Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa, nianze kwa kusema naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali jinsi inavyofanya kazi. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli na Watendaji wote wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Waziri Mkuu imeeleza kwamba bado tuna nafasi ya kuweza kukopa kama Watanzania kwa sababu deni letu ni himilifu. Naomba sasa tukope ili kusudi miradi ya maendeleo ambayo katika Jimbo la Njombe Mjini haitekelezeki, sasa itekelezeke. Mradi wa kwanza ni ujenzi wa barabara ya Itoni – Manda. Barabara hii miaka yote imekuwa ikiambiwa itajengwa ili kwenda Mchuchuma na Liganga, lakini haijengwi. Amewekwa mkandarasi kilometa 50. Kutoka Njombe ni kilometa 50 ndani ya Jimbo la Ludewa, lakini mkandarasi yule hana nguvu kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipande cha kuanzia Njombe mpaka linapoishia Jimbo la Njombe Mjini hakijaanza. Sasa tuombe kama fedha hiyo ya kukopa ipo. Kama Serikali ina fedha ya kutosha, iweke mkandarasi mwingine aanze kutengeneza barabara kutoka Itoni kwenda Manda ili kusudi tunaposema kwamba tuna mradi kielelezo wa Liganga, basi hata barabara iendane. Maana barabara ile ina uchumi mkubwa kwa wananchi lakini vile vile ina madini hayo yaliyopo huko ambayo tunahitaji yachangie uchumi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni maji. Maji katika Jimbo la Njombe Mjini ni tatizo kubwa sana. Miradi ya maji haitekelezeki. Wakandarasi wako site lakini malipo yanachelewa sana. Yuko Mkandarasi anafanya kazi katika mradi wa Igongo, malipo yake yanachelewa sana; na tunajua kabisa kwamba hela ya maji ni hela ambayo wote tunachangia kupitia mafuta na kadhalika. Kwa hiyo, naomba sana, kama Wakandarasi wako site na wanafanya kazi, basi walipwe kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Maji, ni msikivu na anajitahidi kufanya kazi vizuri, lakini tunajua kabisa kwamba matatizo yapo kwa Watendaji, lakini kwake kama Waziri na Naibu wake wanafanya kazi vizuri mpaka wanajitwisha na ndoo. Hii ni dalili kwamba kazi wanafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la maji ya Njombe Mjini. Mradi wa maji Njombe Mjini leo hii nasimama hapa Bungeni kwa mara ya tatu na kila bajeti inapokuja ya mwaka wanataja mradi wa Njombe Mjini tutapata maji kutoka Mto Hagafilo, lakini mradi ule haujatekelezwa mpaka leo. Tumeambiwa upo kwenye miradi ya miji 17, tunataka tuambiwe safari hii shida ni nini? Vinginevyo, tuambiwe kabisa kwamba mradi ule haupo ama upo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona kabisa kwamba iko miradi mikubwa katika mikoa mingine inatekelezwa na watu wanapata maji, lakini sisi pale Njombe maji yapo kilometa tisa yanatakiwa yafike katikati ya mji, tunashindwa kuyapata yale maji, kila siku tunaambiwa fedha ipo, tutafanyiwa lakini hatufanyiwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la afya. Naipongeza sana Serikali kwa kazi nzuri inayofanya. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais, sisi katika Jimbo la Njombe Mjini tumepewa shilingi milioni 500, tunajenga Kituo cha Afya pale Ihalula, lakini pamoja na ujenzi huo wa Kituo cha Afya, wananchi kwa kushirikiana na Halmashauri wanajenga kituo kizuri sana cha afya katika Kata ya Makoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Makoo, Kata ya Ihalula na Kata ya Utalengoro ni Kata ambazo ziko mbali sana na mjini. Tunaomba, tutakapokuwa tumekamilisha kazi hizi, basi tupewe magari ya wagonjwa, lakini tupewe Waganga wa kutosha katika vituo hivi vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, iko Hospitali ya Mkoa ambayo inajengwa. Naishukuru sana Serikali kwa kutujengea Hospitali ya Mkoa. Mheshimiwa Waziri Mkuu alifika, aliiona ile hospitali nzuri kabisa inayojengwa pale, lakini hospitali ile bado haijakamilika. Kwa sasa tunatumia Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, ndiyo imechukuliwa kama Hospitali ya Mkoa, lakini ina upungufu mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chumba cha upasuaji, wagonjwa wa aina zote wanapasuliwa chumba hicho hicho. Hebu niambie, huku unapasua mtu labda amevunjika mguu halafu kuna dharura ya mama mjamzito, unafanyaje? Unamtoa huyu mgonjwa unayempasua mguu umwingize mama mjamzito? Kwa hiyo, tunaomba pale Hospitali ya Kibena, tujengewe angalau theatre ya ziada ili kusudi angalau tuweze kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ndiye Mbunge wa watu wenye UKIMWI. Naiomba sana Serikali, kama sisi Njombe tuna UKIMWI na tumekuwa tukitangazwa kwamba hata data zetu ziko juu sana, basi tuhudumiwe. Huduma tunayoiomba, kwanza kabisa hatuna mashine ya kupima virusi vya UKIMWI (viral load). Sisi ndio tunaoonekana kwamba ndio waathirika wa kwanza, lakini inabidi tubebe sampuli za damu tupeleke Mbeya au tupeleke Iringa kwa ajili ya kupima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Njombe tupewe mashine hiyo ya kupima viral load ili tupime pale Njombe. Vile vile tupewe dawa kwa ajili