Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naungana na Wabunge wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri ya mapitio na mwelekeo wa kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Bunge kwa Mwaka wa fedha wa 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mkuu wetu wa Nchi, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa juhudi kubwa anazozifanya katika kutuletea maendeleo ya kiuchumi nchini. Kufufua zana za uchumi wa viwanda, ununuzi wa ndege za usafiri kwa ajili ya Shirika letu la Ndege la Taifa (ATCL), kutekeleza kwa vitendo maamuzi ya Serikali ya kuhamisha Makao Makuu ya Serikali kuja Dodoma, kutekeleza ujenzi wa reli ya kisasa ya standard gauge, kutekeleza ujenzi wa barabara ya juu (flyovers) katika maeneo ya makutano ya barabara Jijini Dar es Salaam, kutekeleza ujenzi wa mradi mkubwa wa uzalishaji umeme wa Stiegler’s Gorge, ni mifano ya juhudi hizo za kujenga uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukuzaji ujuzi. Katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ameelezea umuhimu wa kukuza ujuzi wa nguvukazi tuliyonayo na kusema ni miongoni mwa ajenda muhimu za kisera. Naomba kupendekeza kwamba wataalam wastaafu wazalendo watumike katika kusambaza ujuzi na elimu kwa vijana wetu. Wapo Watanzania wengi wenye ujuzi mkubwa katika fani mbalimbali za uzalishaji uchumi na kadhalika ambao ni wastaafu ambao bado wana nguvu na uwezo mkubwa wa kushauri. Serikali iwatumie wastaafu wetu hawa pamoja na wataalam wengine ambao bado hawajastaafu, ili kuweza kupata matokeo ya haraka ya ukuzaji ujuzi na kuwajengea vijana wetu uwezo mkubwa (capacity building).

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sekta Binafsi. Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji uchumi. Suala hili ni muhimu sana kulisimamia na kuliendeleza kwa nia ya kujenga uchumi wa nchi yetu. Hata hivyo juhudi za mara kwa mara zifanyike na hatua kuchukuliwa za kuwawezesha wafanyabiashara Watanzania na wazalendo kunufaika na uchumi wa nchi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo. Serikali imekamilisha maandalizi ya awamu ya pili ya Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo. Bado uzalishaji katika kilimo ni wa kiwango cha chini ukizingatia ardhi kubwa inayofaa kwa kilimo cha kumwagilia, haitumiki. Nashauri katika maandalizi hayo iwe ni pamoja na kupanga mikakati ya kulima maeneo yote yanayolimika na kutafuta masoko ya nje na ndani kwa mazao yote yatakayolimwa na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, afya; Serikali imetoa fedha za kutekeleza ujenzi na ukamilishaji wa miundombinu ya vituo vya afya na maabara ya upasuaji kwa akinamama wanaojifungua. Jumla ya vituo vya afya 100 vimepatiwa jumla ya shilingi milioni mia saba, kila moja ikiwa shilingi milioni mia nne; ni kwa kazi za umaliziaji miundombinu na shilingi milioni mia tatu zinanunulia vifaa na madawa MSD. Nimeomba Serikali ijumuishe Vituo vya Afya vya Mvuha, Mtamba (Kisemu) na Tawa vilivyomo kwenye Jimbo la Morogoro Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.