Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja zote mbili zilizowasilishwa na Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii pamoja na Kamati ya Masuala ya UKIMWI. Napongeza kazi nzuri walizofanya Kamati zote mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia maoni yangu katika masuala matatu yaliyonigusa katika taarifa ya Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza, katika ukurasa wa 49 hadi mwanzo wa ukurasa wa 50, Kamati imetoa maoni na kupendekeza Serikali ilipe kipaumbele suala la kutoa elimu ya lishe kwa jamii. Naafikiana na mapendekezo haya lakini pia naomba ligusiwe suala la watu au jamii ambayo inakabiliwa na janga la njaa. Pamoja na umuhimu wa kutoa elimu juu ya lishe, Serikali ipange mkakati wa kuwapa chakula jamii zinazokabiliwa na ukame wa muda mrefu katika Wilaya za Kaskazini, Mashariki ya nchi yetu hususan Wilaya za Longido Ngorongoro na Monduli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala langu la pili, linahusu maboresho yanayohitajika kwa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC), tazama ukurasa wa 50. TBC Radio ndicho chombo kinachotegemewa kupata habari, elimu na burudani na asilimia kubwa ya wananchi wanaoishi vijijini mahali pasipo na TV wala magazeti au upatikanaji wa Radio za FM. Kwa jamii za pembezoni hasa wale waishio karibu na mipaka ya nchi jirani, wanaishia kupata huduma muhimu ya habari, elimu na burudani kupitia radio za nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maboresho yaliyopendekezwa na Kamati, naomba kipaumbele kitolewe katika kuboresha miundombinu ya kisasa na kuiwezesha Radio ya Taifa isikike katika kila kona ya nchi yetu kupitia mid-wave(MW) na FM frequencies.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu, ninalopenda kuchangia ni kuhusu Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima kama ilivyoelezewa katika ukurasa wa 61 wa taarifa ya Kamati. Nakiri kwamba ni kweli Elimu ya Watu Wazima imedorora katika nchi yetu, lakini siafiki taasisi hii kufutwa bali ihuishwe kwani bado kuna watu wengi katika nchi yetu na hasa katika jamii za wafugaji ambao hawajui kusoma na kuandika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile, napendekeza Serikali ianzishe taasisi mahsusi ya Elimu ya Awali nchini. Hili ni kutokana na hali halisi kwamba Kiwango cha Elimu ya Awali ni duni mno katika jamii ya vijiji ambapo umbali wa shule kwa kaya nyingi ni kati ya kilomita kumi hadi kumi na tano hasa Umasaini. Kwa maoni yangu kazi ya Taasisi ya Elimu ya Awali itakapoundwa itakuwa ni pamoja na:-

(1) Kuhakikisha kila kitongoji kwa jamii za vijijini wanakuwa na shule ya awali yenye kukidhi haja ya kuwajengea watoto wetu wachanga msingi bora wa elimu.

(2) Kubeba jukumu la kusomesha na kuajiri Walimu stahiki wenye sifa kamili za kutoa Elimu ya Awali kwa watoto walio chini ya umri wa kuanza elimu ya msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ilivyo kwa sasa utakuta katika vitongoji vilivyo mbali na shule ya msingi kwa watoto wadogo kuweza kutembea, shule za awali zinafundishwa na failures wa darasa la saba ambao ni wanakijiji wa kawaida tu wasio na taaluma yoyote ya ualimu zaidi ya kujua kusoma na kuandika.

(3) Kuandaa na kusambaza mitaala ya Elimu ya Awali katika shule zote za awali nchini pamoja na kuzisimamia shule za awali hadi zile za ngazi ya kitongoji kwamba Wizara ya Elimu inavyosimamia shule za msingi na sekondari.