Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. JASSON S. RWEIKIZA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru tena kwa fursa hii ya kuhitimisha taarifa yangu, lakini pia niwashukuru sana Wajumbe wa Kamati yangu ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa kazi kubwa sana walioifanya tulioifanya pamoja ambayo imetufikisha hatua hii ya sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kutoa shukrani kwa Wabunge wote waliochangia na waliosikiliza taarifa hii tangu asubuhi kwa umakini mkubwa. Wabunge waliochangia taarifa yangu wako jumla 19. Wa kuandika wako Mheshimiwa Susan Lyimo, Mheshimiwa Zaynabu Vullu, Mheshimiwa Ester Mahawe, Mheshimiwa Albert Obama, Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mheshimiwa Omary Mgumba, Mheshimiwa Mary Deo Muro, Mheshimiwa Sebastian Kapufi, Mheshimiwa Ester Matiko, Mheshimiwa Angelina Malembeka, Mheshimiwa Rhoda Kunchela na Mheshimiwa Waitara Mwita na Wabunge saba wamechangia kwa kusema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri na Mheshimiwa Naibu Waziri George Kakunda, Mheshimiwa Waziri Selemani Jafo na Mheshimiwa Waziri George Mkuchika kwa majibu waliyoyatoa wakijibu hoja za Wabunge ambao kwa kweli wamejibu kwa ufasaha na kwa ukamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongezee kwenye mambo kadhaa machache ambayo yametajwa katika michango ya Waheshimiwa Wabunge niliowataja, la kwanza ni MKURABITA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, MKURABITA ni mpango mzuri sana ambao unasaidia wananchi wanyonge kurasimisha biashara zao na mali zao, ardhi, lakini MKURABITA ina hela kidogo sana, ukiangalia kwenye bajeti inapata mgao kidogo sana. Kwa hiyo, kwa kweli nipende kusisitiza kwamba ni vizuri Serikali ikaangalia kuongeza bajeti kwenye MKURABITA kusudi kazi ya MKURABITA iweze kuonekana kwa manufaa yanayokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na la pili, kwenye MKURABITA kusisitiza kwamba hati miliki za kimila zikubaliwe na mabenki. Kuna baadhi ya mabenki ambazo zinazikataa hati miliki hizi kwa sababu ile ardhi ambayo juu yake kuna hiyo hati miliki ya kimila haiuziki. Sasa niseme kwamba ni vizuri Serikali ingefanya utaratibu ili ardhi hiyo ikaweza kuuzika kama mkopaji ata-default, na ikiwa hivyo benki zitakubali kutoa mikopo kwa hati miliki hizi.Haki miliki hizi ziwe na manufaa kwa wananchi wanyonge waweze kukopa na kujiendeleza kiuchumi lakini pia kuondoa migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni TASAF. TASAF nayo imefanya kazi nzuri sana kwa miaka iliyokuwepo; TASAF ya kwanza, TASAF ya pili, leo ya tatu. TASAF ya kwanza na ya pili zilijenga barabara nyingi, zilijenga madaraja kadhaa, zilijenga shule, madarasa na kadhalika. TASAF hii ya sasa inaweka mkazo kwenye kaya maskini sana, na kwa msaada wa TASAF kaya nyingi zimeweza kupata chakula kizuri, milo miwili kwa siku, milo mitatu kwa siku. Watoto wameweza kwenda kliniki na kwenda shule kwa ufasaha. Kwa hiyo, niiombe Serikali iongeze mchango wake kwenye TASAF. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu tulionao imetoa shilingi milioni 750 kati ya lengo la bilioni tatu; ni kidogo lakini si haba. Ni robo ya lengo la Serikali kutoa lakini si haba sana. Kwa hiyo, waongeze jitihada ya kutoa fedha kusudi na wale wafadhili waweze kuongeza fedha TASAF iweze kuendelea kutuneemesha Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo limeongelewa na Wabunge wengi kwenye michango yao ni asilimia 10 kutoka Halmashauri kwenda kwenye wanawake na vijana. Jambo hili limekuwa gumu kwa sababu Halmashauri zinafanya kwa hiari, hazilazimiki kutoa asilimia 10, hakuna sheria inayowalazimisha kwamba watoe asilimia 