Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Salome Wycliffe Makamba

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru nami niweze kuchangia bajeti hii japo kwa dakika tano. Nimesoma vizuri kitabu cha Mheshimiwa Waziri. Jambo kubwa lililopelekea tukashindwa kufanikisha bajeti iliyopita ni ukosefu wa fedha za wahisani. Kukosa fedha za wahisani Mheshimiwa Waziri anasema eti tulichelewa kufanya negotiation na wahisani ndiyo maana tulichelewa kupata pesa.

Mheshimiwa Waziri, wahisani wanatupa pesa pale tutakapokuwa tumetimiza masharti ya kupewa mikopo. Hatuwezi kupewa pesa kama Serikali yetu haizingatii utawala wa kidemokrasia, haizingatii utawala bora, uhuru wa vyombo vya habari na tunapitisha Sheria kandamizi zinazowakandamiza Watanzania. Mheshimiwa Waziri angekuwa mkweli juu ya hilo, kwamba tunahitaji tusimamie utawala bora, utawala wa sheria na kila mtu awe chini ya sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anasema kwenye kitabu chake, ili tuweze kupunguza deni la Taifa, ameamua kuwekeza miundombinu kwenye maeneo ambayo yanachochea uchumi. Miundombinu hiyo anataja ni barabara, reli na ndege. Bajeti inapitishwa tunakwenda kujenga kiwanja cha ndege Chato; hivi kweli Tanzania nzima tukitafuta sehemu zenye vichocheo vya kiuchumi utataja Chato kweli? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Chato wameweka traffic light!

Inapita gari moja baada ya saa nzima ndiyo inapita gari pale. Wanaweka kiwanja cha ndege wanasema pale ndiyo kuna vichocheo, tupate pesa kwa ajili ya kuboresha uchumi kwenda kulipa deni la Taifa. Hizi ni ndoto ambazo haziwezi kutekelezeka. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeweka Sh.40/= kwenye mafuta ikiwa ni mbadala wa Motor Vehicle Licence. Kweli mafuta ya taa wataalam wetu waliosomeshwa na pesa za nchi hii wanasema tupandishe mafuta ya taa kwa sababu petroli imepanda, kwa sababu ndiyo njia pekee ya kuzuia uchakachuaji magari yasiharibike. Huo ndiyo utaalam wa Wazalendo wa Tanzania waliowekwa kwamba tuwakandamize masikini kuokoa magari yasiharibiwe, mafuta yatachakachuliwa. Huo ndiyo utaalam umeishia hapo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli sijaelewa vizuri kuhusu taratibu za manunuzi na Mheshimiwa Waziri wa Fedha anapokuja atueleze; kweli bado tunazingatia Sheria ya Manunuzi Tanzania au ni mtu mmoja ndio anaamua tununue vipi, tufanye vipi shughuli za manunuzi Tanzania?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba akija aje atueleze ni taratibu ipi ya manunuzi ilitumika kuwapa mkataba watu wanaokuja kujenga reli ya Dar es Salaam – Morogoro? Atueleze utaratibu upi ulitumika kununua zile ndege mbili ambazo mpaka sasa hivi inasemekana ndege moja iko down? Utaratibu upi ulitumika wa manunuzi kujenga barabara kwa pesa za uhuru barabara ya Mwenge – Morocco? Ni utaratibu upi umetumika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ndiyo mambo tulitegemea kuyaona kwenye bajeti hii ambayo sisi tulipitisha hapa sheria, watu wanakwenda kinyume na sheria, Bunge linadharauliwa kile tulichokifanya, halafu tumebaki tunacheka, tunapiga makofi, tunapongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa hivi bado sijapata picha ya zile propaganda zinazoenezwa kuhusu suala la madini na migodi. Tunaonekana kwamba sisi...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)