Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. William Vangimembe Lukuvi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ismani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii na mimi nitoe mchango wangu kwenye hoja ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitumie fursa hii kuunga mkono hoja yetu ya Ardhi, Maliasili na Utalii kabla sijaenda mbali. Lakini pili, kumpongeze Makamu Mwenyekiti ambaye kwa sasa anakaimu Mwenyekiti dada yangu Mheshimiwa Kemilembe Julius Lwota na Wajumbe wote wa Kamati hii kwa kuendelea kutushauri na kutuunga mkono katika kutekeleza majukumu yetu tuliyopewa katika Wizara ya Maliasili na Utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, nitapenda kuanza kuchangia kwanza kwa kulitambulisha Bunge lako tukufu kwamba sekta ya maliasili na utalii ni katika sekta nyeti sana katika Taifa letu. Na unyeti wake unaanza pale ambapo Tanzania inatambulika kimataifa katika tafiti iliyofanyika mwaka 2012 kama nchi ya nne kati ya nchi 140 duniani zenye vivutio vya asili. Kwa hiyo, nchi yetu ina utajiri vikubwa sana wa vivutio vya utalii. Lakini pili, sekta ya maliasili na utalii inachangia pato la Taifa kwa kiwango cha asilimia 17.6 ya GDP yaani pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia sekta hii inachangia kwa kiasi kikubwa na niseme tu ni sekta namba moja kwa kuingiza fedha za kigeni nchini mwetu. Katika mwaka wa fedha uliopita sekta hii ilichangia jumla ya shilingi bilioni 2.1 za Kimarekani, lakini pia sekta hii ina changamoto nyingi mbalimbali na changamoto zake zinatokana na uasili wenyewe wa sekta hii. Sisi kwenye Wizara ya Maliasili na Utalii tunasimamia rasilimali ambayo inatumika lakini pia inajirudia, kwa maana kwamba wanyamapori wanazaliana; misitu inaweza ikaota ikakua. Kwa hiyo, ni sekta ambayo ina rejuvenate kadri ambavyo tunaendelea kui-manage kwa uendelevu.

Lakini pia sekta yetu inachangia kwa kiasi kikubwa sana kutoa ajira hapa nchini, inachangia takribani asilimia 12 ya ajira zote zinazotolewa katika Taifa letu na kwa msingi huo sekta hii ni nyeti sana na mimi katika hatua hii nikubaliane na Kamati yetu ya Ardhi, Maliasili na Utalii pamoja na Waheshimiwa Wabunge wenzangu wote waliosema kwamba sekta hii kwa hakika inahitaji umakini wa namna ya kipekee katika kuiongoza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipoteuliwa kwenye nafasi hizi nina hakika mamlaka ya uteuzi ilizingatia umuhimu huo kuweka watu wanaoweza kuiongoza sekta hii kwa weledi lakini pia kwa uzalendo na uadilifu wa hali ya juu na ndiyo maana tunatekeleza majukumu yetu bila kumwangusha Mheshimiwa Rais lakini pia bila kuliangusha Taifa letu.