10, tano kwa vijana na tano kwa wanawake. Tunasisitiza kwamba sheria ingetungwa ili Halmashauri hizi zilazimike kutoa michango hii kwenda kwa wanawake na vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni TARURA. TARURA ni mamlaka au wakala changa sana ina miezi michache imeanzishwa lakini imefanya kazi nzuri sana. Kazi nzuri imeonekana, barabara nyingi za vijijini na mijini zimeanza kujengwa. Hata hivyo inapewa mgao kidogo sana kutoka Road Fund Board, asilimia 30. Kwa kweli hiki ni kiasi kidogo mno. Ina Halmashauri 185 barabara zote za Halmashauri za vijijini na za mijini. Kwa hiyo, ni kwakweli ni jambo jema kama walivyosema wabunge kiasi hiki kiongezwe ili kusudi TARURA iweze kufanya kazi ambayo inaonesha ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watumishi hewa waliopunguzwa kutokana na vyeti hewa na vyeti Ifake wameathiri sana utendaji kazi Serikalini hasa kwenye afya na madereva. Kama walivyosema Wabunge madereva walikuwa na uzoefu mkubwa, lakini wana vyeti fake, basi nitoe wito kwamba wengine waajiriwe, waajiriwe wa kutosha kusudi upungufu huu uliojitokeza hata kwenye afya uweze kuondolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya afya amesema Mheshimiwa Kahigi na Waheshimiwa wengine, kuna Wilaya hazina Hospitali za Wilaya. Halmashauri 64 hazina hospitali za wilaya. Hizi halmashauri 64 Mkoa wa Katavi wote hauna hospitali hata moja ya Wilaya. Mkoa wa Kagera wote, Kagera ina Wilaya nane hauna hata wilaya moja yenye hospitali ya Wilaya. Kwa kweli ni vizuri sana kama alivyosema Mheshimiwa Jafo tulimsikia, ametoa ahadi kwamba fedha zitatengwa na itajengwa Hospitali ya Wilaya kule Bukoba moja au mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya eimu imezungumziwa sana na Waheshimiwa Wabunge mbalimbali, lakini mimi niongelee jambo moja kwenye sekta ya elimu. Ukosefu wa vyoo kwenye shule za msingi na sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shule nyingi hazina vyoo, hili ni jambo la fedheha kubwa sana. Jana liliongelewa jambo la taulo za wanafunzi wa kike, mimi nasema la vyoo ni kubwa zaidi, kwa sababu la linahusu wasichana na wavulana, wanakwenda wapi? Serikali iweke bidii na jitihada kubwa sana kujenga vyoo. Ni bora nyumba za walimu zikasubiri, shule mpya zisijengwe ili zilizopo zipate vyoo watoto wapate mahali pa kujisitiri, vijengwe vyoo vya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nchi hii imeendelea na kupiga hatua. Barabara nyingi zimejengwa lami, tunajenga barabara za juu pale TAZARA na Ubungo, tunajenga reli ya umeme (standard gauge) lakini hatuna vyoo mashuleni, ni jambo la aibu, fedheha na adha kubwa kwa wanafunzi. Hili lingetiliwa mkazo kusudi liweze kutatuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri Serikali ikitia nguvu akisema Rais kwamba liishe linaisha. Rais amesema madawati likaisha, tatizo la madawati limekwisha. Kwa hiyo, nafikiri hata Mawaziri wanaohusika na sekta hii ya elimu wakazanie suala la vyoo mashuleni na liondolewe matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maji vijijini ni tatizo kubwa sana. Leo asubuhi nimesikia miongozo humu ndani kuhusu maji vijijini. Waheshimiwa Wabunge wamesimama wote wanalalamika kuhusu maji vijijini. Juzi alisema Naibu Waziri wa TAMISEMI kwamba kuna fedha shilingi bilioni 156 kwenye akaunti ya maji vijijini, lakini kitu kinachopungua ni wakala; wakala haujaanza kusudi huduma hii iweze kutolewa kwa vijiji. Nisisitize kwamba ni vizuri kama wakala huu angeanza mara moja kusudi ishughulikie adha ya maji vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo kwa ufupi niombe tena Bunge lako Tukufu liazimie kama taarifa yetu ilivyosema na ninaomba kutoa hoja.