Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi. Kipekee naipongeza sana Kamati yangu ambayo inaitwa Guantanamo kwa kuwa ina vichwa vikali sana. Pia napongeza kwa taarifa nzuri, lakini vilevile Taarifa ya UKIMWI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza zaidi kwenye elimu kwa sababu mimi ni mwalimu, lakini vilevile nitagusia mambo ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna nchi yeyote au jamii yoyote hapa duniani ambayo imeendelea bila kuwekeza kwenye elimu, lakini sekta ya elimu hapa nchini inakumbwa na changamoto nyingi sana. Changamoto ya kwanza hatuwezi kuwa na elimu bora kama walimu hawajapewa mahitaji yao. Kumekuwa na kilio kikubwa sana cha walimu na hapa Bungeni kila siku tumekuwa tukizungumza na hata leo maswali mengi huwa yanaelekezwa kutetea maslahi ya walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyoongea, walimu walioajiriwa Januari hadi leo hawajapata mishahara wala fedha za kujimu. Hawa ni vijana wadogo wanaomaliza vyuo. Tunategemea vijana hao, hasa watoto wa kike waolewe na Wenyeviti wa Mitaa au waolowe na Wenyeviti wa Vitongoji? Kwa hiyo, hayo ni matatizo makubwa. Tunaomba Serikali ituambie, ni kwa nini wanaajiri watu halafu hawawapi mishahara wala posho za kujikimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwa walimu ni kuhusu masuala ya madaraja. Niliuliza swali kwa Waziri Mkuu hapa kwamba watumishi...

T A A R I F A . . .

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli wanaweza, lakini hiyo watakuwa wanaolewa bila ya ridhaa yao kutokana na matatizo hayo ambayo wanayapata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu suala la madajara. Baada ya zoezi la kuhakiki, ndani ya mwaka mzima, baadhi ya watumishi pamoja na walimu hawakulipwa nyongeza hizo. Na sisi tunajua kabisa watumishi ni endelevu, kwa hiyo, hilo zoezi la uhakiki limewaathiri sana watumishi wa umma wakiwemo walimu. Tunaomba pia Serikali ituambie ni kwa nini katika zoezi hilo wamehakikisha kwamba mwaka mzima watu hawa hawajapata maslahi yao au nyongeza zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kwa sababu nimesema kwenye elimu bora, ni walimu, vitabu na mazingira bora ya kufundishia, utakumbuka kwamba wakati wa bajeti ya mwaka 2017 tulizungumza suala la vitabu vibovu, ikapelekea Kamishna wa Elimu pamoja na baadhi ya watumishi kusimamishwa kazi lakini mpaka leo tunavyozungumza na Waziri alisema itaundwa Tume, lakini mpaka leo kama ambavyo imeandikwa kwenye Kamati yetu, bado hatujapata report, lakini kubwa ambalo nataka kuzungumza, mpaka leo wanafunzi hawana vitabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nieleweke kwamba life span ya vitabu ni miaka miwili mpaka mitatu kwa darasa la kwanza mpaka la nne kutokana na matumizi, lakini vitabu vya mwisho vimekuwa published mwaka 2013. Leo ni mwaka wa tano bado hatuna vitabu na tunategemea wanafunzi hawa wafaulu. Wanafaulu vipi kama walimu hawana morale, lakini na vitabu navyo havipo ambavyo ndio sehemu kubwa kabisa ambayo watoto wangeweza kusoma vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana kuwe na Tume kabisa au Kamati ya Bunge ambayo itapita kwenye shule kuona kweli tatizo hili ni kubwa kiasi gani ili Wizara iwajibike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna suala kubwa tulizungumza na limezungumzwa kidogo, suala la re-entry policy. Naomba nirudie, tulizungumza, nikategemea Kamati inapotoa ushauri, maana yake wameona mambo mengi, lakini Serikali ikalipiga chini. Leo limekuja kwa mlango mwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme hivi, Serikali hii ilitoa guidelines kwa jinsi gani wanafunzi hawa wanaweza kurudi shuleni. Hata hivyo lilikuwa diluted ikaonekana kwamba watoto wanaopata ujauzito ni wachache sana. Sasa najiuliza, kama ni wachache sana kwa nini wasirudi shuleni?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mazingira mengi ambayo yanasababisha matatizo hayo. Kuna mazingira magumu sana yanayosababisha matatizo hayo ambapo Serikali nayo inayajua. Mazingira hayo ni pamoja na kubakwa, vilevile tunajua kwamba shule ziko mbali, watoto wanakienda shule wanapita maeneo magumu, wazazi ni masikini, lakini hayo yote hayajazingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ni kwamba tunaomba sasa ni kwa nini kama Kamati imetoa maelekezo yake au ushauri, mtu mmoja tu anaweza kuja akabadilisha the whole thing. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona mgongano mkubwa uliopo, pamoja na kwamba maombi ya re-entry, yaani warudishwe shuleni yamekataliwa, lakini hapo hapo, AG tayari Mahakama ilishatoa hukumu yake mwaka juzi (2016), kwamba ile Sheria ya Ndoa, kifungu namba 13 na 17 hukumu ikawa in favour, lakini AG hapa Bungeni akatuambia kwamba Serikali imekata rufaa na wakati kweli ilikuwa haijakata.

