Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kuwepo hapa tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuwapongeza Mawaziri na hasa nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha pamoja na Naibu wake. Nimpongeze sana pia Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kuwa mshauri mzuri kwa Waziri na hatimaye kutuletea bajeti yenye tija na inayojali maslahi ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Kondoa wana msemo usemao kwamba mwana wa mukiva amanyire michungiro. Usemi huu una maana kubwa sana na ndiyo maana nikampongeza Naibu Waziri kwa sababu ya ushauri wake mzuri na kuweza kumsaidia majukumu Mheshimiwa Waziri na hatimaye tumeletewa bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze sana Serikali kwa hatua zake katika kujali maslahi ya kundi la watu wenye ulemavu. Kubwa zaidi niipongeze Serikali, kuondoa kodi katika vifaa vya watu wenye ulemavu, ukurasa wa 71. Vifaa hivi ni muhimu sana. Vifaa hivi ndivyo vinavyowasaidia watu wenye ulemavu kuweza kutekeleza majukumu yao lakini pia ni sawa na miguu au mikono ya watu wengine ambayo wamepewa na Mwenyezi Mungu. Kwa hiyo, kwa kitendo hiki cha kuondoa kodi katika vifaa vya watu wenye ulemavu ni faraja kubwa sana kwa sababu hivi sasa vifaa hivi vitakuwa na bei angalau afadhali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, calipers ambazo zimekuwa zikitumiwa na watu wenye ulemavu zinafika kwenye Sh.400,000/= mpaka Sh.500,000/= lakini nina matarajio makubwa sana kwamba baada ya kuondolewa ushuru wa kodi kwa vifaa hivi, basi vitapungua na walemavu wengi wataweza ku-afford vifaa hivi. (Makofi)

TAARIFA . . .

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hiyo kwa mikono miwili na kwa sababu mwenzangu amekuwa akitumia sana vifaa hivi, kwa hiyo, anachokizungumza anakifahamu kwa undani zaidi. Kwa hiyo, niungane naye tu katika kuipongeza Serikali kwa maana kwamba sasa hiyo gharama ambayo imekuwa ikitozwa itapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda katika Hospitali ya CCBRT, Hospitali ya KCMC lakini pia Hospitali ya Seliani ambazo zimekuwa zikihudumia sana watu wenye ulemavu, naamini kabisa kwamba msamaha huu wa kodi uwatawasaidia. Kwa maana hiyo pia tutaweza kuboresha hospitali yetu ya Muhimbili ili basi na wenyewe waweze kuboresha zaidi kitengo hiki cha huduma ya vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naipongeza kwa moyo wa dhati kabisa Serikali na niendelee tu kuipongeza Wizara, Mama yangu Ndalichako, Mheshimiwa Waziri Mkuu ambaye pia hivi karibuni alipokea vifaa vya watu wenye ulemavu ambavyo vimesambazwa katika shule na vyuo mbalimbali. Kwa hiyo, naamini kabisa kwamba Serikali hii imekuwa ikijali maslahi na kuangalia kundi hili la watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizi na kuishukuru Serikali, nitoe tu pia ushauri kwa Serikali kwa sababu kuhusu Kitabu hiki cha Hali ya Uchumi wa Taifa kwa mwaka 2016. Pamoja na kwamba tumepunguza kodi lakini bado kuna mahitaji mengi ya watu wenye ulemavu. Kwa hiyo, ni vyema katika bajeti ijayo tuone ni kwa jinsi gani tutasaidia zaidi kundi hili. Kwa mfano, maisha ya watu wenye ulemavu ni ya chini sana na hasa maeneo mengi ya vijijini hali zao za kiuchumi ni mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapokuja na bajeti tuone kundi hili tunaliangalia vipi? Kwa mfano, kwa hivi sasa tulipo katika Sera ya Serikali katika kuhakikisha kwamba inajikita zaidi katika viwanda, pia tuangalie hivyo viwanda ni kwa jinsi gani vitaweza kutoa ajira kwa watu wenye ulemavu, kuwasaidia na hali ngumu au maisha magumu waliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze pia Serikali na nimpongeze sana Mheshimiwa Rais ambapo nilizungumza kwa undani zaidi na nimekuwa nikilipigia sana kelele suala la TBC kutokana na uchakavu wa mitambo. Kwa sababu ni Serikali sikivu Mheshimiwa Rais alifanya ziara katika shirika hili na kujionea hali jinsi ilivyo lakini pia akaweza kutatua baadhi ya changamoto zilizopo katika shirika hili, nampongeza sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote haya, sasa ni wakati muafaka kabisa kwa wafanyakazi na watumishi wote wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kutoa ushirikiano, kufanya kazi kwa bidii katika kuhakikisha kwamba shirika hili linarudi katika hali yake iliyokuwepo hapo awali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri aliyoifanya ambayo hivi sasa Afrika inafahamu kwamba Tanzania inaye Rais anayeitwa Dokta John Pombe Magufuli. Kitendo alichokifanya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni kitendo cha kuungwa mkono na Watanzania wote, ni kitendo cha kuungwa mkono na wale wote wapenda maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu mimi katika kundi ninaloliwakilisha na naomba nijikite kulizungumzia hili, ni watu wenye maisha duni sana. Rasilimali hizi zikitumika ipasavyo ni dhahiri kabisa kwamba tutatatua changamoto nyingi za watu wenye ulemavu na kupunguza ukali wa maisha waliyonayo. Kwa maana hiyo, naomba sana nimpongeze Rais. Pia naamini kwanza ni fundisho ambalo tumejifunza lakini pia tutakuwa makini katika kupitisha mikataba ili mikataba hiyo isije ikatufunga sisi na ikatuumiza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali ya hivyo pia, ni wakati muafaka sasa na ningemwomba Mheshimiwa Rais aangalie mkataba na mwekezaji wa Pori la Loliondo ambao kwa muda mrefu umekuwa ni mgogoro unaoumiza ndugu zangu wa jamii ya Kimasai. Kwa hiyo, namwomba pia kuangalia ni kwa jinsi gani watapitia mkataba huu ili kama kuna vipengele ambavyo vinawabana au vinawaumiza wananchi vifanyiwe marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine pia ambalo napenda kuishauri Serikali, kwanza nampongeza Mheshimiwa Spika kwa kuunda Kamati kupitia Mkataba wa Sky Associate pamoja na State Mining Companies Limited (STAMICO) ili kuweza kurekebisha upungufu uliopo. Kabla Mkoa wa Manyara haujagawanywa madini haya yalikuwa ndani ya Mkoa wa Arusha na nafahamu kabisa ni kwa jinsi gani yamekuwa yakisaidia wakazi wa Arusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa ukienda hali ni ngumu sana kwa vijana wengi ambao walizoea kuchimba madini haya na kujipatia kipato, hali imekuwa tofauti. Kwa hiyo, kwa kitendo hiki cha Mheshimiwa Spika kuunda hii Kamati kupitia mkataba huu, ni faraja kubwa na naamini kabisa sasa mikataba hii itaangalia ni kwa jinsi gani itakwenda kuwanufaisha wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naishauri Serikali katika Halmashauri na Mikoa yetu kuangalia kwa mfano, ndiyo, tumepunguza kodi katika vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu lakini tunawaandalia mazingira gani mazuri ya kuwawezesha watu hawa kufanya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga hoja mkono.