Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi jioni hii nami niwe mchangiaji wa kwanza kutoa mchango wangu katika hoja iliyopo mbele yetu ya Wizara ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyetuwezesha uhai na uzima tumeonana jioni hii ya leo. Katika mchango wangu wa kwanza ninaishukuru Serikali kwa utendaji mzuri ambao wanaufanya na wanatutumikia watu wa Morogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili nichukue nafasi hii kuwapa pole sana wananchi wa Kata ya Matombo, Halmashauri ya Morogoro Vijijini na wanachama wa CCM kwa ujumla kwa kuondokewa na Diwani wetu wa Viti Maalum asubuhi hii ya leo, Mheshimiwa Zuhura Mfaume aliyetangulia mbele ya haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwape pole wananchi wangu wa Kijiji cha Kisanga Stendi, Kata ya Tununguo, Tarafa ya Ngerengere ambao siku mbili zilizopita walivamiwa na majambazi na ndugu Mbaga amefariki dunia kwa kupigwa risasi na watu wengine sita wamepigwa risasi ni majeruhi bado wapo hospitalini. Waliotangulia mbele ya haki Mwenyezi Mungu awape mapumziko mema na wale ambao wako kwenye majeruhi wapate nafuu wapone haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba nilitoa pongezi za awali lakini kuna watu wengine wanaona kwamba labda tukitoa pongezi ni kama kujipendekeza Serikalini au tunataka tuipake mafuta Serikali yetu, lakini mimi kama mwakilishi wa Morogoro Vijijini na watu wa Morogoro Vijijini tusipoishukuru Serikali hii ya Awamu ya Tano tutakuwa hatujatenda haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe ni mzoefu ni mmoja wa wakongwe nchi hii, unafahamu Morogoro ilikuwa ndiyo mji wa viwanda pamoja na Tanga, ilikuwa ni ndoto za Mwalimu Nyerere na Mwalimu Nyerere ndiye alikuwa Mbunge wetu wa kwanza Mkoa wa Morogoro, wa pili alikuwa Ndugu Kambona, tatu alikuwa Ahmed Jamal, tangu aondoke Ahmed Jamal Morogoro ilirudi nyuma kiviwanda, hapo katikati tuliyumba sana, hata vile vilivyobinafsishwa vilikuwa havifanyi kazi sawasawa.

Sasa Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa kuja kuufufua Mkoa wa Morogoro ninyi wenyewe ni mashahidi kila akipita alikuwa akisimama Msamvu ni juhudi kuwahamasisha waliochukua viwanda wavifufue, hasa vile vilivyokuwa vinafugiwa mpaka mbuzi. Pia akatutafutia viwanda vipya vitatu, tena hivyo vitatu vimekuja kwenye Jimbo langu la Morogoro Vijijini, kwa nini nisimshukuru? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kujipendekeza ni ili kupewa kiwanda kikubwa cha sukari zaidi ya kuzalisha tani laki mbili ambapo kitaajiri watu laki moja acha nijipendekeze. Kama kujipendekeza kuletewa Kiwanda cha Kuchakata Mbaazi katika Jimbo langu acha nijipendekeze, kama kujipendekeza ni kuletewa Kiwanda cha Sigara cha kutengeneza Marlboro ambayo inakwenda kuuzwa Marekani kwenye Jimbo langu acha nijipendekeze, kama kujipendekeza ni kuletewa shilingi milioni 500 Februari mwaka huu kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya elimu katika Jimbo langu acha nijipendekeze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kujipendekeza ni kuletewa zaidi ya bilioni nne kwa miradi ya maji katika Kijiji cha Fulwe - Mikese, Kijiji cha Kiziwa milioni 700, Kijiji cha Kibwaya milioni 600, Kijiji cha Nyumbu milioni 600 pamoja na Tulo-Kongwa acha nijipendekeze. Kama kujipendekeza ni kuja kuweka kambi ya ujenzi wa Standard Gauge reli ya kisasa katika Kata yangu ya Ngerengere nyumba zaidi ya 70 zinajengwa kwa ajili ya watumishi wakiondoka, acha nijipendekeze, kama kujipendekeza ni kutengeneza barabara ya kutoka Ngerengere - Maturi - Kwaba - Mkulazi mpaka Kidunda kwa thamani ya one point eight billion acha nijipendekeze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikisema hapa mengi ambayo tumefanyiwa kwenye Jimbo langu sitaki Jimbo la mtu mwingine nitajipendekeza sana kwenye Serikali hii. Kama kujipendekeza barabara ya kwenda Stieglers Gorge ipitie kwenye Jimbo langu kutoka Ubena Zomozi - Ngerengere - Tunungua mpaka Mvua acha nijipendekeze. Kama kujipendekeza ni kuletewa 1.5 billion shillings kuweka kwenye mpango kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya ambayo tuliiomba hapa Bunge lililopita acha nijipendekeze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kujipendekeza ni kujengewa kituo cha afya cha milioni 400 kwenye Kata yangu ya Mkuyuni acha nijipendekeze. Nayasema haya wenzetu hata kwenye mitandao wanapotosha sana, wanasema Wabunge wa CCM kazi yao wakifika ni kuisifia tu Serikali ya CCM kama imefanya nini. Nawaambia kama wale watu haya wanajua ni uwongo waje katika Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki, ndani ya Halmashauri ya Morogoro, Mkoani Morogoro waje wayaone haya ambayo yamefanyika, kama hawajajipendekeza na wao. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo pamoja na mafanikio ndiyo maana uongozi uko kwa miaka mitano na kila mwaka tunapanga bajeti tunakuja kuwasemea wananchi wetu Serikali inayachukua kwa kufanya maboresho kwa ajili ya kuondoa changamoto hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM katika Jimbo langu, katika Halmashauri yangu lakini nina maombi machache ndani ya Serikali yangu.