Mheshimiwa Mwenyekiti,Serikali pamoja na kugundua kwamba AG amekata rufaa Septemba, 2017 yaani mwaka mmoja na miezi miwili baada ya hukumu; tulikuwa tunaomba AG atasaidie, hivi ni muda gani au ni time frame gani baada ya hukumu mtu anaweza kukata rufaa? Kwa sababu hii ni mwaka mmoja na miezi miwili, ndiyo AG ameenda kukata rufaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtuambie, kwenye Katiba inaonesha kwamba kazi za AG ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye anaishauri Serikali. Sasa naomba mje mtueleze, hivi kweli AG anatoa ushauri kwamba mtoto wa chini ya miaka 18 anaweza akaolewa at the same time mnasema mtoto asipate ujauzito. Mtoto aliyepata ujauzito, asirudi shuleni! Kwa hiyo, hii contradiction na tutaomba hii contradiction mtusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nataka kuzungumzia ni suala la mabweni yanayojulikana kama Magufuli Hostel kwa suala la expansion joint. Niliongea kwa muda mrefu, yale mabweni mlituambia yamegharimu shilingi bilioni 10, lakini wengine wanasema shilingi bilioni 53, lakini madhara yake tumeyaona. Mnatuambia expansion joint; mimi navyojua joint ni pale kwenye maungano. Sasa kama zimepasuka mpaka maeneo mengine kwenye makabati na wapi, joints hapo ziko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naomba kabisa CAG afanye utafiti na ukaguzi wa kina, aje atuletee ripoti, hayo mabweni yamegharimu shilingi ngapi? Kwa nini kumekuwa na huo mpasuko? Kwa nini aliyeripoti akapelekwa Polisi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nilitaka kuzungumzia ni kuhusu matokeo ya mitihani ya kidato cha nne. Tumekuwa tukizungumza mara zote na kwa historia, nashukuru kwamba Kamati imeleta summary kwamba kwa miaka mitano na hata hiyo mingine, ufaulu haujawahi kuzidi asilimia thelathini kwa maana ya division one mpaka division three. Naamini ina maana division four na zero, hiyo ni sawa na zero tu.

