Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa sana anayoifanya ya kutekeleza miradi mikubwa katika Taifa letu. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ya kusimamia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapainduzi. Niwapongeze kwa dhati Mawaziri wale ambao wamefanya kazi kwa nia njema ya kulisaidia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza kwa sababu tuna miradi ambayo imeanza kutekelezwa kwenye maeneo ya Mkoa wetu. Tuna miradi ya maji ambayo imetekelezwa kwa kiwango kikubwa, miradi ya afya, miradi ya elimu, miradi ya umeme vijijini, miradi ya barabara kwenye maeneo ya Mkoa wa Rukwa, Mkoa wa Katavi, Mkoa wa Kigoma na Mkoa wa Tabora. Pale Serikali inapofanya vizuri tuna haki ya kuipongeza na pale ambapo pana changamoto tutaishauri Serikali ili iweze kutusaidia kwenye maeneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilayani kwangu nina miradi ya maji ambayo imeshaanza kutekelezwa, miradi mikubwa ya Kijiji cha Majarida, Kijiji cha Igagala, wananchi wanapata maji, Kijiji cha Ikola wana miradi mikubwa ya maji ambayo imetekelezwa. Nampongeza sana Waziri mwenye dhamana kwa jitihada ambazo anazifanya kuwatendea haki wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ipo miradi ya maji ambayo inatekelezwa Vijiji vya Mwese, Kamjela, Kabungu, hiyo yote ni miradi ambayo inatekelezwa na tuna visima 20 ambavyo vinachimbwa kwa ajili ya kuwapa huduma ya maji. Kwa hiyo tunaipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna miradi ya afya, tunavyo vituo vya afya cha Karema, Mwese, Mishamo, Serikali imetoa fedha kwenye vituo vya afya vya Mwese na Mishamo karibu zaidi ya shilingi milioni 800. Tuna matumaini makubwa sana kwamba Serikali itaendelea kusaidia kwenye sekta hii ili vituo hivi viweze kukamilika hasa kile kituo cha Mwese ambacho kinahitaji fedha kwa ajili ya kukamilisha ule mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna miradi ya elimu ambayo inatekelezwa, kuna ujenzi wa shule za msingi, ujenzi wa shule za sekondari, karibu kila sehemu shule zinajengwa kwa kutegemea nguvu za wananchi na Serikali yenyewe pale ambapo panahitajika kutoa huduma hiyo. Tunawapongeza na tunaiomba Serikali kwenye miradi hiyo iweze kuongeza nguvu kuwasaidia wananchi kwa sababu wengi wamejitokeza kujenga shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa ya kipekee kwenye miradi, hasa ya elimu, nimpongeze sana Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika kwa jitihada anazofanya za kusimamia utekelezaji. Pia nimpongeze Mkuu wa Mkoa kwa kulinda amani na usimamizi mkubwa wa miradi mingi inayotekelezwa Mkoa wa Katavi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo changamoto ambazo tunaiomba Serikali iweze kuzisimamia. Changamoto ya kwanza tunamwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu aingilie kati mgogoro wa Mradi wa Umeme Vijijini (REA) ambao unaunganisha Mkoa wa Katavi na Mkoa wa Kigoma. Kwa nini tunamwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu, miradi ya REA imesimama kwenye Mikoa ya Kigoma na Katavi kwa sababu ya mgogoro ambao upo, watu walioomba tenda wamegombana na wakashtakiana wakapelekwa Mahakamani, kiasi kwamba sasa ule mradi umesimama, REA Awamu ya Tatu karibu sehemu nyingi nchini inatekelezwa, kwenye mikoa hii hakuna kilichotekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu aliingilie hili jambo ili wananchi wa mikoa hii miwili waweze kuepukana na mgogoro ambao kwao wao hauna manufaa, tunaomba Serikali iingilie ili tupate huduma ya umeme vijijini kwa vijiji vya mikoa hiyo miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana Serikali iongeze fedha za Mfuko wa Barabara. Fedha za Mfuko huu zikiongezwa zitasaidia sana kuimarisha ujenzi wa barabara za vijijini na mijini. Mfuko wa sasa ambao upo una fedha kidogo sana na karibu wananchi wengi wa nchi nzima wanategemea sana fedha hizi ziweze kuwasaidia kuimarisha miundombinu ya barabara. