Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia Wizara hii. Awali ya yote, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri ambayo kaitoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwenye suala la pembejeo. Pembejeo zenye ruzuku ya Serikali ni tatizo kubwa sana. Mkoa wa Katavi ulipokea pembejeo ambazo zilikuwa na gharama kubwa kuzidi hata zile zinazouzwa kwenye maduka binafsi. Ni jambo la kushangaza sana kwamba pembejeo zenye ruzuku ya Serikali zinakuwa na gharama kubwa kuliko hata zile zinazotolewa na Serikali. Naomba Mheshimiwa Waziri alifuatilie hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba kwenye suala zima la masoko, tuna tatizo la masoko hasa ya mazao ya chakula kwa maana ya mahindi na mpunga. Mazao haya yanazalishwa kwa wingi sana kwenye maeneo ya Mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma.
Tulikuwa tunaiomba Serikali iandae mazingira ya kuwasaidia wakulima hawa wadogo wadogo ili waweze kupata nguvu ya uzalishaji mkubwa pale wanapokuwa na masoko mazuri ya mazao yao. Tunaiomba Serikali ifuatilie na iangalie mazingira ya kuaandaa viwanda vidogo vya usindikaji kwa ajili ya mazao ambayo yatasaidia sana kutengeneza mazingira ya kuwapa masoko wakulima wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni miradi ya umwagiliaji. Tuna miradi ya umwagiliaji ambayo ilianzishwa na Serikali; upo mradi wa scheme ya Karema ambapo Serikali imetoa fedha nyingi lakini imeshindwa kukamilisha huu mradi ambao sasa unaharibika kwa sababu umechukua muda mrefu na kusababisha hasara. Tunaomba miradi ile ambayo Serikali imeanzisha iweze kutekelezwa kwa haraka ili kusaidia wananchi hasa katika shughuli za uzalishaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huo wa Karema una fedha nyingi, lakini tunao mradi wa Mwamkulu na Iloba na miradi yote hii bado haijakamilika. Tunaomba Serikali iangalie na itume fedha ili hii miradi iweze kukamilika na isije ikachukuliwa kwamba kila mradi unaoshindikana kukamilika, wale ambao ni wasimamizi wanachukuliwa hatua; kumbe tatizo kubwa sana ni ukosefu wa fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la uvuvi. Mkoa wa Katavi tunalo eneo la uzalishaji hasa kwa wavuvi wetu wa Ziwa Tanganyika. Wavuvi hawa wanafanya uvuvi ambao ni wa kienyeji. Tunaiomba sana Serikali iweze kuangalia mazingira ya kuwasaidia wavuvi wadogo wadogo. Serikali ilishatengeneza mazingira mazuri, ikajenga mwalo pale eneo la Ikola, lakini ule mwalo hautakuwa na thamani kama haujawezesha wale wavuvi wadogo wadogo. Nilikuwa naomba Serikali kupitia Wizara iwawezeshe wavuvi wadogo wadogo, wapatiwe mitaji na kuwapa zana za kisasa. Tutakapowasaidia wavuvi hawa tutakuwa tumesaidia mazingira ya kukuza uchumi kwenye maeneo husika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna uvuvi haramu ambapo kuna nyavu zinazotoka nchi jirani ya Burundi, zile nyavu ni hatari sana kwa wavuvi na kwa usalama wa Ziwa Tanganyika.
Mwenyekiti, naiomba Serikali iangalie na iweke mikakati ya kuzuia nyavu haramu ambazo zikikatikia kwenye eneo la ziwa, zile nyavu zinaendelea kuua mazao yanayotokana na ziwa lile kwa sababu zile nyavu hazifai kwa matumizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la zao la tumbaku. Zao la hili lina changamoto kubwa sana. Naiomba Serikali itafute soko lenye uhakika la kuwasaidia wakulima wa zao la tumbaku nchini. Serikali imejitahidi kutafuta masoko, lakini bado kuna matatizo ambayo wanayafanya Serikali kama Serikali. Unapoenda kutafuta soko, ukayashirikisha makampuni ambayo yananunua hapa hapa nchini, hujafanya kitu chochote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali itafute soko liwasaidie wakulima. Unapowabeba hawa wafanyabiashara ambao ndio wanaowanyonya wakulima, unaenda nao kutafuta soko, hujawasaidia, kwa sababu bado unatengeneza mazingira ya kubana lile soko ambalo linahitajika kwa wakulima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna eneo ambalo tunahitaji Serikali iingilie kati. Kuna utitiri wa fedha zinazotozwa mkulima. Tunaomba zile tozo ambazo zinamfanya mkulima akose bei nzuri ziangaliwe upya na ziweze kukokotolewa ili ziweze kuwasaidia. Ni pamoja na zile kodi za Halmashauri ya Wilaya, kuna asilimia tano ambayo sasa hivi inatozwa, tunaomba itozwe asilimia mbili na Halmashauri ibaki na asilimia tatu, nyingine ziwarudie wakulima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la mabenki, mkulima anatwishwa mzigo mkubwa sana kwa sababu ya riba kubwa sana za mabenki. Naiomba Wizara iangalie kwa karibu sana kusaida kupunguza riba ili mkulima awe na mzigo mdogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine kwenye zao la tumbaku tunahitaji mwangalie umuhimu wa kuajiri ma-classifier. Bila kuwa na classifier hatuwezi kuwasaidia wakulima wa zao la tumbaku. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la mifugo. Eneo langu lina wafugaji wengi sana na tunaomba sana muwasaidie wafugaji kwa kuwatengea maeneo. Tukitenga maeneo tutakuwa tumewasaidia wakulima/wafugaji na tunaepusha migogoro ambayo haina ulazima. Ipo haja ya kutenga maeneo na kuweza kuangalia umuhimu wa kuwapa wakulima wamiliki ardhi na wafugaji wawe na maeneo yao ili kuepusha migogoro ya mara kwa mara kati ya wakulima na wafugaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuwajengee mazingira ya kuwakopesha hawa wafugaji ili na wao wafuge kisasa. Hiyo ni pamoja na kuwapelekea huduma zile za dawa, majosho na kadhalika ili viweze kuwasaidia na waache ufugaji wa kuhamahama. Wafugaji wanafuata malisho, ndiyo maana wanatembea kila eneo, lakini kama tutawajengea miundombinu kwenye maeneo yao, hawatakuwa na ufugaji wa kuhamahama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwenye suala la ushirika. Kwenye eneo la ushirika bado tumewasahau kwenye Idara hii. Kwanza Bunge lililopita tuliazimia kwamba watakuwa na Kamisheni ya Mfuko utakaokuwa unashughulikia suala zima la ushirika. Tunapouwezesha Ushirika ndiyo tunafanya sasa wapate kuwa na uwezo wa kukagua. Leo hii ukifika kwenye Idara ya Ushirika, hawana nafasi ya kufanya jambo lolote lile kwa sababu hawana fedha za kuendesha shughuli zao.
Tunaomba mpeleke fedha kwenye Idara ili zikaimarishe Mfuko wa Ukaguzi, ni pamoja na kusaidia Shirika la COASCO ambalo linakagua ukaguzi wa ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Waziri mwenye dhamana aangalie maeneo haya ili aweze kusaidia shughuli za kilimo kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante.