Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia bajeti ya siku ya leo ambayo iliwasilishwa siku ya jana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kipekee kabisa kutoa pongezi, hasa kwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI pamoja na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora kwa kazi kubwa ambazo wanazifanya, kwa kweli wanastahili kupongezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niwapongeze hata watumishi wa Serikali ambao ni Katibu Mkuu pamoja na wenzake wote na wafanyakazi wote kwa ujumla. Nikiangalia kwa kipindi cha miaka miwili na nusu sasa katika Serikali ya Awamu ya Tano nimeona jinsi ambavyo Ofisi ya Rais, TAMISEMI imefanya kazi kubwa sana, hasa Mheshimiwa Waziri kuweza kupitia sehemu mbalimbali kwenye Majimbo yetu, kwenye Halmashauri mbalimbali kwa ajili ya kuangalia changamoto mbalimbali ambazo zimekuwepo kwa muda mrefu na hatimaye kuweza kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo, nikianza na suala ambalo limezungumzwa na Wabunge walio wengi, nami lazima nilisemee suala la kuwarudisha Watendaji wa Vijiji na Kata ambao walikuwa ni darasa la saba ilikuwa ni kilio kikubwa sana ambacho kimekuwepo na binafsi pia katika Halmashauri yetu takribani Watendaji 83 walikuwa wameondolewa kazini. Jambo hili wiki iliyopita nilimuona Mheshimiwa Waziri, Kepteni Mkuchika, nikamuelezea changamoto hii na akanihakikishia kwamba Serikali inaangalia namna ya kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kipekee kabisa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla kwa jinsi ambavyo suala hili wameweza kulitendea haki. Niwaombe tu hao Watendaji wafanye kazi kwa bidii ili kuweza kuleta maendeleo katika Halmashauri pamoja na wananchi wote kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika sekta ya afya katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kipekee kabisa niishukuru Serikali kwa jinsi ambavyo imeweza kufanya jitihada kubwa katika sekta ya afya. Kulikuwa na changamoto kubwa siku za nyuma, kwa sasa tumeona jinsi ambavyo Serikali inafanya kazi. Iliweza kuleta shilingi milioni 500 katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita ambazo zilikwenda kwenye kuboresha Kituo cha Afya Nzela.

Nitumie tu fursa hii kuomba sasa, katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita ina majimbo mawili, Jimbo la Busanda kwa kweli hatujapata hiyo fedha, niombe kwa ajili ya kituo cha afya Katoro ni kituo ambacho kina watu wengi sana, kina msongamano mkubwa, hata wewe mwenyewe Mheshimiwa Waziri naomba utume watu waende pale wakajionee hali halisi. Ukienda kuangalia Hospitali ya Rufaa ya Geita watu wengi wanatoka Katoro, pale ambapo wodi ya wazazi inajaa inabidi wazazi hawa wapelekwe kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Geita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nichukue fursa hii kuomba sasa TAMISEMI kupitia Mheshimiwa Waziri, ikiwezekana tuma wataalam wako wakaangalie hali halisi, lakini kikubwa zaidi tunaomba fedha zaidi ili kuweza kukiboresha Kituo cha Afya Katoro ambacho kina msongamano mkubwa sana wa watu, hatimaye basi waweze kupata huduma bora kama maeneo mengine. Vilevile ninashukuru kwa ajili ya gari la wagonjwa ambalo nilipatiwa kwa ajili ya Kituo cha Afya Katoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizi, niombe tena kwamba katika Jimbo la Busanda kuna tarafa mbili, kuna Tarafa ya Busanda ambayo haina gari la wagonjwa hata moja. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kuiomba Serikali katika Kituo cha Afya Bukoli pamoja na Gengekumi, niiombe Serikali basi iangalie, Kituo kinaitwa Kashishi na Igengekumi Serikali ione uwezekano wa kupeleka gari ya wagonjwa angalau hata gari moja kwa sasa kwa ajili ya Tarafa ya Busanda ili tuweze kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kanda ya Ziwa inaonesha inaongoza kwa vifo hivi vya akina mama wajawazito wakati wa kujifungua. Ili tuweze kupunguza vifo hivi ninaomba sasa Serikali iweze kutuletea gari ya wagonjwa ili kupeleka huduma hizi kwa akina mama. Tunajua kwamba vijijini watu hawana uwezo, pale ambapo mama anashindwa kujifungua kwenye kituo cha afya au zahanati anakuwa hana uwezo wa kukodisha gari kwenda kwenye Hospitali ya Rufaa, lakini mkiongeza magari ya wagonjwa yatawezesha kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi kwa sababu kutakuwa na uwezekano wa kusafirishwa kwenda katika Hospitali ya Rufaa ili waweze kupata huduma iliyo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya afya tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita tu tuna upungufu wa watumishi zaidi ya 200. Niliuliza swali tarehe 30 Januari, ikaonesha kabisa kwamba upungufu uliyopo ni watumishi zaidi ya 240.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitumie fursa hii katika bajeti ya mwaka huu Halmashauri yetu ikileta maombi kwa ajili ya kibali cha ajira kwa watumishi, imeomba watumishi 121 niiombe Serikali basi iweze kutupatia hivyo vibali ili watu waajiriwe tuweze kupunguza adha na matatizo na changamoto mbalimbali, hasa katika sekta hii ya afya ambayo ni ya muhimu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua juhudi za Serikali jinsi ambavyo wameongeza bajeti katika sekta hii ya afya, nina imani kubwa kwamba hizi changamoto Serikali itaendelea kuzifanyia kazi ili hatimae wananchi wetu waweze kunufaika na kuwa na afya bora. Haiwezekani kuwa na maendeleo kama afya haipo katika hali nzuri. Kwa hiyo, naiomba Serikali hasa watumishi katika sekta ya afya tuna upungufu mkubwa, iweze kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii pia kuishukuru Serikali, hasa Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kwa jinsi ambavyo imeweza kupanga mpango wa kuweza kujenga hospitali ya wilaya katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita, jambo hili nalipongeza sana. Ilikuwa ni hitaji kubwa kutokana na kwamba, iliyokuwa hospitali ya wilaya ilibadilishwa matumizi ikawa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa. Kwa hiyo, niombe sasa hizo shilingi bilioni 1.5, fedha hizi zije mara moja ili ziweze kuanza kazi kuweza kujenga Hospitali ya Rufaa katika Wilaya ya Geita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika sekta ya afya tunatambua kwamba katika Wilaya yetu, kwanza nitumie fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Mkuu wetu wa Mkoa pamoja na Mkuu wa Wilaya kwa mkakati mkubwa ambao wamejipanga kuweza kutekeleza Sera ya Taifa ya Afya, kwamba kila kijiji kiwe na zahanati, kila Kata iwe na kituo cha afya, na tayari mpango huu umekwishaanza. Kwa sababu hii niiombe Ofisi ya Rais, TAMISEMI tujipange basi kuweza kuona kwamba utekelezaji huu unaungwa mkono kwa dhati, hasa kwa kuleta vifaa muhimu, lakini vilevile na watumishi pale ambapo zahanati zitakamilika pamoja na vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nizungumzie sekta ya barabara. Tunatambua kwamba tumetunga sheria ya TARURA, TARURA kweli tunaona ipo tumeiazisha lakini bado haijaanza kufanyakazi yake vizuri, nitumie fursa hii hasa kuiomba Serikali iweze kuiongezea uwezo TARURA ili iweze kufanya kazi zake vizuri. Tunaona jinsi ambavyo barabara nyingi za vijijini asilimia kubwa zaidi ya 70 ni watu wanaishi vijijini, barabara za vijijini hazipitiki. Ninaiomba Serikali iwekeze hasa kwenye barabara za vijijini, haiwezekani tunaweza kufikia uchumi wa kati bila ya kuweza kufanikisha barabara vijijini.

Kwa hiyo, niombe Serikali kuhusu TARURA iongeze kasi zaidi na fedha ili tuone kwamba barabara za vijijini zinapitika wakati wote, hapo tunaweza kuwawezesha wananchi kuaanzisha viwanda wataweza kuuza mazao yao sehemu tofauti kwa sababu barabara zinapitika. Kwa hiyo, TAMISEMI iangalie sana TARURA ili hatimaye tuweze kuona mafanikio makubwa kutokana na kuwepo kwa barabara hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema hivi kwa sababu Jimbo langu la Busanda lipo vijijini ninaona changamoto iliyopo kubwa, barabara nyingi hazipiti. Kwa hiyo, niiombe TAMISEMI iwekeze kwenye barabara kwani ndiyo msingi wa maendeleo yetu hasa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.