Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuturuhusu na sisi tuweze kuanza kutoa mchango kwenye baadhi ya maeneo yanayogusa sekta zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwanza naunga mkono hoja yake aliyoiweka mezani na maelezo ya kina kuhusu baadhi ya hoja zilizotolewa na Wabunge tutayatoa wakati wa bajeti yetu ya Wizara. Hapa niseme tu yale yaliyo ya jumla na nianze kwa haya ambayo yamesemewa kwenye michango na yamejitokeza kwenye baadhi ya maswali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na hili ambalo lilikuwa linaongelea kusuhu masuala ya upelelezi kuchukua muda, haki za watuhumiwa na watu kubambikwa kesi. Niseme kwenye jambo hili ambalo ni la msingi na linahusu haki za watu wala sisi Serikali hatuwezi tukatofautiana na ninyi Waheshimiwa Wabunge. Hata juzi Arusha kule Mheshimiwa Rais alituelekeza kati ya mambo ambayo tunatakiwa tuyafanyie marekebisho kwenye utendaji wetu wa kazi ni kuhusu masuala ya ubambikaji wa kesi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme hili ni jambo ambalo tumelichukua na tumeshaanza kulifanyia kazi. Kama kuna baadhi ya maeneo ambako bado mambo hayo yanaendelea kujitokeza yatakuwepo makosa ya kibinadamu ambayo yanaweza kujitokeza katika utekelezaji wa kazi, lakini Serikali kama Serikali kusudi lake ni kuhakikisha inalinda haki za raia wake kwa sababu ni sehemu ya haki muhimu sana ambazo Watanzania wanatakiwa kuzipata.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu upelelezi kuendelea kufanyika wakati mtu ameshafikishwa Mahakamani, hili nalo lipo kwenye utaratibu wa kisheria na si wote wanapokwenda Mahakamani wanakosa dhamana. Kwa hiyo, huwa tunaona ni vema mtu akapelekwa Mahakamani kwa sababu dhamana inakuwa wazi ili mtu aweze kupata dhamana hata kama upelelezi unaendelea. Kwa wale wanaokwama kupata dhamana yenyewe inakuwa inatokana kwa kiwango kikubwa na aina ya makosa pamoja masuala ya kiusalama.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge walilisemea kwa sauti kubwa suala hili linalohusiana na watu kulundikana magerezani huku wakiwa hawajapata ufafanuzi kuhusu makosa yao ama hatma ya makosa yao. Hata sisi kama Wizara ni jambo ambalo tunaliangalia kwa jicho la tofauti. Kwanza ni gharama kwa Serikali kuwa na watu ambao labda makosa yao yangeweza kumalizika haraka, lakini la pili ni jambo hatarishi kuwachukua watu ambao wana makosa madogo wakakaa pamoja na watu walio na makosa makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimewaambiwa hata wasaidizi wangu Jeshi la Polisi pamoja na wengine kwamba kama kuna watu ambao tunaweza tukatathmini tukajua yale waliyofanya na tukaangalia kama hayana matatizo ya kiusalama kwa wao kuwa nje, basi ni vema sana hao watu kutokuwachanganya na watu ambao wana makosa makubwa ambao wako magerezani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu taarifa za kiuchunguzi tulizozipata kuna baadhi ya watu wanapokaa na wahalifu wazoefu ama na wahalifu wenye makosa makubwa ilhali wao wakiwa na makosa madogo, wengine wanapata mafunzo ya kufanya makosa makubwa na wengine watengeneza ushirika na wale ambao wanafanya makosa makubwa. Kwa maana hiyo, tunazipokea zile hoja na tutaendelea na kuzifanyika kazi. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa sababu sekta hizi zote zinapofanya kazi kwa pamoja zinaharakisha utoaji wa haki za watu ameziangalia kuanzia Mahakama hadi Magereza pamoja na Jeshi la polisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ambayo ilizungumziwa ni kuhusu matumizi ya askari kwenye masuala ya chaguzi. Sisi kama Jeshi la Polisi na kama Wizara ya Mambo ya Ndani hatupendi kuona wananchi wetu wanaumizana kwenye masuala ya uchaguzi. Kwenye chaguzi nyingi tumeshuhudia na mara zote ninapopata fursa ya kuongea na wananchi naendelea kuwaambia ni aibu sana kwa nchi ambayo ina siasa za vyama vingi kwa zaidi ya miaka 20 lakini wananchi wake wanafanyiana fujo pale panapotokea pana uchaguzi katika eneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni dhahiri kwamba kama pana uchaguzi katika Kata A na vyama vyote vinashiriki maana yake vyama vyote vitakuwepo katika eneo hilo. Kwa hiyo, tulitarajia watu waheshimu taratibu na wanapoheshimu taratibu maana yake hapatakuwa na ugomvi katika maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara ya Mambo ya Ndani hatutavumilia kuona watu wanakatana mapanga halafu tukasema kwa sababu ni chaguzi ama ni siasa tukaacha kwa sababu tunawajibika kulinda usalama wa raia mara zote na kuwahakikishia usalama mara zote wanapotokea wana mikusanyiko ama wako katika maisha yao ya kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kwa sababu nimeisikia kengele, liliongelewa suala la kijana kule Mtwara pamoja na lile la Msikitini. Nimewaelekeza wafanye uchunguzi wa ndani ili tuweze kupata taarifa kamili na tutaendelea kuzitoa taarifa hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe tu Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge pale panapokuwepo na jambo limempata mmoja wa Watanzania tuepuke sana kuliunganisha jambo hilo na dini yake kwa sababu yanapotokea masuala ya uhalifu mtu hakamatwi kutokana na dini yake, kabila au chama chake cha siasa alichonacho bali anakamatwa kutokana na kosa alilolifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tusije tukatumia utaratibu wa kuunganisha kosa mtu alilofanya pamoja na kabila lake, dini yake au chama chake cha siasa. Ingekuwa vitu hivi havifanywi na watu wa makabila haya haya, wa vyama hivi hivi, wa dini hizi hizi basi katika maeneo mengine ambapo tunapaamini kwamba ni mahali patakatifu tusingekuwa tunapata makosa ya aina hiyo. Kwa hiyo, watu wanakamatwa kutokana na makosa waliyofanya na wala kosa alilofanya mtu lisiunganishwe na imani yake, chama chake cha siasa ama kabila lake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendelea kufafanua hivi vitu kwenye bajeti zetu za Wizara husika. Kwa muda huu, naomba kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri Mkuu iliyowekwa mezani. Ahsante sana.