Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kutoa mchango wangu kwenye bajeti hii ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kutuletea bajeti nzuri lakini pia niwashukuru sana watendaji wao wakuu, Katibu Mkuu pamoja na timu yao hiyo nyingine iliyopo ofisini. Wamefanya kazi nzuri na wametuletea bajeti ambayo kila Mtanzania aliposikia alifurahia na alipongeza. Kwa hiyo, nawapongeza sana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niwapongeze pia TRA kwa makusanyo yao mazuri ambayo kupitia hayo yametusaidia kufanya mambo makubwa kwa mwaka huu unaoisha na naamini hata kwa mwaka ujao tunaweza kuendelea kufanya mambo makubwa zaidi. Tumelipa mishahara sisi wenyewe, tumelipia reli sisi wenyewe, tumelipia ulinzi na usalama wa nchi yetu sisi wenyewe, tumelipia ndege ingawa watu wanazidharau lakini tumelipa sisi wenyewe, kwa hiyo imetusaidia kujitegemea kama nchi kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kwa watu wa TRA ni kwamba waweze tu kuongeza kujenga mazingira mazuri kwa walipa kodi wetu ili makusanyo yao yaweze kuongezeka. Wafanye juu chini kuwafanya walipa kodi wetu wajisike fahari kulipa kodi yao, waone kwamba wanastahili kulipa, waelewe kwamba kulipa kodi ni ustaarabu lakini wataona hivyo baada ya wao TRA pia kujenga mazingira mazuri kwa ajili yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia naomba kodi za TRA zieleweke, mtu akitaka kuanza biashara fulani ajue kabisa atatakiwa kulipa kodi zipi. Kuwe na namna za kodi elekezi ambazo TRA wanakuwa nazo ili mimi nikitaka kufanya biashara nijue TRA watachukua hela yao kiasi gani hapa. Unajua wafanyabiashara wanataka mambo yao yajulikane, yawe wazi na wanataka uhakika ili atakapoingia kwenye biashara aweze kupata faida anayoitarajia. Uchumi wetu unakua, kwa hiyo lazima pia TRA wajenge mazingira ya biashara kukua, ya kilimo kukua na uchumi wetu kuendelea kupanda vinginevyo makusanyo yao yanaweza yasiwe endelevu sana kama biashara na kilimo havikui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie pia upande wa ajira pamoja na mzunguko wa fedha, hivi vitu vina uhusianao sana. Fedha au pesa inazo tabia nyingi lakini tabia mojawapo ni kwamba pesa ni adimu, money must be scarce or limited in supply na pesa inazunguka kwa mtu ambaye anafanya kazi, pesa haizunguki tu kwa zamu kwamba ni zamu yako imefika, inazunguka kwa mtu ambaye anafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naisihi Serikali itengeneza mazingira ya watu kufanya kazi ili kwamba waweze kupata pesa. Naiomba Serikali waanze kufikiria miradi ambayo itazalisha au itatoa mazao kwa haraka, inatoa faida kwa haraka, hiyo nayo watie nguvu hapo ili kwamba watu wafanye miradi kama hiyo waweze kupata pesa. Miradi ambayo tunaita ni quick wins au low hanging fruits ili watu waweze kujiingiza huko na kupata hela mzunguko wa pesa uweze kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi kama hiyo ni kama wachimbaji wadogo, viwanda vidogo vidogo vikitiwa nguvu na moyo vinaweza vikafanya mzunguko wa fedha ukawa mkubwa kwa sababu wengi wataingia huko. Pia miradi mikubwa ya kielelezo ambayo nchi yetu imekwishakuianza iajiri Watanzania. Najua kandarasi kubwa wamepewa watu wa nje lakini tuwe na utaratibu ambao hata nadhani sheria zetu unaukubali kwamba Watanzania waajiriwe wengi kwenye miradi hii, wanaweza kuajiriwa wale watu wakubwa wakubwa kule juu kidogo lakini hapa katikati na huku chini waajiriwe Watanzania ili waweze kupata pesa iweze kuzunguka hapa nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia NGO’s zilizoko kwenye nchi yetu hii walazimishwe waajiri Watanzania. Hizi NGO’s nazo wanapokuja hapa wanalazimisha kuleta watu wao kutoka nje. Nafikiri umefika wakati sasa kazi hizo zinazofanywa kwenye NGO’s zifanywe na Watanzania kwa sababu tuna ujuzi na weledi wa kutosha kufanya kazi hizi ili pesa zinazokuja kwa sababu wanazileta kwa lengo la kusaidia umaskini wetu, basi umaskini wetu uwe ni fursa isiwe ni kitu ambacho ni balaa au kinatupita pembeni. Watanzania wengi waajiriwe kwenye hizi NGO’s kuanzia chini, katikati na hata juu ili pesa zinazokuja zizunguke hapa na zitusaidie kweli kama wanataka kuondoa umaskini kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kazi za makampuni makubwa ya hapa nchini pia yapewe kazi kubwa kubwa. Nimesikia juzi Mheshimiwa Makamu wa Rais anasema wakandarasi wanaweza wakapata kazi isiyozidi shilingi bilioni 10, nadhani hili ni jambo zuri kwa sababu hawa wakandarasi wa ndani wakipewa pesa kama hiyo itafanya izunguke hapa ndani na kufanya mazunguko wa fedha uwe mkubwa hapa nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la kukuza viwanda kwenye nchi yetu. Kwanza nipongeze kabisa hotuba ya Mheshimiwa Waziri hasa kwa upande wa viwanda vinavyozalisha mafuta ya kula kwamba wameweka tozo/ushuru kwenye mafuta ghafi yanayoingia kutoka nje hasa yanayotokana na mawese. Hongera sana kwa jambo hili kwa sababu tozo hii ilikuwa imeondolewa hapo nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba tozo hii iongezwe badala ya asilimia 10 aliyoiweka Mheshimiwa Waziri iwe asilimia 15 ili kulinda viwanda vyetu vya mafuta ya kula hapa ndani lakini pia kulinda wafanyabiashara wetu. Kwa sababu hata hayo mafuta wanayosema wanaingiza mafuta ghafi lakini ukiyachunguza asilimia ya mafuta ghafi ni kama 10 tu, asilimia 90 ya mafuta haya yako kamili kabisa. Kwa hiyo, ili tuweze kujenga viwanda vyetu, ushuru kwa bidhaa zinazotoka nje lazima uongezeke ili tuweze kulinda viwanda vyetu hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nizungumzie suala la wastaafu hasa wale wanaopata pesa zao kupitia Hazina, walio na account zao Benki ya Posta. Hawa wana dirisha la kupata mikopo huko Benki ya Posta lakini wanapoomba mikopo yao nyaraka zinachelewa sana kutoka Hazina tofauti na nyaraka au na wale ambao walikuwa kwenye Mifuko ya PSPF na LAPF.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Mheshimiwa Waziri awafikirie hawa wastaafu maana na wenyewe bado maisha yanaendelea, kwa hiyo tuwasaidie wale wanaopata hela zao kutoka Hazina wakiomba mikopo kupitia Benki hii ya Posta wapewe mikopo yao mapema, hiki kisingizio cha nyaraka zinachelewa nadhani hakina sababu ya kuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kama muda wangu pia utakuwa haujaisha niongelee suala la …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)