Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hotuba hii ya Waziri Mkuu. Awali ya yote, naomba nitoe ombi kwa Serikali ya CCM ya Awamu ya Tano na ombi hili naomba Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Lindi na Mtwara waniunge mkono kwa sababu hii ni hoja yetu sote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Serikali ya Awamu ya Tano, naomba sana haka kasungura kadogo tulikonako basi tukagawanye sawa sawa, kwa sababu sisi sote tunachangia kwenye haka kasungura. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini naleta hili ombi? Kwa sababu ukipitia bajeti, hii ni bajeti ya tatu, bado Mkoa wa Lindi na Mtwara kwenye bajeti hii tunapata hasa kwenye pesa za miradi wa maendeleo kidogo sana. Kwa ushahidi jana dada yangu Mheshimiwa Hawa Ghasia kalisema hili, kwamba bajeti iliyokwenda kwenye Bandari ya Mtwara ni ndogo. Siyo bandari tu, yeye ameongea hivi kwa busara tu kwa sababu ya mazingira aliyonayo, lakini ukweli ni kwamba bajeti tunayopewa Mikoa hii miwili ni ya shida sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu ukiangalia, juzi tu hapa kuna mradi umetokea wa ukuzaji wa maliasili Ukanda wa Kusini, lakini ukanda wenyewe wa Kusini uliotajwa na kupelekwa zile pesa ni Morogoro, Mbeya, Iringa, Liwale, Lindi haipo, Mtwara haipo na pesa zimetoka. Ni jambo la kushangaza sana! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu Mheshimiwa Masala amesema asubuhi hii, kuna barabara ya Masasi – Nachingwea – Nanganga, ile barabara upembuzi yakinifu umeisha mwaka 2015 lakini mpaka leo pesa zinatafutwa. Ipo miradi kwenye nchi hii imefanyiwa upembuzi yakinifu mwaka 2017/2018 na sasa wakandarasi wako kazini. Suala hili nimewahi kuliuliza, hivi kuna tatizo gani? Kuna barabara nyingine utasikia zimejengwa na fedha za nje, kwa nini hizi bararaba zetu za Liwale, Lindi, Mtwara hazijawahi kupata wakandarasi wa nje? Suala hili ni zito sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuongezea hilo hilo sisi Mwenyezi Mungu alitujalia tukapata gesi asili Mtwara, nafikiri uletaji wa gesi ile Dar es Salaam palitokea vita sana ya maneno na migomo mbalimbali. Leo hii mkoa ambao una tatizo la umeme; kwa siku unakatika zaidi ya mara kumi au mara tano au mara sita ni Mkoa wa Lindi na Mtwara. Kulikoni Mkoa wa Lindi na Mtwara? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ushahidi zaidi, hata Kamati zako za Bunge zinazotembelea kukagua miradi iliyopewa fedha za Serikali, uendaji wa Mkoa wa Lindi na Mtwara ni mdogo sana na wakienda, basi walikuwa wamekusudia kwenda Songea, wakapitia Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Kamati ya Ulinzi na Usalama imeweza kwenda Mtwara na Lindi, ni kwa sababu tu ya matokeo yale ya Rufiji, inasemekana wale watu wamejificha Lindi na Mtwara, walikwenda kufanya tathimini hiyo kuona kuna nini, lakini siyo kufuata miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikatai kwamba hakuna miradi ya maendeleo inayokwenda, inakwenda lakini ni miradi midogo sana. Hakuna miradi mikubwa inayovutia Kamati yako ya Bunge kwenda kukagua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali ya Awamu ya Tano tusifanye hivyo. Sisi sote tunachangia kwenye pato la Taifa hili na tuna haki ya kufaidi matunda ya Taifa hili.