Pamoja na fursa zote zilizopo lakini sekta hii ina changamoto kubwa sana ya maeneo yake kuvamiwa na watu mbalimbali, ina changamoto ya mipaka kutokuwa wazi, kutokueleweka vizuri baina ya wahifadhi na wananchi, ina changamoto kwamba sekta ya utalii imekuwa ikichangia kidogo sana kwenye kuondoa umaskini wa watu wetu japokuwa inaonekana ni sekta nyeti. Lakini pia ina changamoto kwamba sekta hii imejikita katika ukanda mmoja tu wa nchi yetu na kwa kiasi kikubwa kwa zaidi ya asilimia 90. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hivyo sasa changamoto hizi tumeziwekea mikakati mbalimbali ya kuzitatua. Mojawapo ya mikakati tuliyoweka kwenye ya awamu ya tano ni utekelezaji wa mradi mkubwa wa kufanya diversification ya kijiografia kwa maana ya kutambua na kuwekeza nguvu zetu kwenye maeneo mengine zaidi ya kitalii. Lakini pia kufanya diversification ya mazao ya utalii yaani toursim product katika maeneo mengine mbalimbali na katika hili napenda kutambua diversification ya kijiografia ambayo tumeanza kuifanya na tutaifanya kwa mafanikio makubwa ya kuelekea kuifungua circuit ya utalii ya kusini ambapo tunaanza kuelekea kutekeleza mradi mkubwa unajulikana kama RIGRO ambao una dola za Kimarekani milioni 150 zaidi kidogo ya shilingi bilioni 300. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mradi huo tutafanya mambo mengi ikiwemo kujenga uwanja wa ndege wa Nduli na kuufanya uwe wenye kiwango cha kutua ndege kubwa. Lakini pia kujenga barabara ya kutoka Iringa mpaka geti la kuingia Ruaha National Park pale Msembe, lakini pia kujenga viwanja vidogo vidogo vya ndege 15 katika mbuga nne ambazo zinapatikana kwenye circuit ya kusini. Na hapa nazungumzia Udzungwa, Ruaha National Park, nazungumzia Selous Game Reserve lakini pia nazungumzia Mikumi National Park. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo hayo ambayo tunakusudia kuyafanya kwenye mradi wa RIGRO tunakusudia kuwekeza kwenye uhifadhi wa bonde la Usangu ambalo kwa kiasi kikubwa limeingiliwa na shughuli mbalimbali za kibinadamu na hivyo kusababisha maji kwenye Mto wa Ruaha Mkuu kupungua kwa siku zaidi ya 60 katika kipindi cha miezi 12 ya mwaka hali ambayo inaweza kuhatarisha bionuai inayopatika kwenye hifadhi ya Ruaha na maeneo mengine yanayolindwa kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii ni diversification ya kijiografia kwamba kanda ya circuit ya kaskazini imeelemewa sana, lakini pia inafanya vizuri sana sasa tunaifungua circuit ya kusini ili na kwenyewe kuweze kuwa na hadhi ya kiutalii kama ambavyo circuit ya Kaskazini ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu pia unakuja na kufanya maboresho kwenye kituo cha treni cha Matambwe kilichoko pembezoni mwa Pori la Akiba la Selous lakini pia kujenga air strips zenye hard surface nne kwenye maeneo yote hayo niliyoyataja na mambo mengine mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kufanya diversification ya kijiografia, tumejikita pia kufanya diversification kwenye mazao ya utalii yaani tourist product ambapo hatuangalii utalii wa wanyama pori peke yake tunaanza kufikiria kutanua wigo wa vivutio kwa kuwekeza kwenye kufanya maboresho ya utalii wa fukwe, utalii wa mikutano lakini pia…

KUHUSU UTARATIBU . . .

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante, ni Mjumbe wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii na hii ni hoja ya Kamati kama Mbunge ninachangia hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msingi huo tunafanya jitihada nyingi mbalimbali ikiwepo jitihada kuongeza mazao ya utalii kama nilivyosema na hapa tunazungumzia mbali na hizo talii za fukwe, utalii wa kuvutia mikutano na matukio mbalimbali ya michezo ya kimataifa tunawekeza nguvu zetu kwenye kuandaa mwezi maalum wa urithi wa Mtanzania, ambapo tumekusudia mwezi wa tisa kuandaa…(Makofi)

(Hapa kengele ililia na kuashiri kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

T A A R I F A . . .

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, huyo ndio Mnyamwezi Kingwangalla huyo. (Makofi)

