Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa ulinzi wake, lakini pia nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwapongeza sana Wenyeviti wa Kamati, Kamati ya UKIMWI na Kamati ya Maendeleo ya Jamii na hasa nampongeza sana Mheshimiwa Serukamba kwa ripoti yake nzuri na hasa nimesoma katika ukurasa wa 41 kuhusu pads za watoto wa kike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili tuliliongea katika Kamati yetu ya Bunge Wanawake (TWPG) na tukaunda vikundi vidogo vidogo vinavyoshughulikia mambo ya jinsia, bajeti ya jinsia. Nakumbuka kikundi kinachoshughulikia taulo za wanawake ni kikundi cha ambacho Mwenyekiti ni Mheshimiwa Zaynabu Vulu na Katibu wake ni Mheshimiwa Catherine Ruge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili tumelishughulikia na Bunge la mwezi Novemba, 2017 tuliwaita Wakurugenzi kutoka Wizara mbalimbali tukakaa nao, tukajadili mambo mengi yaliyohusu jinsia na mambo yaliyohusu watoto wa kike na hasa taulo za kike na tukaiomba Serikali kwamba isipoweza kupunguza bei, basi watoe bure taulo hizo kwa sababu hata wanawake wa vijijini wanapata shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina imani kabla ya Bunge la Bajeti kama tulivyowaagiza wale Wakurugenzi wapeleke taarifa ofisini kwa Mawaziri wao kwamba tukutane na Mawaziri, Waziri wa TAMISEMI na Waziri wa Afya watuambie kwamba habari ya taulo za kike kupunguzwa bei au kutolewa bure kwa wanafunzi limefikia wapi? Ninaamini Mawaziri watalishughulikia na kabla ya Bunge la Bajeti watatuletea taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la uhaba wa watumishi au uhaba wa wauguzi katika Mkoa wangu. Mheshimiwa Rais anafanya kazi nzuri ya kuhamishia Makao Makuu Dodoma na sasa watumishi wengi wamekuja Dodoma na watumishi hawa wanahudumiwa na wauguzi wachache na watumishi wachache wa hospitali wa hapa Dodoma. Hatujaongezewa wauguzi, hatujaongezewa madaktari na kama Kamati ya Maendeleo ya Jamii walivyosema kwamba Hospitali ya Benjamin Mkapa haitumiki vizuri, ni kweli haitumiki vizuri kwa sababu ina vifaa vingi, ina wataalam wachache na ina wauguzi wachache sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini kabisa kwamba Waziri utalichukua hilo na utaongeza watumishi pale Benjamin Mkapa na vifaa tiba najua vipo vya kutosha, lakini hatuna wauguzi na watumishi wa kutosha wa kuweza kutumia vile vifaa ili kupunguza foleni kubwa iliyopo Hospitali ya Mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia uhaba wa walimu katika Mkoa wangu. Siku moja tulikwenda na Waziri wa TAMISEMI hapa Iyumbu tu mjini na tukakuta wanafunzi wako 800 na walimu wako wanane. Hebu fikiria hao walimu wanavyofanya kazi ngumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shule moja ya msingi Ntomoko, shule ya msingi Ntomoko, wanafunzi ni wengi lakini walimu wako watatu. Ninaamini Serikali itaona namna ya kuwaongeza walimu hasa katika shule zetu za msingi na hata shule zetu za sekondari pale ambapo kuna upungufu mkubwa wa walimu. Kwa sababu shule za vijijini, shule ambazo ni remote areas walimu ni wachache mno na hasa walimu wa sayansi, kiasi kwamba hawakidhi mahitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la capitation. Zamani fedha za capitation zilikuwa zinapelekwa shuleni na Walimu Wakuu ndio waliokuwa wanahusika kununua vitabu. Tangu suala la elimu bure, Serikali au Wizara imeamua kununua vitabu kuanzia vitabu vya wanafunzi wa darasa la nne hadi wanafunzi wa darasa la saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna upungufu mkubwa sana wa vitabu mashuleni. Siyo Dodoma tu, naamini hata mikoa mingine kuna upungufu mkubwa wa vitabu vya wanafunzi kuanzia darasa la tano hadi darasa la saba. Tunategemea kwamba hao wanafunzi wanapoanza darasa la tano, wanatarajia kufanya mitihani ya kuingia kidato cha kwanza. Kwa hiyo, kama hakuna vitabu, hawawezi kusoma vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Dodoma takriban kitabu kimoja wanatumia watoto sita hadi nane. Kwa hiyo, naomba tu Serikali yetu sikivu ione umuhimu sasa wa kununua vitabu na kuvipeleka mashuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna upungufu mkubwa wa madarasa. Tangu Serikali itoe elimu bure mashuleni, sasa hivi kuna mfumuko mkubwa sana wa watoto wanaoanza darasa la kwanza. Kwa hiyo, madarasa hayatoshi na hakuna namna ya wananchi kuchangishwa au wazazi kuchangishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hakuna namna ya kuongeza madarasa. Kwa hiyo, naomba Serikali sasa itoe tamko, namna gani tunaweza kuongeza madarasa bila kuchangisha wazazi? La sivyo, Serikali ichukue jukumu la kujenga madarasa ili wanafunzi wanaoingia darasa la Kwanza na wale wanaoanza form one wapate namna ya kusoma na namna ya kusoma kwa uzuri zaidi, wasisome chini ya miti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napongeza sana, tumetoka kuwa na semina na Taasisi ya Moyo kule Dar es Salaam. Niwapongeze sana kwa kazi nzuri...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)