Vilevile nakuja kwenye upande wa elimu; upande wa elimu kwa kweli tunacheza, hatujaamua kuwekeza kwenye elimu. Kwa sababu kwa mujibu wa takwimu iliyotoka Hakielimu, wanasema walimu wanaokwenda madarasani kufundisha kwa ari ni asilimia 37. Ina maana wengine wote wanaokwenda ni kwa sababu wameajiriwa, ilimradi tu wanakwenda. Tatizo ni nini? Maslahi yao hayajatekelezwa. Walimu wanafanya migomo ya kimoyomoyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii katika kuboresha, tumeamua kuongeza tatizo lingine. Tumechukua walimu wa sekondari wakafundishe shule za msingi. Matatizo ya huko ni makubwa mno kuliko tunavyofikiria. Zoezi lile zimeendeshwa tofauti na Serikali mlivyopanga. Zoezi lile limeendeshwa kwa ubaguzi mkubwa na kwa uonevu mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nilikuwa naongea na Afisa Utumishi wa Wilaya yangu, namuuliza mbona kuna malalamiko makubwa sana kwenye hili zoezi? Akanambia hata mimi taarifa hiyo nilikuwa sina, Afisa Elimu amefanya jukumu hili bila kunijulisha. Kweli haya malalamiko ya Watumishi wa Idara ya Elimu hata kwangu yapo. Wameachwa walimu wenye Diploma wanaendelea kwenye shule ya sekondari, wamechukuliwa watu wa Degree wamepelekwa shule za msingi. Kilichofanyika ni watu kukomoana. Wametumia hii loophole kama Mwalimu Mkuu (Head Master) akiona kwamba ana matatizo na mwalimu fulani, anamhamisha anampeleka shule ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kule badala ya kuwa shule ya msingi ama kuinua elimu, tumekwenda kufanya kama kule ni jela. Jambo hili haliwezi kukubalika. Ombi langu, Serikali hebu mrudie hili zoezi mwone ni namna gani limetekelezwa kama nia yenu ilikuwa ni nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu vilevile nataka nizungumzie taasisi hii inayoitwa TARURA. Taasisi hii ya TARURA imeundwa kwa nia nzuri kama mnavyodai, lakini taasisi hii mpaka leo hii haieleweki mhimili wake ni upi? Sisi Wabunge hatuna nafasi ya kuihoji TARURA. Halmashauri, Madiwani wetu hawana nafasi ya kuihoji TARURA. Juzi nimeuliza swali hapa Mheshimiwa Waziri anasema, TARURA watapeleka ripoti yao kwenye DCC. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, hebu tujiulize, ni wangapi tunahudhuria hizo DCC? DCC kwa mwaka zinakaa mara ngapi? Pamoja na kwamba kwa mujibu wa sheria wanatakiwa wakae mara tatu, lakini sina hakika kama kuna Wilaya yoyote ile inayoweza kutimiza hiyo azima ya mara tatu kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba hawa watu wako huru, wanajifanyia mambo wavyotaka. Kuna u-specialist gani wa Meneja wa TARURA wa Wilaya ambaye anamzidi Mhandisi wa Maji, Afisa Elimu na Afisa Maliasili au Afisa Ustawi wa Jamii? Maana hawa wote tunakuwa nao kwenye Baraza la Madiwani. Kwa nini huyu Meneja wa TARURA asiingie kwenye Baraza la Madiwani, ukizingatia hizo barabara anazozihudumia ziko chini ya Halmashauri. Vipaumbele vya barabara gani ijengwe kabla ya ipi, sisi Halmashauri ndio tunajua. Sasa nataka kufahamu, Serikali ije na majibu, kwa nini kuna u-specialist wa TARURA isiende kwenye Halmashauri zetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nije kwenye uwekezaji; mnaongelea mambo ya uwekezaji, lakini uwekezaji huo una matatizo makubwa sana hata kwa wawekezaji wadogo. Hizi mamlaka za usimamizi zimekuwa ni nyingi sana na tumekuwa tukilia hapa mara kwa mara kwamba kama inawezekana, hizi taasisi nyingine ziunganishwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitaka kujua tatizo la uwekezaji nchi hii hasa kwa wawekezaji wadogo, hebu fungua kiwanda kidogo tu cha kusindika tu sembe, atakuja NEMC, atakuja TFDA, atakuja TBS watakuja sijui TRA, watakuja sijui watu wa OSHA, ni vurugu mtindo mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu sasa ili uweze kuwa mwaminifu ukatekeleza hayo yote, basi kama siyo miezi miwili au mitatu itakuchukua kupitia kwenye hizi taasisi. Kwa sababu ingewezekana hizi taasisi zote zingekaa pamoja au kwenye ile fomu moja ambayo utajaza hawa watu ukawakuta kwenye sehemu moja wakakujazia hizo fomu wakaku-verify ukafanya hiyo kazi, lakini hapana. Leo utakwenda taasisi ya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)