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali iongeze fedha kwenye Mfuko wa Barabara ili barabara za vijijini, miradi ya barabara za mijini ziweze kuimarika na zifanye kazi vizuri kwa sababu huko ndiko kuna watu wengi wanaozalisha na wanahitaji huduma hii ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunaomba Serikali iongeze fedha kwa ajili ya kupeleka kwenye miradi ya ujenzi hasa kwenye Wilaya ambazo ni mpya. Mkoa wa Katavi ni Mkoa mpya na una Wilaya mpya ya Tanganyika na bahati nzuri Mheshimiwa Waziri Mkuu alifika kwenye maeneo hayo, anajua changamoto zilizopo. Tunahitaji fedha zipelekwe zikajenge Makao Makuu ya Wilaya, nyumba za watumishi, hospitali ya Wilaya na Hospitali ya Mkoa wa Katavi. Haya maeneo ni ya muhimu sana kwa ajili ya kuimarisha shughuli za kiutawala lakini vilevile kuimarisha shughuli za huduma za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu katika jitihada za kufufua miradi ya kilimo, hasa kwenye mazao ya pamba na tumbaku. Ametoa msukumo mkubwa sana, tunampongeza, lakini yapo mambo ambayo yanahitajika kuyafanyia kazi ili kwenda sambamba na msukumo ambao kautoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tunaomba Serikali inapokuwa inasukuma mazao haya ihakikishe inatengeneza mfumo mzuri wa kupeleka pembejeo. Pembejeo mwaka huu wakulima hawakuzipata kwa wakati, kuna baadhi ya maeneo wamepata hasara kwa sababu hawakupata pembejeo ambazo zilihitaji kuzalisha kwa wakati. Kwa hiyo, tunaomba usimamizi kwenye eneo hili uwe mkubwa sana ili tuweze kupata mazao ambayo yatawasaidia wananchi, hasa wakulima na vilevile kusaidia kipato cha Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye sekta hii ya kilimo bado suala zima la masoko linahitaji ufuatiliaji wa hali ya juu. Wananchi wamelima pamba kwa wingi, tunaiomba sana Serikali wanapolima wahakikishe wanunuzi wa mazao haya wanakuwa wamejengewa mazingira ambayo
yatawafikia wakulima kwa wakati. Naomba kwenye jambo hili tulifanyie umuhimu sana kwa sababu jitihada ambazo amezionesha Waziri Mkuu za kuhimiza mazao ya pamba, tumbaku na korosho zinaweza zikafikia mahali ambapo hazitakuwa na tija pale ambapo wakulima watakosa masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo ni kuhakikisha wanapata pembejeo za madawa ambayo yanahitaji kuhudumia mazao haya ambayo wananchi wamepewa fursa na wamehimizwa wayalime. Bila masoko tutalima mazao mbalimbali lakini hayatakwenda mahali popote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kwenye zao la tumbaku, mfumo wa zao la tumbaku uko tofauti sana na mazao mengine. Tunaiomba sana Serikali ihakikishe inawashirikisha wadau kwa ujumla ili wajue changamoto ya lile zao lakini tuhakikishe tunawajengea mazingira ya masoko yenye uhakika. Bila kutafuta masoko na bila kusaidia Serikali kuingilia kati, zao la tumbaku linaweza likapotea na linaweza lisitoe tija kwa wananchi, tunaomba sana Serikali iyafanye hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu miradi ya umwagiliaji. Kwenye eneo hili bado utekelezaji ni mdogo sana. Tunaiomba sana Serikali na tunamwomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu aangalie au aunde Tume itakayosaidia kuangalia miradi mingi ya umwagiliaji ambayo kimsingi haijafanya kazi na haijaonekana kabisa. Serikali imetumia fedha nyingi kwa ajili ya miradi hii ambayo haijaonekana na ufanisi wake ni mdogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya hakuna mradi wa umwagiliaji ambao ulisimamiwa vizuri, hata Halmashauri zenyewe hawakushirikishwa, ni miradi ambayo ilikuwa inatoka huku juu inaenda moja kwa moja…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja.