Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Hassan Selemani Kaunje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. HASSAN S. KAUNJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii kwa mara ya kwanza kuchangia katika Bunge hili, lakini nichukue dakika chache kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini vilevile kumpongeza Spika na Naibu Spika kwa ushindi wao, pamoja na wewe mwenyekiti kwa kushinda kuwa Mwenyekiti wa Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa nafasi ya kipekee, nimpongeze au niwapongeze wote walioteuliwa kuwa Mawaziri katika Baraza la Mawaziri katika Serikali hii ya Awamu ya Tano; lakini na wao niwatume vilevile wafikishe salamu kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba Mheshimiwa Kaunje, Mbunge wa Lindi anahitaji kupongezwa kwa sababu naye alinituma kazi mbili alipokuja kwenye kampeni Lindi na nilizifanya kwa ukamilifu. Kazi ya kwanza ilikuwa ni kuhakikisha natumbua jipu la Mbunge wa Upinzani katika eneo la Lindi Mjini na nilimwondoa. (Makofi/Vigelegele)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhakikisha kwamba yeye anapata kura za kutosha na hilo nilihakikisha. Hivyo basi, hana budi naye kunipongeza kwa kazi hizo mbili nilizofanya kwa niaba yake. (Makofi)
MHE. HASSAN S. KAUNJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina machache tu ya kuchangia.
Kwanza nitachangia yale yanayohusiana na Jimbo langu, halafu kwa ujumla nitakuja tu kuzungumzia biashara ya korosho. Nitamwomba ndugu yangu, Mheshimiwa Mwigulu atakapokuja kufanya majumuisho aniambie kwa nini Lindi Mjini kama Jimbo na Halmashauri ya Manispaa ya Lindi inakosa fungu la maendeleo ya kilimo wakati wakulima wapo katika Manispaa ya Lindi Mjini? (Makofi)
Pili, aniambie mkakati alionao wa kuwasaidia wananchi wa Kata ya Ng‟apa na Tandangongolo ambao wanazalisha nazi nyingi zinazoliwa Dar es Salaam tangu dunia ilipoanza mpaka leo lakini kiwanda cha kuwasaidia hakipo, na yeye ana mpango gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nitamwomba atueleze Wanalindi ambao hatuli nyama ya ng‟ombe wala mbuzi, kwa nini Ranchi ya Taifa ya Ngongo ilifungwa na kama ana mpango wowote wa kuianzisha tena ili sisi ambao tunakosa nyama na kupata maumbo mafupi kama haya, tuweze kupata na warefu watokee Lindi? (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, anieleze vile vile ana mpango gani wa kuwasaidia wakulima wa mwani ambao wanapatikana katika Ukanda wa Pwani ya Lindi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee azungumzie kiwanda kilichopo Lindi cha ubanguaji wa korosho ambacho ni kikubwa, atakavyoweza kusaidia kukifungua na wananchi wa Lindi waweze kupata ajira.