Hawaendi popote. Kwa hiyo, ina maana asilimia 70 ya wanafunzi wanaomaliza kidato cha nne kwa miaka yote, hawaendi popote. Halafu tunazungumzia ubora wa elimu. Ukiangalia, hiyo asilimia 30, asilimia zaidi ya 80 wanatoka shule binafsi. Halafu Serikali hii inawaambia watu wenye shule binafsi, ni marufuku watoto kukariri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishangaa hii Serikali, tumesema siku zote, haiwezekani Serikali ambayo ina shule zake, yenyewe iwe refa, iwe mchezaji, iwe kocha; haiwezekani. Tukasema ni lazima kuwe na chombo maalum kitakachosimamia hizi shule; na ndiyo sababu kumekuwa na ubaguzi mkubwa kwenye suala la ukaguzi katika shule za private. Wanalipa shilingi 5,000 kwa kila mwanafunzi, lakini kwenye shule za Serikali ni bure na ndiyo sababu hakuna ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa nadhani ni muhimu sana Serikali iangalie kwamba kuna umuhimu wa kuwa na chombo ili kudhibiti ubora wa elimu hapa nchini, na sio wao wenyewe wanasimamia, shule nyingine zinakuwa hazina hata vyoo, hazifungwi, zinaendelea, zinasajiliwa, lakini za private hazifanyiwi hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni suala la afya. Kwenye suala la afya napongeza juhudi zote, lakini niseme tuna tatizo kubwa la watumishi wa Wizara ya Afya na wamekiri wenyewe kwenye kitabu chao kwamba wana upungufu wa asilimia 48. Sasa hivi wana asilimia 52 tu. Kwa hiyo, jambo ambalo linanishangaza, nadhani linawashangaza Wabunge wote, kwamba tuna ma- graduate kibao wako mitaani, tunahamasishwa tufungue Vituo vya Afya na Hospitali, lakini Hospitali hizo na Vituo vya Afya vinafungwa kwa sababu hakuna watumishi. What a contradiction? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nilikuwa nadhani Serikali ituambie, tatizo ni kwamba hawana fedha za kuwalipa? Kwa sababu madaktari wapo, lakini hawaajiriwi, watu wanaendela kufa, akina mama wanajifungua wanakufa, watoto wanakufa na watu wazima wanakufa. Kwa hiyo, nilikuwa nadhani mtuondelee hiki kitendawili kwamba kama Serikali inakusanya kodi kama ambavyo mnatamba, kwa nini mkose fedha za kuwalipa wataalam ambao watakuja kusaidia maisha ya wananchi wetu kwa sababu naamini hakuna Taifa lolote linaloendelea kama wananchi wake wana afya mbovu. Kwa hiyo, niseme tu kwamba tuna kila sababu ya kuishawishi, kuiomba au kuishauri Serikali, ikahakikishe kwamba Watumishi wa Wizara ya Afya wanapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni suala la Mloganzila. Niseme tu kwamba ile hospitali ni ya kufundishia (Training Hospital). Tunaomba sana ibaki kwenye lengo lile lile, maana yake kulikuwa kuna maneno kwamba Hospitali ya Muhimbili ihamie kule na nini. Nadhani sisi kama Watanzania, ni lazima tu-think globally but acting locally.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda vyuo vikuu vyote duniani vikubwa, vinakuwa na hospitali zake ambazo zina specialty. Hii yetu ya Mloganzila ina specialty yake ya moyo.

Hii ilikuwa ni kwa East Africa kwamba wagonjwa wa moyo wa kutoka Kenya, Rwanda na Uganda watibiwe hapa. Leo nasikia tayari kuna baadhi ya wagonjwa wa Mwaisela wameshahamishwa wamepelekwa kule, hali ambayo inafanya Madaktari wa Muhimbili watoke Muhimbili waende kutibu kule Mlonganzila, jambo ambalo haliwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nadhani lengo lile la awali libaki pale pale ili ile Hospitali hii ya Chuo Kikuu cha Muhimbili ibaki na malengo yaliyokusudiwa. Maana yake tutaonekana watu wa ajabu kwamba Uganda wao wanaendelea, sisi Tanzania ibadilike iwe hospitali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Kamati yangu.