ya magonjwa nyemelezi. Kama kweli Serikali inatutambua sisi kweli ni waathirika wa kwanza katika nchi hii kwa maradhi ya UKIMWI, basi tupewe dawa za kutosha za magonjwa nyemelezi na vitendanishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine unaenda kufanya vipimo unaambiwa vitendanishi hakuna. MSD hawatoi vitendanishi, vitendanishi wanatakiwa kutoa Wizara ya Afya na Wizara ya Afya inachelewa kutoa. Linapokuja suala la kugawa Waganga, sisi tunaoumwa zaidi, tupewe zaidi Waganga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya sana tupo mjini, tunaambiwa ah, Hizi Halmashauri za Mjini tusiwape Waganga wa kutosha, lakini sisi tunaomba mtambue kwamba sisi ni wagonjwa zaidi na tunakiri hilo na tunaomba mtusaidie. Msiendelee kututangaza tu kwamba sisi ni wagonjwa zaidi, lakini hamtusaidii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Njombe Mjini hakuna hata kijiji kimoja ambacho umeme wa REA umewaka. Wakandarasi wanakuja, wanaulizia wanaondoka. Naomba sana, najua ndugu yangu Waziri wa Nishati yuko makini na tunawasiliana naye kwa karibu. Hebu awasimamie hawa watu wafanye ile kazi kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la elimu. Hapa nazungumzia habari ya mikopo ya elimu ya juu. Mikopo ya elimu ya juu inanyanyasa wanafunzi. Anakopeshwa mwanafunzi mwaka wa kwanza, mwaka wa pili hakopeshwi, atapata wapi fedha ya kuendelea kujisomesha? Matokeo yake wanaanza kuzurura mitaani, wanaomba misaada. Mara waje kwa Waheshimiwa Wabunge, mara waende wapi. Kwa hiyo, naomba Bodi ya Mikopo ikimkopesha mwanafunzi mkopo mwaka wa kwanza, ihakikishe kwamba huyo mwanafunzi anakwenda naye mpaka mwaka wa nne. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu bila malipo ni zuri sana na linawasaidia sana wananchi huko vijijini na wananchi wote kwa ujumla, lakini tatizo lake kubwa ni kwamba elimu bila malipo ingewekewa kiwango maalum kwamba kiwango cha chini kabisa ambacho Serikali itatoa kwa shule ni kiasi fulani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kuna shule ambazo zina wanafunzi wachache. Kuna shule zina wanafunzi 150. Kwa hiyo, ukichukua ile namba ya wanafunzi na kutoa ile fedha ya Serikali, unajikuta kwamba fedha ya matengenezo na michezo haipatikani pale shuleni. Kwa hiyo, naomba sana kuwe na angalau kiwango cha chini ambacho kinaanzia angalau kuweza kulipia zile gharama za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile liko suala la elimu msingi. Elimu msingi, watoto sasa hivi wako darasa la nne na watoto hawa kila nikisimama hapa wanasema kwamba itafika mahali tutakuwa na form one mbili; tutakuwa na form one waliosoma miaka saba, lakini tutakuwa na form one waliosoma miaka sita. Je, maandalizi yetu yakoje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile suala la kuandaa Walimu kwa ajili ya elimu msingi limekwama. Ilikuwepo NACTE na NECTA, sasa zimeingia kwenye ushindani, kwamba Mabaraza haya mawili ya Mitihani yanavutana jinsi ya kutoa elimu kwa Walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali itoe maamuzi, kama tuliamua kwamba Taasisi ya Elimu ya Ufundi wajibu wake ni kusimamia mitihani yote ya ufundi ikiwemo ya Majeshi, Polisi na kadhalika, basi isimamie. Isirudi tena Wizara ya Elimu ikatoa mitihani mingine ikairudisha Baraza la Mitihani. Huku ni kuleta mkanganyiko na kuwavuruga Watendaji. Vilevile wapo wawekezaji katika masuala ya elimu, nao wanapata shida sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la Polisi. Nimetembelea Gereza la Njombe pale mjini. Pale kuna mahabusu wana miaka sita, saba mpaka kumi wanalalamikia suala la Polisi kwamba upelelezi unachelewa. Naomba sana, wanaotuhumiwa kwa mauaji upelelezi ukamilike ili kusudi kesi zao ziweze kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile liko suala la Mahakama. Mahabusu wa Gereza la Njombe wanailalamikia sana Mahakama. Moja, Njombe hatuna Mahakama Kuu, inakuja kwa vikao. Ikikaa kikao Njombe, haimalizi kesi, matokeo yake mahabusu wamelundikana sana katika Mahakama ya Njombe na wanasababisha ile mahabusu ionekane ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama inapokuwa haifanyi vikao na ikakamilisha zile kesi, ina maana inasababisha mlundikano wa mahabusu pale Magereza, matokeo yake kunakuwa na watuhumiwa wengi sana, halafu Gereza linaonekana ni dogo. Kwa hiyo, naomba sana, Idara ya Mahakama, namwona Mwanasheria Mkuu yuko hapa, tuone, tupeleke Mahakama Kuu Njombe ili kusudi Vikao vya Mahakama Kuu vifanyike Njombe. Kwa sababu Mheshimiwa Rais ameshawadhihirishia Watanzania kwamba fedha katika nchi hii siyo tatizo. Kwa hiyo, naomba sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la mawakala wa pembejeo. Mawakala wa pembejeo waliosambaza mbolea mwaka 2015/2016 wamepekuliwa mara nane. Hesabu zao zimepitiwa mara nane, lakini hakuna Wakala hata mmoja aliyepewa jibu. Jamani, huu siyo uungwana. Kama watu hawa wamepekuliwa hivi, wapewe majibu.

(Hapa kengele ililiakuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)