Naomba niipongeze sana Kamati yangu chini ya Makamu Mwenyekiti na Waheshimiwa Wajumbe wote wa Kamati hii kwa michango, lakini pia kwa maelekezo yao ya kila mara ambayo yamesaidia sana katika utendaji wa Wizara yangu. Lakini nawashukuru pia Wabunge wengine wote wa Bunge hili kwa ushirikiano wao mkubwa ambao unatusaidia kama Wizara ya Ardhi katika kutatua na kufanya kazi mbalimbali za kusimamia sekta ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nawapongeza vilevile Waheshimiwa Mawaziri wenzangu wa sekta zilizotangulia ambazo ni watumiaji wa ardhi wote waliotanguliwa wa Mifugo, wa Kilimo, wa Maliasili wote ni watumiaji wa ardhi nawapongeza sana kwa mikakati yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikua tu niwakumbushe kwamba tunajua kwamba tuna migogoro mingi sana na kwa upande wa ardhi tuna migogoro ndani ya vijiji na ndani ya miji na tunajua kila Mbunge hapa alishawahi kuorodhesha migogoro yake kutoka kwenye Jimbo lake na hata tungeorodhesha yote tusingeweza tukaimaliza hata tungepata kipindi cha Bunge la mwaka mzima. Nataka muamini tu kwamba migogoro yote mliyoorodhesha kuanzia kwenye Kamati Teule ya Sendeka na ndiyo maana hata mdogo wangu Mheshimiwa Nape hapa mimi naona hakuna sababu ya kuunda Kamati Teule nyingine kwa sababu ile Kamati ya mwisho ya mwaka 2015 ndiyo tunafanyia kazi kama Serikali hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, orodha yenu ya migogoro ndio tunafanyia kazi ndiyo iliyosababisha tuunde Kamati ya Mawaziri watano, nataka kuwaambia tunaendelea vizuri isipokuwa kama mnavyojua baadhi ya Mawaziri wameingia karibuni tumepeana muda ili kila mtu akaangalie sekta yake, halafu tutakutana tena nafikiri wakati wa Bunge la Bajeti kila Wizara itakuwa na maeneo mapya ya kusemea kuliko ilivyo sasa. Kwa hiyo, Kamati yetu inaendelea vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwakumbushe tu kwa sheria ya mipango miji na za vijiji za ardhi zote za mwaka 1999 masuala yote yanayohusu ardhi yanasimamiwa na Halmashauri zetu za Wilaya. Halmashauri za Wilaya ndio zinazohusika na mipango mijini lakini ndizo zinazohusika na mipango ya matumizi bora ya ardhi katika vijiji.

Kwa hiyo, kila tunachosema tujue mamlaka ya mwisho ya kuandaa mipango ya matumizi bora mjini au mipango ya matumizi bora vijijini ili kuepusha mapigano ya wakulima na wafugaji na wavamizi wengine ni sisi Halmashauri ndio tumepewa dhamana hiyo kwa mujibu wa sheria zote hakuna mtu mwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ningependa kila mara tuwe tunashiriki vizuri katika kusimamia ardhi yetu kwa kushiriki katika upangaji mijini lakini vijijini. Nawapongeza sana Halmashauri ambazo hivi sasa mijini wameshaandaa master plan ziko Halmashauri 23 za miji, lakini ziko Halmashauri nyingine 24 na miji midogo ambayo wameandaa mipango ya kati na ziko Wilaya karibu asilimia 20 ambao wameshaandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi.

Kwa hiyo, nawahimiza tu Waheshimiwa Wabunge angalau kila Wilaya kwenye bajeti ingeweka angalau kila mwaka kufanya matumizi bora ya ardhi vijiji vitano vile vyenye migogoro mikubwa ambavyo vinashirikisha jamii nyingi pengine tungepiga hatua. Kwa hiyo, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge tujue kwamba jukumu la mipango ya matumizi bora ya ardhi ni la kwetu sisi. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Lukuvi dakika moja samahani kidogo. Kwa mamlaka niliyokuwa nayo naongeza nusu saa mpaka saa mbili na robo, endelea Mheshimiwa Lukuvi.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Wizara kwa kutambua hilo na ninyi wote Waheshimiwa Wabunge mnajua sehemu kubwa ya nchi hii haijapangwa, mijini na vijijini hakujapangwa yaani utambuzi na upangaji wa matumizi mbalimbali mijini na vijijini haujafanyika kwa zaidi ya asilimia 75.

Kwa hiyo, Wizara yangu na Serikali kwa sasa tunaandaa mpango wa kitaifa wa kupanga na kupima kila kipande cha ardhi cha nchi hii. Kwa sababu hiyo tutakuja na mapendekezo kwenye budget speech yetu pengine kuanzisha fund maalum ambayo itasababisha zoezi hili la upangaji wa vijiji na upimaji na mijini liweze kutekelezeka. Kwa hiyo, tunakusudia angalau kila eneo na kila kipande cha ardhi kiweze kupangwa ili ulinzi wa ardhi uwe madhubuti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na zoezi hilo tumeliona linawezekana kwa sababu hivi sasa tuanza katika Wilaya ya Kilombero, Malinyi na Mahenge. Tumeanza kupanga kila kipande cha ardhi na katika mwaka ujao tutakuwa tunakamilisha mpango wa Wilaya hizo tatu tutakuwa tuna uwezo wa kutoa hati za Kimila zaidi ya laki nne katika Wilaya hizo tatu. Kwa hiyo, tunafikiri kwamba kila mwananchi akiwa na hati katika eneo analomiliki ikiwa kijijini hati ya kimila na mjini title deed itamwezesha kutumia rasilimali ardhi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na zoezi hilo kwa sababu hii nchi hii haijapangwa kwa muda mrefu mijini hata vijiji kwa mijini tumekuja na programu ya urasimishaji wananchi wote ambao walijikuta wamejenga katika maeneo ambayo hayakupangwa na kupimwa kwa matatizo mbalimbali pengine kwa Serikali kuchelewa kupanga maeneo hayo. Tumeanzisha programu ya urasimishaji katika maeneo hayo ili wananchi hao waweze kupata huduma za msingi katika maeneo hayo kama vile barabara maeneo ya upitishaji miundombinu ya umeme na maji, lakini pia tuwawezeshe kuwa title deed waweze kumiliki ardhi kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wajumbe mjue jambo hili linahimizwa na Serikali kama una squatter, kama una wananchi katika Jimbo lako wanaishi katika makazi holela, jitahidi sana kuhakikisha mnashirikisha wananchi katika mitaa ile wanafanya urasimishaji ili watoke kwenye makazi holela wakae kwenye makazi yaliyo rasmi. Tunafanya zoezi hilo ni rasmi, najua wote mnaokaa mjini mna maeneo ambayo yanamakazi holela. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni fursa imetolewa na Serikali ya Awamu ya Tano kurasimishwa maeneo hayo na mpaka sasa mikoa ambayo inaongoza kwa urasimishaji ni Mkoa wa Mwanza ambao kwa sasa Wilaya mbili tu za Ilemela na Nyamagana wanakaribia kutoa hati 30,000 kuwawezesha wao…

T A A R I F A . . .

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kila Wizara inasimamiwa na sheria zake. Sheria yangu inaniruhusu kurasimisha makazi holela, lakini halitakuwa jambo la kudumu, ndiyo maana tunahimiza master plan na tunakuja na mpango wa kupanga na kupima kipande cha ardhi. Tukiweza kupanga na kupima kila kipande cha ardhi, kwa vyovyote vile urasimishaji utakoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka niwapongeze sana viongozi na wananchi wa Wilaya za Ilemela na Nyamagana peke yao wamewezesha wananchi wao ambao walikuwa wamejenga majengo ya fahari na hayana hati, leo wanamiliki wakiwa na hati katika makazi holela. (Makofi)

Pia Mkoa wa pili ni Dar es Salaam, Dar es Salaam kuna maeneo mazuri wanafanya vizuri Kimara, Makongo kule kwa maprofesa wanafanya kazi nzuri wamechanga wenyewe. Lakini na mikoa mingi wanaendelea kufanya zoezi hilo, kwa hiyo, nawapongeze sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na mapendekezo ya Kamati kwamba kuanzia sasa hatutatumia makampuni ya nje kufanya master plan. Tumefanya master plan kwa kutumia Kampuni ya Singapore kama walivyosema watu wa Kamati, Wajumbe wangu wa Kamati kwa gharama kubwa. Tumefanya Mwanza na Arusha ni kweli, lakini nimesema nimekubaliana na mapendekezo ya Kamati yangu ya Ardhi kuanzia sasa haitawezekana kabisa kuajiri makampuni ya nje kwa ajili ya kufanya master plan, kwa sababu vyuo vyetu vya ndani vimetoa wataalam wengi, na hizi master plan…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)