Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa niipongeze Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa kuwasilisha vyema. Pia niishauri Serikali ichukuwe taarifa yote ya Kamati na kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wimbi kubwa sana la migogoro ya ardhi hapa nchini; na migogoro hii itaendelea kama tu Serikali haijachukua hatua za haraka juu ya suala zima la kupima ardhi katika maeneo yote ambayo ni mipaka ya ardhi ya wakulima na wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hifadhi na wafugaji na watu binafsi wenye mashamba au viwanja kuvamia maeneo ya watu hasa wale ambao hawana uwezo. Kwa hiyo niishauri Serikali yangu Tukufu kuharakisha mchakato huu hasa kwa kupeleka fedha za kutosha na kwa wakati ili maeneo yote yapimwe na kuanishwa ili makundi yote hayo yatambue mipaka yao hasa kwa kuweka mawe ya mipaka (beacon).

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuajiri watumishi wa kutosha kwani kwa sasa Wizara ina watumishi wachache sana ambao hawakidhi mahitaji ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kupima miji na majiji kwa vile vifaa vya kisasa ambavyo vimetumia Satellite, hivi vifaa visambazwe kwa kasi vifike mpaka kwenye wilaya kuliko ilivyo sasa ambapo vipo tu kwenye baadhi ya majiji kwani hii itafanya wananchi wapate hati kwa haraka kuliko ilivyo sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Misitu. Maeneo mengi hapa nchini hayana miti ya kutosha na kuna maeneo mengine hayajapandwa miti kabisa. Naomba niishauri Serikali iwape pesa za kutosha hasa Wakala wa Mbegu ambao ni TTSA,TAFORI, DANIDA pamoja na hawa Wakala wa Misitu Tanzania TSF na kuwasimamia na kuhakikisha wanazalisha miche ya kutosha na kupanda maeneo yote yenye ukame pamoja na yale ambayo misitu yake imeungua kama vile Misitu ya Lushoto takribani maeneo mengi ya Misitu ya Lushoto imeungua na kubaki vichaka tu. Kwa hiyo, niiombe Serikali maeneo hayo yapandwe miti haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na kuwashirikisha watu binafsi wenye bustani za miti pia kuwapa support ili nao wawe wanachangia katika suala zima la kupanda miti. Pamoja na kusimamiwa Sheria Ndogo hasa hizi zinazotoka Halmashauri na kuwaelekeza mpaka Wenyeviti wa Vitongoji wasimamie zoezi hili. Serikali ikifanya hivyo, naamini nchi nzima hii itakuwa ya kijani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mapango ya Amboni. Tulitembelea Mapango ya Amboni tumekuta Serikali inapoteza pesa nyingi sana kwani mapango yale ni ya asili ambayo huwezi kuyapata popote pale hapa duniani lakini mapango yale yanaendeshwa kikawaida sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali iyaboreshe maeneo yale ya Ambaoni kwani inapoteza fedha nyingi sana, patangazwe na kuwe na miundombinu ya barabara, waajiriwe watumishi wenye taaluma . Pia tutangaze mbuga zetu ndani na nje ya nchi kwani hii ndiyo secta inayoingiza pesa nyingi za kigeni. Pia nashauri kuundwe Tume hapa Bungeni itakayochunguza migogoro ya wafugaji na Wizara ya Maliasili na Utalii. Kwani hali si nzuri, kuna malalamiko ya wafugaji pamoja na wadau, yaani watu wanaomiliki vitalu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naunga mkono hoja ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii.