Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na mimi kunipa nafasi kuchangia katika Taarifa za Kamati zetu zote mbili hizi. Kwanza nachukua nafasi hii kuzipongeza Kamati zote mbili kwa taarifa ambazo zinaakisi hali halisi iliyopo nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nijielekeze moja kwa moja kwenye masuala ya mbaazi pamoja na mahindi, kwa sababu sisi watu wa vijijini na ukizingatia nchi hii, watu zaidi ya asilimia 70 wanategemea kilimo, siku zote lazima tuwasemee wakulima ambao ndio tumekuja kuwawakilisha hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mbaazi limetikisa sana na limeathiri sana wakulima wetu Tanzania kwa ujumla. Tatizo kubwa kuna lugha inazungumzwa kwamba Serikali ilihamasisha sana. Mbaazi hatujawahi kuhamasishwa, tulikuwa tunalima siku zote kutokana na kuvutiwa na bei zilizopo sokoni, lakini kilichotokea mwaka 2017 tu alipokuja Waziri Mkuu wa India kuja kusema atanunua yeye mbaazi zote za Tanzania, ndiyo pale labda watu wengine tunachanganya kusema kwamba Serikali ilihamasisha tununue mbaazi hizi na leo hakuna mnunuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichotokea na kwa mbahati mbaya sana, kabla hatujafikia mwisho wa majadiliano na kusaini mikataba, baadaye India ikatokea kwamba wamezalisha mbaazi zaidi kuliko mahitaji yao. Kwa hiyo, wakawa hawahitaji tena kuingia mkataba na Tanzania wala na nchi nyingine kwa sababu walichozalisha wenyewe ni ambacho kilikuwa kinawatosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe ushauri tu kwa Serikali kwamba ni vizuri tukafanya utafiti mkubwa na mahitaji ya soko husika kabla ya kubeba hiyo kauli kuipeleka kwa wananchi. Wanaweza kuichukua na kuongeza uzalishaji wakati hitaji hilo kwa wakati huo hakuna. Ni vizuri tukawekeza zaidi kwenye research and development, kufanya utafiti kwa maana ya masoko, nini kinahitajika kwa wakati gani, hata ambacho tukizalisha tunakuwa na uhakika muda gani kinahitajika na wapi tunakipeleka na kwa bei gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa mfano wa pili, sasa hivi kuna taarifa nyingi tunaletewa kwamba sasa hivi China inahitaji sana mihogo. Kama viongozi tunaweza kuichukua kauli hiyo tunapeleka kwa wananchi wetu, tukawaambia kwamba mihogo inahitajika, lakini mpaka sasa hivi nina uhakika kwamba hata mikataba haijafanyika na hatujui ni bei gani? Kwa hiyo, tusije kuchukua kosa lile lile tulilofanya kwenye mbaazi kwenda kuwahamasisha watu wakaanza kulima kabla ya kuingia mikataba rasmi na kujua bei yake.

Matokeo yake wakulima watakuja kuilaumu Serikali pasipokuwa na sababu za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kuhusu suala la mahindi, ni vizuri Serikali mkaliweka vizuri suala hili kwa sababu wananchi wengi wameaminishwa kwamba Serikali ndiye mnunuzi mkubwa wa mahindi kupitia NFRA, kitu ambacho siyo sahihi kabisa, kwa sababu labda sisi wenyewe Wabunge tunasahau. NFRA tumepitisha wenyewe hapa bajeti ni shilingi bilioni 100 tu. Shilingi bilioni 100 unanunua mahindi hata tani 100,000 hayazidi. Sasa kuwaaminisha watu kwamba Serikali itakuja kununua mahindi wakati pesa yenyewe tuliyotenga ni chache, storage capacity ni ndogo kwenye uzalishaji wa tani zaidi ya 4,000,000 za mahindi Tanzania ni just a peanut. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwanza NFRA kama inavyofahamika yenyewe National Food Reserve Agency. Huyu ni wakala tu wa kuhifadhi chakula cha dharura cha msaada, kwa hiyo, sio mnunuzi wa mahindi yetu Tanzania. Katika hili naomba kuishauri Serikali, ni wakati muafaka sasa wa kuifufua na kuwekeza zaidi katika Shirika la Hifadhi la Chakula (National Milling Corporation) ili lichukue nafasi yake kama zamani ndiyo iwe kampuni mbadala ya kununua mahindi yetu na kuyahifadhi na kufanya biashara kwa niaba ya umma. Tuna uhakika tunatengeneza soko la mazao yetu ya nafaka badala ya kutegemea NFRA ambayo kazi yake ilikuwa ni kununua chakula cha hifadhi tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba sana Serikali, ni vizuri tukawatafuta wadau au Serikali yenyewe kulifufua shirika letu la usagishaji ili lifanye kazi yake kama ilivyokusudiwa kwa mujibu wa sheria na ndiyo itakuwa mkombozi wa mazao yetu ya kilimo. Kama mnavyojua, Serikali au Watanzania wengi tumejiajiri kwenye kilimo, kuwaacha nyuma wakulima ni kuliacha Taifa na watu wengi zaidi maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu labda ni uwekezaji katika mabwawa. Mimi natoka Morogoro na kama mnavyojua sasa hivi mafuriko yako mengi sana, Kilosa, Morogoro Vijijini na sehemu nyingi tu ambapo yanatuathiri na kuturudisha nyuma kiuchumi. Sasa badala ya kutumia haya kama ni majanga, Serikali tuyageuze kama ni fursa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, badala ya kuyaachia maji haya yaende baharini, ni vizuri sasa tukaanza kuwekeza na kuyavuna maji haya ya mvua kuanzia Manyara, Dodoma, Morogoro yote, kwa sababu maji haya yanayotuathiri Morogoro yanaanzia Manyara, yanapita Dodoma yanakuja huku, kote huko, tukijenga mabwawa halafu tukayatumia kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji tutakuwa tumepiga ndege wawili kwa jiwe moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tumeokoa maafa yanayosababishwa na mafariko, lakini pia tumetengeneza uchumi, maji haya tunaweza kuyatumia kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Tukiwekeza hivyo tutakuwa tumewaondoa wananchi wetu kwenye lindi la umasikini na kuondoka katika kilimo cha kujikimu cha kutegemea kilimo cha mvua. Sasa hivi tutakuwa na maji ya uhakika na hawa wananchi wanaweza kukopesheka hata na taasisi za fedha kwa sababu watakuwa na uhakika wa kuvuna, kwa sababu maji yatakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, nizungumze Bwawa la Kidunda. Naipongeza sana Serikali kwa juhudi na mikakati…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)