Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia kwenye mjadala uliopo mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa rehema na baraka zake ambazo siku zote zimetuwezesha kuwatumikia Watanzania vyema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, napenda kuipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali inazochukua katika kuhakikisha maisha ya watu wetu yanaendelea kuboreka siku hadi siku. Tumekuwa na mjadala mrefu juu ya mambo ya makinikia lakini taarifa za hivi punde zinaonesha kwamba tunaelekea kwenye right direction, hongera sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 nilipochangia nilikuwa bitter, nilitumia lugha kali kwa Wizara hii na nilikuwa na sababu ya kufanya hivyo. Nilifanya hivyo kwa sababu Kamati ya Bajeti walikuja hapa wakalalamika kwamba Wizara hii imekuwa na shingo ngumu, ilikuwa haisikilizi ushauri inayopewa na Kamati. Nafurahi mwaka huu mambo yamebadilika. Wizara imekuwa sikivu, hongereni sana. Huo ni mwanzo mzuri, tuendelee kuwa wasikivu, maana wote tunajenga nchi hii kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa mapendekezo ambayo watu wengi humu tumekuwa tukipigia kelele ni kuongeza tozo ya mafuta ili twende kupata huduma za maji vijijini. Serikali imesikia hilo, imeongeza tozo kwenye mafuta. Wenzetu wa Kamati ya Bajeti wanashauri kwamba fedha yote itakayopatikana na ongezeko hili, asilimia 70 tuipeleke kwenye maji vijijini, asilimia 30 iende kwenye maji mijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tunapiga kelele kuhusu maji vijijini? Kwa nini tunapiga kelele kuhusu huduma ya maji? Takwimu za Wizara ya Maji zinaonesha kwamba tumepeleka maji vijijini kwa asilimia 72 peke yake. Hii maana yake nini? Maana yake ni kwamba takriban Watanzania zaidi ya milioni 10 vijijini hawana maji. Hatuwezi kuiacha hali iendelee kuwa hivi. Lazima tuongeze nguvu kuhakikisha tunapeleka maji vijijini. Ndiyo maana naipongeza Serikali kwa kuwa sikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zimekuwepo hisia za hofu kwamba pengine uamuzi huu wa kuweka tozo umekuwa ni blanket, utagusa kila aina ya mafuta. Naiomba Serikali itakapokuja kuhitimisha hapa, itueleze tozo ile imewekwa kwa mafuta ya aina gani? Vilevile, Wizara itakapokuja kuhitimisha hoja ituambie ina mkakati gani wa kuhakikisha tunafuta Railway Development Levy kwa mafuta ya ndege? Kwa sababu jambo hili limetusababishia kukosa biashara ya kuuza mafuta ya ndege kwa sababu kampuni za ndege zinajaza mafuta Kenya kwa sababu wenzetu hawakuweka levy hii. Kwa hiyo, naomba wakija watupe ufafanuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipochangia Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji nilisema mchawi wetu wa Tanga ni Wizara ya Fedha na Mipango. Nilisema hivyo specifically kwa sababu ya Kiwanda cha Tanga Fresh. Tunaingiza maziwa ya dola milioni 40; tuna uzalishaji wa maziwa hapa nchini lita bilioni mbili; lakini usindikaji tunasindika only 1.4 percent. Hii haiwezi kuwa sawa. Tanga Fresh kwa miaka miwili sasa wanahangaika kutaka kuongeza uwezo wa kiwanda chao wanazuiwa na TRA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanazuiwa na TRA kutumia majengo yao kama dhamana ya kukopea. Kwa sababu gani? Kwa sababu aliyewauzia majengo Tanga Fresh, alikwepa kodi. Mkwepaji kodi huyu anajulikana, anafanya biashara katika nchi hii. TRA wanaacha kwenda kumkamata mkwepa kodi, wanamuadhibu Tanga Fresh. Hii haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanga Fresh wamemwandikia barua Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji; Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji ameandika barua tangu mwanzoni mwa mwezi wa Tatu kuja Wizara ya Fedha na Mipango. Mpaka leo hatuna jibu. Nataka mtakapokuja kuhitimisha mtuambie, nini hatma ya Kiwanda cha Tanga Fresh? Kwa nini wanawaadhibu Tanga Fresh kwa kosa ambalo siyo la kwao? Kwa nini uzembe wa wafanyakazi wao usababishe Tanga Fresh wakose haki yao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, naipongeza Serikali kwa jitihada inazofanya za kuhakikisha suala la lishe linapewa kipaumbele. Tuna watoto milioni 2.7 waliodumaa; tuna watoto 600,000 wenye utapiamlo; hii ni hatari kwa Taifa letu. Naipongeze Serikali kwamba kwa mwaka huu wameonesha commitment ya kutenga shilingi bilioni 11.4 zipelekwe kwenye Halmashauri zetu. Rai yangu ni kwamba tuhakikishe fedha hizi zinakwenda kwa wakati. Ziende zikaondoe baa hili. Pili, mtakapopeleka fedha hizi, mpeleke maagizo maalum kwamba huko kwenye Halmashauri fedha hizi zisibadilishiwe matumizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie sula la huduma za kifedha. Tunayo Taasisi inaitwa SELF Microfinance. Mwaka 2016 walipanga kutoa mikopo ya shilingi bilioni 12, lakini wakatoa shilingi bilioni tisa; mwaka huu 2017, wamepanga kutoa shilingi bilioni 20. Naipongeza sana taasisi hii kwa kazi kubwa inayofanya. Wakati nikiipongeza Serikali, hebu fanyeni mambo pale. Mmeondoa Bodi, haipo in place, wanashindwa kutoa mikopo kwa sababu bodi haipo. Harakisheni mhakikishe bodi inakuwa in place ili SELF iweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni shilingi milioni 50 za kila kijiji. Fedha hizi hebu tuziwekee utaratibu maalum. Tumeshasema hapa kwamba njia nzuri ya fedha hizi kwenda kwa wananchi hebu tuhakikishe mfumo wa benki za jamii (Community Banks) unaimarishwa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)