Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu.

Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametupa nguvu na afya kuwepo mahali hapa, lakini nichukue pia nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri zinazofanyika. Ndugu zangu Watanzania wanaona yale yanayofanyika. Kwa hiyo, ninampongeza Mheshimiwa Rais, anafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninajua kipindi hiki kama Watanzania tuko kwenye vita na ni vita ya kiuchumi. Vita ya kiuchumi kuna watu ambao watatu-support, lakini wapo watu wengine ambao watabeza, lakini kitu cha muhimu sisi tuangalie ni wapi tunakoenda na lile ambalo tumelikusudia. Hao wapiga debe tuachane nao, siku zote nilishawahi kusema hapa Bungeni, mara nyingi wapiga debe huwa sio wasafiri. Ukiwa kwenye kituo cha mabasi utaona watu wanasema twende, twende lakini mwisho wa kusafiri hawaendi. Hao wapiga debe tuachane nao tusonge mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii niongelee kwanza upande wa afya. Niipongeze Serikali yangu, Kyerwa tulikuwa hatuna kituo cha afya hata kimoja, lakini sasa hivi tuna kituo cha afya kimekamilika, kiko vizuri na niishukuru Serikali wamenipa shilingi milioni 700 kwa ajili ya kuboresha kituo cha Mlongo. Kwa hiyo, nina kila sababu ya kupongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali, bado tuna upungufu wa watumishi na ukilinganisha kwa mfano Wilaya yangu ya Kyerwa bado tunahitaji zaidi huduma za afya. Nina Kata 24, naomba sana Serikali kwenye mgao huu ambao mnaenda kugawa Hospitali za Wilaya 67, naomba na Wilaya yangu ya Kyerwa ipewe mgao kwa sababu tunahitaji sana huduma ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende upande wa maji, wengine tunapopongeza wanasema tunajipendekeza lakini mambo kama yamefanyika lazima tupongeze. Kwenye Wilaya yangu ya Kyerwa nimepewa zaidi ya bilioni mbili na milioni 900. Sasa hivi tumeweza kuboresha miradi midogo kwa mfano mradi wa Kaishori, Rutunguru na Isingilo, mradi wa Mabira, hii ni miradi ambayo itawahudumia wananchi lakini kwa muda mfupi tumeweza kufanya usanifu wa mradi mkubwa ambao huu mradi utaweza kuwahudumia wananchi wa Kata 15 kati ya 24.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe sana Serikali bado tuna uhitaji sana wa huduma ya maji. Kama walivyoshauri Waheshimiwa Wabunge wenzangu, niiombe sana Serikali ile shilingi 50 ambayo tumeomba iongezwe bado uhitaji wa maji kwa wananchi wetu ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe sana Serikali ilizingatie na iweze kuliongeza. Niiombe sana Serikali, kwenye mradi wetu ambao tumeshafanyia usanifu tutakapomaliza kutangaza tender ninaamini Serikali yetu ni sikivu tutapatiwa pesa kwa ajili ya kukamilisha huu mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la TARURA, Waheshimiwa Wabunge, tulikuwa tunaongea sana hapa Bungeni tunasema miradi inaharibika kwenye Halmashauri, haisimamiwi vizuri. Serikali imeleta chombo kizuri ambacho ni TARURA. Mimi niwaeleze ukweli Waheshimiwa Wabunge, Mbunge una uwezo wa kukaa na yule Meneja wa TARURA mkajadiliana miradi ambayo unayo kwenye jimbo lako, lakini ninashangaa leo Wabunge ninyi ndiyo mnashauri irudishwe kwenye Halmashauri, kwa nini mlikuwa mnapiga kelele? Hili niiombe Serikali, ushauri mwingine tusiusikilize. TARURA wameanza vizuri, kwa muda mfupi kwenye jimbo langu wameonesha jambo kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo niishauri Serikali tuongeze, badala ya asilimia 70 kwenye TANROADs tufanye nusu kwa nusu au kama ikishindikana tufanye asilimia 45 kwa 55 kwa sababu barabara nyingi ziko vijijini na wazalishaji wakubwa wako vijijini. Kwa hiyo, niombe sana Serikali hili ilizingatie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la umeme. Tunahitaji umeme, kule kwetu Kyerwa bado kabisa, kwa hiyo, niombe sana waendelee kuongeza uwezo wa kuzalisha umeme ili wananchi wetu wapatiwe umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nilizungumzie ni suala la kahawa. Ninaamini Serikali yetu ina nia njema kwa ajili ya kuwakomboa wakulima hao ambao wameachwa muda mrefu. Wakulima hawa walikuwa wanauza kahawa kwa butura ambayo butura wanauza 20,000 na yule anayenunua anakuja kupata zaidi ya 100,000. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali, ilisimamie hili kwa karibu kwa sababu hii na yenyewe ni kama vita. Wale waliokuwa wananunua na wao wangetamani hili la Serikali lisifanikiwe. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ambalo niishauri Serikali kama walivyochangia Wabunge wengine, hawa wananchi walishazoea kahawa kabla haijakomaa wanaweza kuuza butura sasa kukomesha biashara ya butura, tuanzishe SACCOS ambazo zitaweza kuwahudumia hao wananchi kabla kahawa haijakomaa aweze kutatua matatizo yake. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali iweze kulizingatia tuweze kuwakomba wakulima ambao wameachw amuda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nishauri kwa upande wa kahawa. Kuna madeni ambayo walikuwa wanadaiwa hawa KDCU, KCU, haya madeni yasije yakahusishwa na wananchi wanapouza kahawa zao. Madeni watafute namna ya kuwalipa, lakini sio wananchi wanaenda kulipa madeni, wananchi hawakusababisha haya madeni. Kwa hiyo, kama Mbunge ambaye natoka Mkoa unaolima kahawa, suala hili lisije likahusishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nishauri Serikali katika zao hili la kahawa. Kama kuna uwezekano waajiri watu kuliko haya mambo ya kuchaguana. Ndiyo maana wanachagua hata watu wengine ambao hawana uwezo, mwisho wa siku wanakuja kuharibu. Kwa kuwa, Serikali ina nia ya dhati niiombe sana Serikali wawekwe waajiriwa ambao wana uwezo kama ni wahasibu, kama ni mameneja ambao wataweza kusimamia haya mazao yetu. (Makofi)

Mheshimiwa MWenyekiti, kitu kingine tuombe sana Serikali iwezeshe hivi vyama vya msingi kwa sababu sasa hivi hawana pesa na walikuwa hawajajiandaa ni kama wameshtukizwa. Sasa jamno ambalo wameshtukizwa leo unawaambia wanunue kahawa na huko kwenye mabenki wanadaiwa. Hii itakuwa ngumu na inaweza ikasababisha chuki kwa wananchi kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niendelee kuipongeza Serikali na niendelee kuwatia moyo. Serikali songeni mbele, kazi mnayoifanya ni kubwa, Watanzania wanaona na kwa muda mfupi kwa kweli mmeonesha mabadiliko makubwa. Watanzania wako wengi wanawaunga mkono. Hizi kelele tuachane nazo tusonge mbele. Ahsante.