Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Mwanne Ismail Mchemba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. MWANNE J. MCHEMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hotuba zote mbili za kamati tatu, lakini nijikite kwanza kwenye Kamati yangu ya Utawala na Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa iliyotolewa na Kamati yangu ni sahihi na ninaipongeza na ninaunga mkono.

Kazi yangu leo sasa hivi hapa ni kuiboresha tu au kukazia yale ambayo yamo kwenye taarifa yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende haraka haraka, hivi karibuni Kamati yangu ilikwenda ziara Mkoa wa Iringa, lakini niiombe Serikali, miradi mingi ambayo ilianzishwa na Serikali kwa miaka iliyopita ikamilishwe kwa haraka iwezekanavyo. Kwa mfano tulipokwenda Iringa kwenye Wilaya ya Kilolo tulikuta kuna mradi mkubwa sana wa Serikali ambao pesa zake nyingi zimetumika, lakini kwa bahati mbaya pesa iliyobaki ni kidogo, lakini Serikali haijatoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nizungumzie tu hivi, Hospitali ile ya Wilaya Mheshimiwa Jafo anaijua jinsi ilivyoanza, ni hospitali ya mfano, ina maghorofa manne, inajengwa kwa shilingi bilioni 4.4; ndiyo gharama ya ujenzi na inasimamiwa na TBA, lakini ukiangalia jinsi inavyosuasua inasikitisha, kwa sababu sisi kama Kamati tulisema hivi, ile hopsitali iwe ya mfano kwa nchi nzima. Hii ni kwa sababu kuna makadirio mengine ambayo ni ya hospitali hizo za Wilaya zinatumia zaidi ya shilingi bilioni 10 na 15, lakini hawa niwapongeze sana Halmashauri ya Kilolo kwa kazi nzuri waliyoifanya. Kamati zote zimeenda, watu wa Hazina wameenda, Hazina Makao Makuu wameenda, Hazina Mkoa wameenda, wamethibitisha kwamba yale majengo yako vizuri na gharama yake inaridhisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niiombe Serikali na najua Serikali ina azma nzuri na ina matarajio mazuri ya kuhakikisha wananchi hawapati tabu kwenye huduma ya afya, lakini niombe Serikali ihakikishe inapeleka pesa haraka sana za wakandarasi, imeathiri. Eneo lile hospitali ile kama ingekamilika ingehudumia wananchi wengi sana ukizingatia na jiografia ya Iringa ilivyo kwa kweli, wananchi wanateseka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ambalo tulikuwa tumeomba kwenye Kamati yetu ni kwamba Wizara ya TAMISEMI itusaidie kutoa waraka wa ujenzi ambao utazingatia mazingira magumu au utazingatia walemavu/ mahitaji maalum. Kwa sababu kuna maeneo mengi wanajenga majengo ya Serikali lakini kwa bahati mbaya hawazingatii mahitaji maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ambalo mimi nimeliona pia ni kwamba, wanapojenga nyumba, madarasa wanapojenga hawazingatii kutoa waraka wa sera ambayo itasaidia ujenzi wa matundu ya vyoo. Sasa hivi wanaongeza kujenga madarasa, lakini matundu ya vyoo hayapo, ujenzi wa nyumba za walimu haupo, ujenzi wa nyumba za madaktari haupo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naomba sana, namuomba Mheshimiwa Jafo, ni msikivu na Serikali yangu ya Awamu ya Tano ni sikivu, itusaidie kwa hilo ili angalao tuweze kwenda sambamba na mahitaji ya Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nilikuwa nataka nimuombe Mheshimiwa Mkuchika Waziri wangu, samahani nakutaja jina lakini Waziri wa Utumishi, nafasi ambazo ziko wazi baada ya uhakiki wa vyeti fake kwa kweli Serikali ingeangalia upya, ili iangalie namna ya kujaza hizo nafasi upande wa madaktari, upande wa walimu, hakuna kinachofanyika kwa sasa hali ni ngumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningeiomba Serikali iangalie jinsi ya kuweza kuhakikisha kwamba, EGA badala ya kuwa wakala awe na mamlaka kamili ili kuhakiki takwimu za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nataka kuomba pia kuhusu TARURA, kwa sababu tunaenda haraka haraka. TARURA sasa hivi inafanya kazi nzuri, lakini inafanya kazi kwa kusuasua.

Nilikuwa naishauri, kama walivyosema Kamati yangu, kwamba sasa ipewe 50 kwa 50, TANROADS wapate 50 na TARURA wapate 50 kwa sababu, barabara za vijijini zimeharibika sana na Kamati yangu inakwenda mpaka vijijini barabara hazifai, madaraja hayafai, masika hii hakuna njia…

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, hotuba zote.