Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii ili nami niweze kutoa mchango wangu katika Bajeti Kuu. Kwanza naomba kuunga mkono hoja hii ya bajeti ya Serikali kwa kuwa inakwenda kujibu matatizo ya wananchi wetu. Niipongeze Serikali kwa namna inavyoanza kutekeleza miradi ya vielelezo ambayo itakwenda kuharakisha maendeleo kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge. Reli hii kwa Mikoa ya Magharibi inakwenda kuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi kwa kushusha gharama ya usafirishaji na gharama ya maisha. Reli hii inakwenda kusaidia kushusha bei ya saruji kwa kupunguza gharama ya usafirishaji, kwa sababu Mikoa ya Magharibi haina kiwanda cha saruji na saruji hii imekuwa ikisafirishwa kwa mfuko Sh.5,000/= kwa hiyo na kuongeza bei ya saruji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, bei ya saruji baadhi ya Wilaya ni Sh.16,000/= wakati wilaya nyingine ni Sh.12,000/= hadi Sh.13,000/=. Inakwenda kushusha bei ya gharama ya kusafirisha ng’ombe kutoka Mikoa ya Magharibi na kuleta mikoa mingine. Inakwenda kupunguza gharama ya usafirishaji wa marobota ya pamba kutoka Mikoa ya Kanda ya Ziwa na kupeleka bandarini Dar es Salaam kwa ajili ya kusafirisha nje. Reli hii inakwenda kusaidia kupokea mizigo kutoka nchi ya Rwanda ambayo itapita reli ya kati na kuongeza kodi za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niipongeze Serikali kwa kuleta marekebisho kwenye Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa ili kupunguza ushuru wa mazao unaotozwa na Halmashauri za Wilaya kutoka kiwango cha asilimia tano hadi tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niipongeze Serikali kwa msimu mfululizo katika Awamu hii ya Tano, bei ya pamba mwaka jana ilitoka Sh.600/= mpaka Sh.1,000/=, mwaka huu bei ya pamba kwa kilo ni Sh.1,200/=, naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuwajali wakulima wa pamba. Kwa kupunguza ushuru huu pia kwa bei ya mwaka huu tunakwenda kuongeza Sh.24/= kwa kila kilo, lakini bado upo wigo mwingine, Serikali inaweza ikaangalia ni wapi pia iweze kupunguza tozo ili iweze kumwongezea mkulima bei ya pamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mfuko wa Uendelezaji Zao la Pamba. Mkulima amekuwa akichangia Sh.15/= na mnunuzi amekuwa akichangia Sh.15/=, sawa na Sh.30/= kwa ajili ya uendelezaji wa zao la pamba. Fedha hizi kwangu mimi naziona ni nyingi, kwa mfano 2015/2016 tani 149,000 zilikusanywa, mfuko huu uliwekewa Sh.4,483,350,000/=. Naishauri Serikali ifuatilie matumizi ya fedha hizi ili iweze kulinganisha, je, matumizi ya hizi bilioni nne yanamsaidia mkulima wa pamba? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hakuna tija mnunuzi apunguziwe Sh.10/= na mkulima apunguziwe Sh.10/=, wachangie shilingi tano tano, naamini itakwenda kusaidia katika kuendeleza zao la pamba katika mambo ya utafiti. Ukizingatia Serikali imekuja na mbegu mpya ambayo inaongeza uzalishaji, kwa hiyo kilo za pamba zinakwenda kuongezeka na fedha zinakwenda kuwa nyingi sana, kwa hiyo Sh.10/= pekee inatosha kuendeleza zao la pamba katika shughuli za utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado pia kuna tatizo katika ucheleweshaji wa usambazaji wa mbegu na dawa na wakati mwingine hayatoshelezi. Nashauri Mabaraza ya Madiwani yapewe mamlaka ya kuweza kuuhoji huu mfuko ili utekelezaji uweze kuharakishwa. Kwa kufanya hivyo, naomba mfuko huu kama kuna viongozi wa kisiasa wasiwe viongozi katika Mfuko wa CDTF ili kuepuka mgongano wa maslahi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niongelee athari zitakazopatwa na Halmashauri kuhusu kupunguza ushuru huu. Halmashauri za Mkoa wa Simiyu zaidi ya asilimia 60 ya bajeti yake ya mapato zinategemea ushuru wa pamba. Naishauri Serikali ifanye kama ilivyofanya 2003, baadhi ya vyanzo vya mapato vilivyokuwa kero kwa wananchi vilifutwa, Serikali ilifanya mapitio kuangalia athari ya bajeti na baadaye Halmashauri hizo zilifidiwa. Naomba Serikali iweze kufidia Halmashauri zitakazoathirika kwa kushuka tozo ile kwa asilimia mbili kwa sababu zitashindwa kujiendesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2016/2017, umeendelea kutekeleza maeneo ya kipaumbele kwa kufungamanisha maendeleo ya uchumi na watu. Serikali imeendelea kusomesha kwa wingi kwenye fani za ujuzi maalum ambao pia ni adimu ili kuendana na mahitaji katika viwanda tarajiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana hawa wana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.