Nimkumbushe vilevile eneo la Lindi Manispaa lina ukanda wa bahari wenye urefu wa kilometa 104, lakini ukienda kwenye mapato ya Manispaa ya Lindi Mjini, kutokana na ushauri mbovu au maendeleo hafifu yanayotokana na Idara ya Uvuvi mapato kwa mwaka hayazidi shilingi milioni nne. Kwa maana ya kwamba kwa kila siku mapato ya Bahari ya Lindi hayazidi shilingi 1,000 katika kuchangia pato la Manispaa hiyo. Sasa anishawishi kwa nini tuendelee kubaki na wataalam wake wa uvuvi waliopo pale na namna gani asiweze kuwaondoa akatuletea wengine ambao waka-brand, wakautumia ukanda ule kuweza kuleta mapato katika eneo la Manispaa ya Lindi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumaliza hayo, nichangie sasa kwenye eneo la zao la korosho. Kama ulivyomwomba Mbunge aliyekaa aeleze interest, na mimi nataka ku-declare interest kwamba pamoja na kuzaliwa Lindi kwenye zao la korosho lakini nimefanya kazi katika sekta ya korosho kwa miaka yote kabla ya kuja Bungeni. Kwa hiyo, nataka tu nieleze yale ninayoyafahamu ambayo yatachangia ku-boost hii sekta ya korosho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kitu kinachoitwa Mfuko wa Maendeleo ya Tasnia ya Korosho (CIDTF). Kama walivyoeleza Wabunge wengine Mfuko huu ndiyo ule wenye mamlaka ya matumizi ya almost shilingi bilioni 70 zilizotajwa na Wabunge waliopita. Ukichukulia matumizi ya fedha hizi kwa kila mwaka, unaweza ukakuta zinazotumika haziwezi kuzidi bilioni 30 kurudi kwa wakulima kwa maana ya pembejeo na mambo mengine. Ukija katika mipango yao, kila siku wameendelea kupanga mipango ya kujenga viwanda vya kuendeleza tasnia ya korosho au kubangua korosho zinazopatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu nini? Nataka niwashauri, tunapozungumzia maendeleo ya tasnia ya korosho na wakulima wa korosho na wananchi wanaotegemea korosho, haimaanishi tu yanatokana na uwepo wa pembejeo na ubanguaji wa korosho. Wakulima wale wataona korosho ina tija pindi tu korosho ile itakapoweza kuwasaidia kutibiwa, kupata elimu, kuondokana na madhila ya benki, kwa maana ya kwamba uwepo wa fedha wa kuweza kuwakopesha kipindi cha ununuzi, lakini pale inapotokea anguko la korosho, basi fedha ziwepo za kuweza kufidia wakulima. Mambo haya yote yanawezekana katika suala la korosho kwa sababu fedha hizo zipo na vitu hivyo vinaweza kufanyika. Kwa sababu katika Tanzania hili ndilo zao lililo huru linaloweza kujiendesha lenyewe kutokana na fedha zinazopatikana. (Makofi)
Kwa hiyo, nilikuwa ninamwomba Mheshimiwa Waziri, pamoja na mambo mazuri yanayofanywa na CIDTF hebu awaelekeze wapanue wigo wa maendeleo ya zao la korosho na wakulima wa korosho, haiishii tu kwa kuwapelekea pembejeo na mpango usiokwisha wa kujenga viwanda; waangalie maeneo mengine ambayo yanaweza yakawasaidia. Wakulima wa korosho hawazidi 500,000. Kwa mwaka wakiamua tu kuwachangia katika Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, shilingi bilioni tano wananchi wote wanaolima zao la korosho watatibiwa katika familia zao. Inawezekana katika shilingi bilioni 70 wanazochukua. Mambo haya tunapaswa tuwashauri na wayafanye kwa ajili ya maendeleo ya zao la korosho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, nilipenda tu nishauri katika sekta ya ushirika. Tumekuwa tunalalamika Wabunge hapa kuhusu ushirika, lakini tujiulize dhana ya ushirika na wanaushirika ni nani ili nao tuwaombe msaada?
Mwanachama wa Chama cha Msingi kilichopo Lindi analeta malalamiko kwa Mheshimiwa Waziri amsaidie kuvunja Bodi ya Chama cha Ushirika, lakini Chama kile cha Ushirika amekiunda yeye katika Mkutano Mkuu. Kwa nini wanachama hawa wasiweze kuziondoa bodi zao? Kwa hiyo, ni lazima tuwaelimishe. Kuna vitu vingine au kuna majipu mengine tunataka watatue wengine wakati sisi wenyewe tuna uwezo wa kuyatatua kule chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe wito kwa wakulima, nitoe wito kwa wanaushirika katika vyama vyao kujaribu kutatua matatizo yao bila kusubiri Serikali ije kufanya kwa niaba yao kwa sababu watu waliyokuwepo katika Uongozi ule wamewaweka kwa matakwa yao wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza haya, nakushukuru kwa kuniona kwa mara ya kwanza kuweza kuchangia. Ndiyo salamu za Lindi zimeanza na ninakuomba kila utakapokalia Kiti hicho usinisahau mimi kuniita na kuweza kuchangia katika Bunge hili. Naunga mkono hoja. Ahsante sana.