Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Stephen Julius Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. STEPHEN J. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia bajeti hii ya Serikali. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Dokta Mpango, ama kweli ameonesha uwezo wake kwamba yeye ni mchumi aliyebobea kwa kutuletea bajeti ambayo kwa kweli imeandaliwa kisayansi sana. Pia nipongeze sana timu yake yote ya watendaji, ikiongozwa na Katibu Mkuu Ndugu Dotto James na timu nzima ya Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri ya kutengeneza bajeti ambayo inatoa majawabu ya matatizo ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasiasa na watu mbalimbali wamekuwa wakisema Serikali haisikilizi ushauri, Serikali haishauriwi, lakini nimesoma bajeti hii mambo mengi ambayo wananchi na Wabunge wamekuwa wakishauri yamezingatiwa. Kwa kweli, naomba sasa Mheshimiwa Mpango na timu yake waharakishe utekelezaji wa maamuzi ya kisera waliyoyafanya. Wamepunguza ushuru kwenye baadhi ya maeneo hasa kwenye mazao kwenye Halmashauri na wametoa maelekezo kwa TRA ifanye kazi bila kubughudhi wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natoka Shinyanga, Shinyanga tuna wafanyabiashara wadogowadogo na wakubwa, wafanyabiashara wanasumbuliwa, wanafuatwa na Polisi, wanafuatwa na PCCB. Maelekezo aheshimiwa Mpango naomba ayapeleke kule chini na ayasimamie kuhakikisha wafanyabiashara wanapewa mazingira wezeshi ili waweze kuzalisha na hatimaye Serikali iweze kupata kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia huu ushuru wa mama-ntilie, mama-lishe, wakulima wadogo wadogo wa bustani, yote ambayo wamepunguza maelekezo yaende kwenye Halmashauri zetu. Hatuwezi kujenga Taifa hili kwa kutegemea ushuru wa mama-lishe au wa mama anayeuza mboga. Kwa hiyo, nina imani na kazi yake, nina imani na uwezo wake, naamini atayazingatia haya na atapeleka maelekezo kwenye ngazi za chini za wananchi ili wasiweze kusumbuliwa na wananchi wangu wa Soko la Nguzo Nane kule Kambarage, Soko Kuu la Shinyanga waweze kufanya biashara zao bila kusumbuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wiki nzima hii nchi yetu imekuwa inazungumzia suala la mchanga wa dhahabu. Mimi nimewahi kuwa Naibu Waziri wa Wizara ya Nishati na Madini, nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge kama kuna vita yoyote duniani hivi leo ni vita ya uchumi. Yale yote mnayoyaona yanatokea Syria, watu wengi hawaelewi Syria ni nini kinatokea, pale kuna gesi ya Qatar inazalishwa na Wamarekani wanataka kusafirisha kwenda Ulaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Urusi ndiye muuzaji wa gesi mkubwa Ulaya, Marekani na Qatar wanataka wajenge bomba la gesi lipite Syria liende Ulaya, Urusi hataki lijengwe litaharibu soko lake, anamwambia Assad weka ngumu, hakuna bomba kupita mimi nitakusaidia. Marekani na yenyewe inaingiza nguvu zake kumng’oa Assad. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kuwaambia Waheshimiwa Wabunge, tunapozungumzia masuala ya uchumi ni mazito na yanaingilia hadi na Mataifa. Leo hii Tanzania tumetoa maamuzi haya, Mataifa ya kibeberu na kibepari yatataka kutuingilia ndani. Nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote tumuunge mkono Mheshimiwa Rais kwa maamuzi aliyoyafanya kwa sababu atakumbana na vikwazo mbalimbali vingi na ili Taifa letu liendelee ni lazima tuwe na utulivu wa kisiasa, lazima wananchi tutulie na tuelewe nini tunataka kupata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine unapata tabu Watanzania wanalalamika tunanyonywa, tunaibiwa, unapochukua maamuzi ya kudhibiti kunyonywa na kuibiwa ndipo watu wanaanza kugeuka tena. Mtu anaanza kusema ooh, kwa nini mnafanya hivyo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikiwa Naibu Waziri niliwahi kutoa tamko hapa Bungeni, nilitegemea Watanzania wenzangu na Wabunge wenzangu asilimia kubwa waunge mkono unyonyaji na unyanyasaji tuliokuwa tunafanyiwa na Mataifa ya kibeberu, lakini Wabunge wengine humu wakasimama kuanza kutetea mabeberu. Tulikuwa tunajenga bomba la gesi kutoka Mtwara kuja Dar-es-Salaam kuongeza uwezo…

TAARIFA . . .

MHE. STEPHEN J. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimsaidie rafiki yangu Mheshimiwa Heche. Cha kwanza jana kuna mtu amesema hapa ripoti ile ni rubbish.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hauwezi ukapinga ripoti ya kitaalam na ya kisayansi kwa maneno, unaipinga ripoti ya kisayansi kwa kuja na ripoti ku- counter ripoti iliyotolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wengine humu tumeshakuwa wakongwe. Nataka nimwambie mimi nikiwa Naibu Waziri, Halmashauri zote zenye migodi Tanzania zilikuwa zinalipwa dola laki moja, dola laki mbili. Nilisimamia kuhakikisha kwamba tunafuata sheria za nchi ambapo Halmashauri zetu zinapata asilimia 0.3 ya turn over ya migodi hii, leo Halmashauri ya Geita inapata zaidi ya bilioni tatu kwa mwaka, ilikuwa inapata dola laki mbili tu. Haya mambo yanawezekana, tukiwabana wawekezaji wanaonyonya kwa mikataba nyonyaji tunaweza kufanikiwa kupata mapato zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tufanye radical decisions, hatuwezi tukakaa mezani tunachekeana tukitaka kupata mapato zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Kongo pale thamani ya madini ya Kongo kwa takwimu inaonesha ina thamani zaidi ya GDP ya European Union lakini Kongo inaibiwa, watu wamekaa, wananchi wana shida. Leo Tanzania tumeweka mfano, Tanzania tume- set standard na wote tunatakiwa tumuunge mkono Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimetoka kwenye Vikao vya Bunge la Afrika, nchi nyingine za Afrika zinatuuliza, zinatusifia, zinamsifia Rais wetu na zina hamu aende akashiriki kwenye mikutano ya kimataifa ili waweze kujifunza nini anafanya Tanzania. Kwa hiyo, ndugu zangu nataka niwaambie muda wa kunyosheana vidole huyu kafanya nini, kafanya nini, utatupotezea muda kama Waheshimiwa Wabunge, ni vyema Waheshimiwa Wabunge tuanze kufikiria mapendekezo, maoni ambayo yataboresha ile task force iliyoundwa na Mheshimiwa Rais ya kuboresha mikataba hii. Kama una maoni mazuri yaandike yapeleke kwa Mheshimiwa Profesa Kabudi ili aweze kuyaingiza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mikoa yote yenye rasilimali haipati chochote, pelekeni mapendekezo angalau asilimia moja kinachovunwa kibaki kwenye mikoa husika ili maisha ya wananchi yafanane na rasilimali zao. Leo ukienda Geita maisha ya wananchi hayafanani na rasilimali zao. Ukienda Shinyanga almasi ile, maisha ya watu wa Kishapu na Shinyanga hayafanani. Ni lazima Serikali iamue kwa makusudi asilimia moja ama asilimia yoyote ambayo itaonekana kitaalam ibaki kwenye maeneo ya wananchi ili kuboresha maisha yao yafanane na rasilimali zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba na nimshukuru Mheshimiwa Rais amelianzisha jambo, amelisimamia, amelifikisha mwisho. Kitendo cha watu wa ACACIA kuja kukaa naye mezani maana yake sasa tunapata muafaka wa matatizo tuliyokuwanayo. Unaweza ukalianzisha jambo na usiweze kulisimamia, unaweza ukalianzisha jambo na usiweze kulifikisha mwisho, lakini tuna Rais ambaye ni mtendaji, mtekelezaji, analianzisha jambo, analisimamia na analifikisha mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachoomba Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote tumuunge mkono na tusimamie na tutambue kwamba hii vita tunayopigana siyo vita ndogo. Siyo vita ndogo kuanzia kwa makampuni, siyo vita ndogo kuanzia kwa Mataifa ya kibeberu kwa sababu kazi yao iliyobakia ni kunyonya rasilimali za Afrika. Wanakuja na mbinu mbalimbali lakini Waafrika lazima tusimame tuoneshe mfano na Tanzania imeonesha mfano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja.