Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake aliyoiwasilisha kwa umahiri mkubwa. Nataka nianze mchango wangu kwa kuiasa Serikali kuwa japo upatikanaji wa mapato siyo mzuri sana, lakini hata hicho kidogo kinachopatikana basi kuwe na mgawanyo wa haki, kwani Watanzania wote ni walipakodi wa nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikipitia bajeti zote za Awamu ya Tano. Mgawanyo wa fedha za maendeleo kwa mikoa ya Kusini, Lindi na Mtwara ni kidogo sana. Mikoa hii haina miradi mikubwa ya maendeleo. Jambo hili limekuwa ndiyo chanzo cha kudidimia uchumi wa mikoa hii, hata pale mikoa hii inapokuwa na miradi, basi miradi hiyo haipewi fedha kwa wakati. Mfano, mradi wa barabara ya Masasi – Nachingwea - Nanganga ambayo upembuzi wake ulikamilika tangu mwaka 2015, lakini hadi leo mradi huu haujapatiwa fedha, wakati miradi mingine mipya imekuwa ikipata fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kusisitiza hoja yangu ya mgawo wa fedha za maendeleo kwa Mikoa ya Kusini kwamba siyo wa kuridhisha, hata Kamati zako za Bunge zimekuwa hazifanyi ziara katika mikoa hiyo kwa kuwa haina miradi ya kwenda kukagua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Serikali kuhamia Dodoma ni kwa kuwa Dodoma ni katikati ya nchi yetu. Hivyo kuweka Makao Makuu hapa ni kuwezesha taasisi na wananchi kufika Makao Makuu ya nchi kiurahisi. Lengo hili halitakuwa na maana kwa wakazi wa Mikoa ya Lindi na Mtwara iwapo barabara ya kuunganisha Mkoa wa Lindi hadi Morogoro haitajengwa, kwani barabara hii ni muhimu sana kwa Mikoa ya Lindi na Mtwara ili kufika Dodoma kirahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Tano imekuwa haipeleki fedha za miradi kwenye Halmashauri zetu kwa masharti kwamba miradi hiyo ni lazima ianze kutekelezwa na Halmashauri husika. Utaratibu huu unaendelea kuziacha nyuma zile Halmashauri zenye mapato madogo ambazo hazina uwezo wa kuanzisha miradi mikubwa kama ujenzi wa Hospitali za Wilaya, majengo ya Mahakama za Wilaya na majengo ya Vituo vya Polisi vya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo naishauri Serikali kuangalia upya utaratibu usio wa haki. Mfano katika Jimbo langu la Liwale, hatuna majengo hayo yote niliyotaja hapo juu na Halmashauri haina uwezo wa kujenga majengo hayo. Kama ni lazima miradi hiyo ianzie ngazi ya Halmashauri, basi Wilaya ya Liwale haitakaa ipate majengo ya Hospitali, Mahakama na Kituo cha Polisi cha Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye majibu ya Waheshimiwa Mawaziri Bungeni. Kumekuwa na tabia ya baadhi ya Mawaziri kutoa majibu mepesi kwa Waheshimiwa Wabunge bila kuzingatia hali halisi ya mazingira ya swali. Jambo hili linafanya majibu haya baada ya muda yanaonesha Waziri alilidanganya Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wa majibu haya ni jibu la swali langu kuhusu ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya ya Liwale. Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana alinijibu, ujenzi huo utakamilika ifikapo mwaka 2018. Cha kushangaza, hata kwenye Randama ya Bajeti ya mwaka 2018/2019 mradi huu haumo. Je kujibu vile Mheshimiwa Waziri alikusudia nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie habari ya Utalii. Kumekuwepo na mradi wa kukuza Utalii Kanda ya Kusini. Cha kushangaza, mradi huu Mikoa ya Lindi na Mtwara haimo. Jambo hili haliwezi kuvumilika kwa wakazi wa mikoa hiyo, kwani ukiizungumzia Kusini juu ya utalii, huwezi kuiacha Hifadhi ya Selous ambayo kwa kiasi kikubwa iko Lindi. Iweje fedha zenye jina la kuendeleza Kusini zipelekwe Mbeya, Iringa na Morogoro, ukaiacha Mikoa ya Mtwara, Lindi na Pwani? Hii siyo sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kuendelea kuitenga Mikoa ya Kusini, hata pale Mungu anapoamua kuiinua mikoa hii. Mfano upatikanaji wa gesi ambako hadi leo hakujasaidia lolote kwani hadi leo Lindi na Mtwara ndiko kuna matatizo ya upatikanaji wa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuwa na uandikishaji mzuri kwa wanafunzi wa darasa la kwanza, lakini kiwango hiki hakina uwiano mzuri na wahitimu wa darasa la saba. Jambo hili linaashiria kuporomoka kwa elimu yetu, sababu kubwa ni Serikali kutokuwekeza kwa upande wa Walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikama ya Walimu wa Shule za Msingi ni mbaya sana. Mfano katika Halmashauri yangu kuna Shule za Ndapata, Kikulyungu, Norongopa. Shule hizi zina Walimu watatu kila shule. Jambo hili lipo nchi nzima. Tatizo la Walimu ni kubwa sana. Siyo hivyo tu, hata hawa Walimu wachache tulionao hatuwawekei mazingira bora ya kazi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti zinaonesha ni asilimia 39 tu ya Walimu wanaoingia madarasani na kufundisha kwa moyo au ari. Hivyo asilimia 61 wako kazini tu, kwani wamepoteza morali ya kazi, wana migomo ya kimoyomoyo. Kwa ujumla, Walimu wamekosa mtetezi. Watumishi wengi sasa Serikalini wamepoteza morali ya kazi na kubaki na manung’uniko moyoni mwao kwani mishahara yao ni midogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la TARURA, nashauri litolewe ufafanuzi, kwani haiko wazi kwamba fedha hizi za Serikali zinasimamiwa na Mamlaka gani? Kama ni Mhandisi wa Maji, Afisa Elimu, Afisa Kilimo, wote hawa wanawajibika kwa Madiwani. Kwa nini Meneja wa TARURA asije kwenye Baraza la Madiwani wakati barabara zinazojengwa wamiliki ni Madiwani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.