vyura wa Kihansi wanaendelea kuwepo. Hata hivyo mtaalam kutoka Wizara ya Mazingira moja alilotuambia kwamba wale vyura wa Kihansi wanapoendelea kuwepo; hoja sio vyura kuwepo, hoja ni kwamba wanapokuwepo wanasema mazingira mnayatunza vizuri. Wakipotea maana yake wanakwambia sasa mmeanza kuharibu mazingira. Kwa hiyo tusije tukaangalia vyura wa Kihansi kama vyura bali tuangalie wale vyura kama kielelezo kinachotueleza tunafanya kazi gani kutunza mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka Profesa mmoja pale alituambia akisema ukiwa msafi sana unaishia kuugua sana. Sasa sitaki kuingia huko lakini na hilo somo tumejifunza pia kwamba ukiwa msafi sana basi wewe unaugua sana kuliko wasiokuwa wasafi. Kwa hiyo alitoa theory yake pale, wale maprofesa ni wazuri kwa theory lakini alituzindua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa tuliyoiona pale wale watalam Maprofesa kutoka SUA wanatumia fedha za wafadhili na fedha za wafadhili zinafikia mwisho wakati wowote. Sasa inabidi tuangalie tunasaidiaje tafiti kama hizo ziweze kuendelea. Kama fedha ya wafadhili zikimalizika na zile tafiti zikafungwa basi tutakuwa hatuyatendei haki mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli Wizara ya Mazingira inabidi tuiangalie katika siku zijazo kuhakikisha tunaitengea fedha za kutosha kwa sababu mazingira yanapoleta changamoto kila mtu analalamika. Sasa tusiwe wazuri wa kulalamika tu bila kuchukua hatua; na hatua ya kwanza ni kuhakikisha tunatenga fedha za kutosha ili tuweze kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni hii dhana ya Tanzania ya viwanda. Nimesoma na sote tumesoma hapa, ule mpango wa miaka mitano na zile taarifa mbalimbali kutoka Wizara ya Biashara na Viwanda. Tunaposema Tanzania ya Viwanda hatumaanishi na sidhani kama kuna mtu alishafikiria kumaanisha hivyo; hatumaanishi kwamba sasa Serikali itaanza kujenga viwanda, hapana! Tunaposema Tanzania ya viwanda ni kwamba tungependa kuweka mazingira mazuri ya wawekezaji katika viwanda, watu waje wawekeze katika viwanda, Watanzania wawekeze katika viwanda, hatumaanishi sasa kwamba Serikali itaanza kujenga viwanda.