Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Zainab Mndolwa Amir

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZAINAB M. AMIRI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naipongeza hotuba nzuri iliyotolewa na Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, afya, naipongeza Serikali, ila nashauri kutokana na Hospitali ya Rufaa Muhimbili iliyopo Mkoa wa Dar es Salaam kupokea wagonjwa kutoka mikoa yote ya Tanzania Bara na Visiwani na wengi wa wagonjwa hawana ndugu Mkoa wa Dar es Salaam hivyo, naishauri Serikali ijenge eneo maalum ambalo litawasaidia ndugu waletao wagonjwa wao kuweza kukaa na kutoa huduma za dharura ambazo wauguzi hawawezi kuzifanya na itasaidia ndugu wa mgonjwa kufuatilia maendeleo ya mgonjwa wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali itafute eneo lingine la kuhifadhia maiti katika hospitali ya Mkoa wa Morogoro maana chumba cha kuhifadhia maiti kipo karibu na Shule ya Sekondari Morogoro, hivyo kusababisha ndugu wa wafiwa wanapokuja kuchukua maiti wao hulia na kelele hizo za vilio zinasababisha wanafunzi waliopo madarasani kukosa usikivu wa kufuatilia masomo wawapo darasani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma za kiuchumi, barabara zote za lami nchini zilizojengwa chini ya kiwango, mfano barabara ya Chalinze hadi Mlandizi, zifanyiwe ukarabati ili kuepusha ajali za barabarani. Barabara zilizojengwa pembezoni mwa milima, mfano Milima ya Usambara katika Mkoa wa Tanga zijengewe pavements au uoto ambao utazuia mmomonyoko wa ardhi, hususan kipindi cha mvua ambayo uharibu barabara hizo na kutopitika kwa urahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba njia ya reli ya Dar es Salaam – Tanga ikarabatiwe ili iweze kupitika na kuweza kusaidia usafirishaji wa mizigo na abiria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kutafuta njia mbadala ya msongamano wa magari eneo la mizani, hususan Vigwaza Mkoa wa Pwani, ukizingatia magari ya abiria yanatembea kwa ratiba maalum hivyo, husababisha usumbufu na abiria pia, hupata usumbufu kwa kusafiri kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali iboreshe viwanja vya ndege. Mfano uwanja wa ndege uliopo Mkoa wa Morogoro wakati wa usiku haufanyi kazi kutokana na ukosefu wa taa uwanjani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta za uzalishaji; kilimo, wakulima wahamasishwe kulima mazao ambayo yatatumika kama malighafi katika viwanda vilivyopo nchini, mfano, kilimo cha alizeti, tumbaku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda, viwanda vipya vinavyojengwa vijengwe nje, mbali na makazi ya watu. Viwanda vinavyojengwa viwe ambavyo malighafi zake zinapatikana hapa nchini ili wakulima wetu wapate soko la kuuza bidhaa zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara, wafanyabiashara wakadiriwe na Mamlaka ya Mapato (TRA), kulingana na biashara wanayoifanya na si eneo wanalofanyia biashara. Mfano, maeneo ya Kariakoo katika Mkoa wa Dar es Salaam wafanyabiashara wanakadiriwa kutokana na eneo. Pia, wafanyabiashara wakati wanaanzisha biashara zao wapewe muda maalum (Grace Period) angalau wa miezi mitatu kisha ndio wafanyiwe makadirio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu; maslahi ya Walimu yaboreshwe ili wawe na utulivu wanapofundisha. Madarasa yaongezwe kuepuka msongamano wa wanafunzi katika shule zetu. Wanafunzi wapatiwe angalau mlo mmoja kwa siku wawapo shuleni.