Kwanza katika yote ni barabara ya Bigwa - Kisaki kujengwa kwa kiwango cha lami, hii barabara iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi lakini ni ya muda mrefu. Kama mnakumbuka ndiyo barabara mbili tu ambazo zilichaguliwa kujengwa kwa msaada wa Serikali ya Marekani, baada ya Serikali ya Marekani kujiondoa hii barabara Serikali imesema itaichukua na bahati nzuri Mheshimiwa Rais akiwa Waziri wa Ujenzi wakati Rais wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, anakuja kutuaga katika Jimbo letu alimkabidhi kiporo hicho na aliahidi kwamba atakitekeleza.

Niwaombe sana, hii barabara uchambuzi yakinifu na usanifu wa kina umemalizika, hii barabara ni muhimu kwetu na sasa hivi umuhimu wake umeongezeka zaidi ukizingatia Serikali kupitia Wizara ya Maliasili inataka kufungua utalii kule Kusini kwenda Selous kupitia barabara hiyo. Niwaombe sana tuitengeneze barabara hii ili utalii wetu uende vizuri, lakini pia ni barabara mbadala kutoka Mjini kwenda huko Kisaki, kwenda Stieglers mpaka Rufiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia barabara hii ndiyo inakwenda Makao Makuu ya Wilaya ambayo Mheshimiwa Rais ametuhamisha kwa fedha zake na kwa amri zake sasa hivi tuko Vijijini. Ni kweli Morogoro Vijijini na Makao Makuu yetu yako Morogoro Vijijini, niwaombe sana barabara hii isiishe angalau ndani ya miaka mitano basi ianze angalau wananchi wale wawe na matumaini.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nilishukuru kuhusu ujenzi wa kiwanda chetu cha sukari katika Jimbo langu. Hakuna mazuri ambayo hayaji na changamoto, kwa sababu kiwanda hiki kitaajiri watu zaidi ya laki moja, watu wenye ajira rasmi na wasiokuwa rasmi itaongeza mahitaji ya huduma za jamii makubwa kwa muda mfupi. Kwa taarifa kiwanda hiki mashine zake zilishaagizwa, zilishaanza kutengenezwa na kitaanza kujengwa mwishoni mwa mwaka huu na kitaanza kuzalisha mwakani Septemba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaomba sana kwa sababu watakuwa ni watu wengi wanakuja kwa mara moja, tuziangalie Kata hizi za Maturi na Mkulazi kinapojengwa kiwanda kile hasa ujenzi wa kituo cha afya pamoja na shule ya sekondari ukizingatia ile Kata ya Maturi ni mpya, tumeshaanza wenyewe tumejenga madarasa mawili na tunaendelea lakini kwa ujio wa wakazi hawa wapya hatutoweza kumudu kwa mambo ya shule na vituo vya afya na zahanati kwa wakati mmoja kuwa-accommodate watu wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili pili; barabara hiyo ambayo imetengenezwa mwaka huu, niwaombe sijaiona kwenye mipango ya TARURA, barabara ni ndefu sana ina kilometa zaidi ya 80 ambayo kwa sasa tunasaidiwa na mwekezaji, lakini tukiiacha barabara hii iendelee kuhudumiwa na mwekezaji tutaongeza gharama za uwekezaji na ule uwekezaji utakuwa hauna tija au utakuwa na gharama kubwa kwa mwekezaji wetu.

Niwaombe sana Serikali muichukue barabara hii muiingize kwenye mipango yenu ili muitengeneze kurahisisha kutengeneza mazingira mazuri ya uwekezaji ule na kuwavutia watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni kwenye mkazo wa elimu. Hapa ninataka niongee Kitaifa zaidi, hapa nataka niiongelee UDOM. Serikali ipo hapa mimi ni mmoja ambaye nimepitia vyuo hivyo vyote viwili UDSM na UDOM, nimefika pale kama tunavyofahamu kile Chuo kilitakiwa kijengwe vitivo saba, vitivo viwili bado havijakamilika na Mheshimiwa Rais alishaahidi anatakiwa kukumbushwa tu, mara nyingi Mheshimiwa Dkt. John Magufuli akiahidi lazima anatekeleza, tuliona alifanya katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kwa hiyo niwaombe sana mpelekeeni salamu ili amalizie atupatie fedha pale UDOM waweze kumalizia vile vitivo viwili ili lile lengo lililokusudiwa liweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa sababu UDOM kina uwezo wa kuchukua wanafunzi 45,000 lakini mpaka sasa kimedahili wanafunzi 30,000 tu, madarasa yapo, vyumba vipo, nyumba zipo kila kitu, tatizo kubwa liko kwa wahadhiri ni wachache. Ninakuomba Waziri wa Utumishi katika mipango yako uje utuambie umewaandalia nini watu wa UDOM kwa ajili ya kuongeza watumishi (wahadhiri) ili waweze kudahili wanafunzi wengi zaidi na yale majengo yote yaweze kutumika na lengo letu pale UDOM liweze kutimia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la elimu niongelee kuhusu ubora wa elimu. Katika ubora wa elimu huu mara nyingi unashuka, matatizo yako mengi katika ngazi mbalimbali, ngazi za msingi, sekondari mpaka chuo lakini leo nataka nijikite kwenye vyuo vikuu. Elimu yetu mara nyingi watu wanasema kwamba wanatoka vyuo vikuu lakini hawaajiriki. Miongoni mwa changamoto nilizoziona ni usimamizi wa wale…….

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja.